2016-04-06 12:27:00

Papa asema Huruma ya Mungu ni kwa watu wote


Baba Mtakatifu Francisko katika Katekesi yake kwa mahujaji na wageni , akiwa katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro,mapema Jumatano hii, alifungua ukurasa mpya, ambamo ameanza kuizungumzia  huruma ya Mungu, akilenga moja  kwa moja  juu ya Utume wa  Kristo  katika kutimiza  ahadi  ya kumkomboa binadamu dhidi ya dhambi zake.   Maelezo ya Papa yamesisitiza kwamba, huruma ya Mungu, inayoonekana kupitia kifo na Ufufuko wa  mwanae  Yesu Kristo Msalabani, haibagui mtu.

Baba Mtakatifu Francisko aliianza Katekesi akisema, baada ya kutafakari juu huruma ya Mungu katika Agano la Kale,  sasa  na tutafakari   jinsi Yesu  alivyotumwa na Baba yake kwa ajili ya kutimiza  ahadi yake.  Moja kwa moja amemtaja  Yesu, kuwa ni huruma wa Mungu, iliyomwilishwa, kama anavyonekana katika utendaji wa maisha yake ya kila siku hapa duniani,  alitangaza upendo, kukutana na watu, kuwaponya wagonjwa, kufariji wenye huzuni na kusahaulika ,  kusamehe dhambi n.k.  Matendo ya Yesu yanaonyesha wazi kwamba alitenda kwa upendo mkuu usiokuwa na mipaka.  Ulikuwa ni  upendo safi, na ulio huru  kabisa. Upendo uliofikia kilele chake katika kujitoa  sadaka msalabani.  Haya yote yanatuonyesha  kwam ba kwa  kweli  Injili ni  Neno la Huruma,  kwa sababu Yesu mwenyewe ni Huruma.

Baba Mtakatifu  ameendelea kuyatazama maisha ya Yeus tangu mwanzo akisema Yesu alianza utume wake kwa unyenyekevu , kama ilivyoandikwa katika Injili zote nne zikishuhudia kwamba,  hata kabla ya kuanza huduma yake,  kwa unyenyekevu alijiunga katika msatari wa kwenda kubatizwa na Yohana Mbatizaji.  Hakujiweka kando kama mtu mkubwa na mwenye mamlaka, au mwenye kuhitaji huduma ya kipekee lakini alijichanganya na wengine kama mtu wa kawaida.  Katika hili, Papa anasema , linaonyesha dhamira zima ya maamuzi ya Kristo.  Unyenyekevu wa Yesu ulionekana  hata wakati wa  wakati wa kutolewa hekalu, aliwasilishwa kama mtu wa kawaida , bila  mbwembwe  za kutangazwa kwa sauti ya baragumu, au kujionyeshwa  kama ni Hakimu Mkuu, mtu mashuhuri .  Badala yake, aliishi kama mtu wa kawaida kwa  miaka thelathini  katika nchi yake ya Nazareth. Yesu alikwenda  katika Mto Jordan, pamoja na watu wengi , akajipanga  sambamba na wenye dhambi, ili abatizwe. Na hapo ndipo Baba wa Mbinguni alipomdhihirishwa kuwa ndiye  Masihi, ishara ya Roho Mtakatifu  aliyeonekana katika umbile ya njiwa juu yake na  sauti kutoka mbinguni ikasema, ” Huyu ndiye  Mwanangu, mpendwa; ninaye pendezwa nae”.

Papa amelitafakari  tukio zima la fumbo hili kubwa la upendo wa Yesu, kwa kuutazama sana msalaba , ambako Yesu aliyatoa  maisha yake sadaka kwa huruma  ya  kusafisha dhambi za dunia , dhambi zetu.  Kutoka katika msalaba wake , Yesu anatuonyesha kwamba, hakuna anayebaguliwa katika  Upendo wa huruma ya Mungu , kama alivyosema, ” Baba wasamehe  maana hawajui watendalo”.   Na hivyo kumbe juu ya msalaba wa Yesu,  hakuna sababu za kuwa na hofu katika kutambua na kukiri dhambi zetu  kwa sababu kila dhambi , kwa Sakramenti ya Upatanisho tunapata msamaha,  unaotiririka toka  msalabani  na kutufanya upya kwa neema ya huruma  yake,  iliyotupatia sisi ushindi.  Hatupaswi kuogopa dhambi zetu , kwa kuwa  nguvu ya upendo wa Msulubiwa  hajui vikwazo na kamwe haimwachi nje  anayeiungamia.

Papa ameeleza na kutoa wito kwa watu wote kwamba,   katika hii Jubilee hii ya  Mwaka Mtakatifu wa Huruma ya Mungu, ni wakati wa kukumbatia Injili kwa moyo wa shauku kubwa zaidi ,  nguvu ya Injili ya huruma yenye uwezo wa kuyabadili maisha yetu, nguvu  inayotuwezesha kuingia  ndani ya moyo wa Mungu, nguvu yenye kutuwezesha  kutoa msamaha kwa wanaotukosea na kuitazama  dunia kwa wema zaidi. Amehimiza , kwa kuikubali  Injili ya  Yesu Kristo Msulubiwa na Mfufuka,   maisha yetu yote  yanapata umbo jipya kwa nguvu ya upendo wake  wenye kutubadilisha.

Baada ya Katekesi , Papa alisalimia makundi ya watu waliokuwa wakimsikiliza kulingana na lugha zao. Katika Kundi la wanaozungumza Kiingereza , walikuwepo  mahujaji kutoka Kenya na Zimbabwe . Aliwaasa  tukiwa bado katika kipindi cha  maadhimisho ya Pasaka , na tuifungue mioyo yetu kwa Bwana Mfufuka ili kwamba kwa kuimarisha na neema zake , tuweze  kwa pamoja na familia zetu na jumuiya zetu  kushirikishana ujumbe wa  Injili ya huruma yenye kutukomboa dhidi ya mizigo ya dhamb i. Mwisho kwao wote aliwapa baraka zake za Kipapa. 








All the contents on this site are copyrighted ©.