2016-04-06 11:32:00

Hongera Dr. Magufuli kwa kudumisha maadili na utawala wa sheria!


Askofu mkuu Yuda Thaddeus Ruwaichi wa Jimbo kuu la Mwanza, anaipongeza Serikali ya awamu ya tano nchini Tanzania kwa kujikita katika kanuni maadili, maendeleo na utawala wa sheria katika mapambano dhidi rushwa na ufisadi wa mali ya umma, saratani ambayo ilikuwa imeifikisha Tanzania mahali pabaya katika masuala ya kiuchumi, kijamii na kisiasa!

Haya yameelezwa na Askofu mkuu Ruwaichi katika mahojiano maalum na gazeti la  Dail News linalochapishwa nchini Tanzania. Askofu mkuu Ruwaichi anaunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ya awamu ya tano katika mchakato wa maboresho ya maisha ya watanzania, sanjari na kujikita katika kanunu maadili, utawala wa sheria na heshima ya binadamu. Jitihada za Serikali katika kukusanya kodi zinapaswa kuungwa mkono, ili kuimarisha uchumi na kuondokana na tabia ya kuwa na uchumi tegemezi kwa wahisani wa nje.

Askofu mkuu Ruwaichi anakaza kusema, mchango wa wafadhili kutoka nje, utasaidia mchakato wa maboresho ya maisha ya watanzania wengi, hususan wanaoishi vijijini, kwa kuwa na uhakika wa umeme ili kukoleza shughuli za uzalishaji na huduma; pamoja na kuendelea kuboresha huduma za elimu na afya; mambo ambayo yanawagusa watanzania wa kawaida!

Askofu Mkuu Ruwaichi anaendelea kumpongeza Rais Magufulu na Serikali yake na kuwataka kukaza uzi ili Tanzania iweze kuheshimika kutokana na utawala wa sheria, kanuni maadili na maendeleo kwa watu wake. Mambo haya si tu kwa ajili ya watumishi wa serikali, bali watanzania wote katika ujumla wao, wanapaswa kufuata sheria na kanuni maadili. Kutokana na udhibiti wa ukusanyaji kodi, Pato Ghafi la Taifa, GNP limeongezeka kwa asilia 7% katika miezi ya hivi karibuni!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.