2016-04-03 12:11:00

Kuna kilio kikubwa cha ukosefu wa huruma na amani duniani!


Baba Mtakatifu Francisko ameadhimisha Jumapili ya huruma ya Mungu, tarehe 3 Aprili 2015 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na kuhudhuriwa na umati mkubwa waamini wenye Ibada kwa huruma ya Mungu. Katika mahubiri yake, Baba Mtakatifu amesema, Injili ni kitabu cha huruma ya Mungu ambacho waamini wanapaswa kukisoma na kutafakari yaliyomo! Injili ya huruma ya Mungu ni kitabu ambacho kiko wazi kinachokumbatia matendo ya upendo na ushuhuda wa huruma na kwamba, kila mwamini anapaswa kushiriki kuandika kwenye kurasa za Injili ya huruma kwa kumwilisha matendo ya huruma: kiroho na kimwili!

Huu ndio mtindo wa maisha ya Kikristo unaowapelekea wengine upendo na faraja ya Mungu katika maisha yao, kama mwendelezo wa utume uliofanywa na Kristo kwa kuwashirikisha wafuasi wake waliokuwa na hofu, huruma ya Baba wa mbinguni na kuwapatia zawadi ya Roho Mtakatifu anayesamehe dhambi na kuwapatia waamini furaha ya maisha! Mitume wa Yesu, waliogopa, kiasi hata cha kujifungia ndani, lakini Yesu anawataka watoke huko walikojificha, ili waweze kwenda ulimwenguni kutangaza ujumbe wa msamaha, mwaliko kwa waamini kujitoa katika ubinafsi wao, tayari kumkaribisha Yesu!

Baba Mtakatifu anakaza kusema, Yesu kwa njia ya upendo aliweza kuingia ndani hata pale milango ilipokuwa imefungwa kwa dhambi, kifo na hivyo kukosa maisha ya uzima wa milele. Yesu anawataka wafuasi wake kufungua malango ya mioyo yao, tayari kuwatuma kwenda ulimwenguni kutangaza na kushuhudia nguvu ya upendo wa Mungu inayoponya na kukumbatia. Mbele ya macho ya walimwengu, kuna binadamu aliyejeruhiwa, mwenye hofu; anayebeba makovu ya machungu ya maisha pamoja na kukosa uhakika wa maisha.

Kuna kilio kikubwa cha ukosefu wa huruma na amani, kumbe, kama vile Baba alivyomtuma Yesu, ndivyo waamini pia wanavyotumwa na Yesu ulimwenguni! Kila ugonjwa unaweza kupata tiba ya huruma ya Mungu, kwani huruma hii inataka kujimwilisha katika hali ya umaskini; ili kuwaokoa wale wote wanaoendelea kugandamizwa chini ya kongwa la utumwa mamboleo. Huruma hii inataka kutua katika donda la kila mwamini, ili iweze kuliganga na kuliponya. Dhana ya kuwa ni Mitume wa huruma ya Mungu, maana yake ni kugusa na kumfariji Yesu anayeendelea kujionesha katika miili na nyoyo za watu.

Kwa kutibu na kuganga madonda haya wanamtangaza Yesu aliye hai na kuwasaidia wengine kuguswa na huruma yake kiasi hata cha kumtambua kuwa ni Bwana na Mungu kama alivyoungama Mtakatifu Tomaso. Huu ndio utume ambao waamini wamekabidhiwa. Ni wajibu wa kujenga na kudumisha utamaduni wa kusikiliza kwa makini na kuelewa; kwa kuendelea kutangaza na kuandika Injili ya huruma ya Mungu katika uhalisia wa maisha; kwa kuwatafuta waliopotea kwa uvumilivu na uwazi kama Wasamaria wema wanaotaka kuonesha ukimya na upendo kwa jirani; wahudumu wakarimu na wenye furaha wanaopenda upeo bila kudai malipo!

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kusema, amani ni zawadi ambayo Kristo Mfufuka aliwapatia wafuasi wake, ni amani ambayo pia watu wa nyakati hizi wanaiongojea kwa hamu! Hii ni amani inayobubujika kutoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu; amani ambayo imeshinda dhambi, kifo na woga! Hii ni amani inayowaunganisha watu badala ya kuwagawa! Amani inayojikita katika ukarimu na upendo; amani inayofuta machungu ya maisha na kuwezesha matumaini kuchipua tena. Amani ni kielelezo cha msamaha unaotolewa na Mwenyezi Mungu, mwaliko kwa Kanisa kuwa ni chombo cha amani, dhamana ambayo limepewa na Kristo Mfufuka siku ile Pasaka. Wakristo ni vyombo vya upatanisho, msamaha na mashuhuda wa upendo na huruma ya Mungu.

Baba Mtakatifu anasema upendo wa Mungu wadumu milele, ingawa kuna nyakati za majaribu na kukata tamaa, lakini waamini wanapaswa kukumbuka kwamba, daima Mwenyezi Mungu yu pamoja nao na kamwe hawezi kuwaacha pweke! Baba Mtakatifu anamshukuru Mungu kwa upendo huu usiokuwa na kifani, anawaalika waamini kuendelea kuchota huruma ya Baba, ili kuwapelekea walimwengu, lakini kabla ya yote, waamini waombe neema ya kuwa na huruma, ili kueneza mahali pote nguvu ya Injili!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.