2016-03-22 08:32:00

Serikali ya Tanzania kuendelea kuikagua Bandari, hadi kieleweke!


Waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa amemuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali aende Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ili akague taarifa za mapato ambazo zilikuwa zikilipwa na mawakala wa forodha na bandari kupitia benki ya CRDB lakini hazionekani kwenye mifumo ya benki. Ametoa agizo hilo Jumatatu, Machi 21, 2016) wakati akizungumza na mamia ya mawakala wa forodha na bandari waliohudhuria mkutano aliouitisha ili kusikiliza kero zinazowapata katika utendaji kazi wao.

Akizungumza na mawakala hao kwenye ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu alisema kuna dalili za kutupiana lawama baina TPA na CRDB kuhusu malipo yaliyikuwa yakifanyika benki halafu fedha hazionekana na wakala anaidaiwa kuwa hajalipia mzigo wakati alishaulipia.  “Kimsingi bado liko tatizo baina ya Mamlaka ya Bandari pamoja na Benki ya CRDB. Naona kila mmoja hapa anamkana mwenzake. Nitamtuma CAG ili akafanye ukaguzi wa kina ili tujue ni nani kati yao amehusika na upotevu wa fedha,” alisema huku akishangiliwa na mawakala hao.

Alimwagiza pia Kaimu Mkurugenzi wa Bandari, Eng. Aloyce Matei aandae dispatch zote walizotumia kupokelea malipo za kuanzia mwaka 2015 na ikibidi aandae za kuanzia mwaka 2014 ili CAG anapozopitia aweze kupata picha halisi. Vilevile, Waziri Mkuu alimwagiza Eng. Matei kuhakikisha wananunua mashine ya photocopy ili iwekwe kwenye chumba cha kupokelea stakabadhi za malipo ya benki (bank pay in slip) ili mteja anapoleta nakala ya benki aweze kutolewa photocopy na kubakia na nakala ya malipo aliyofanya, Waziri Mkuu alisema Serikali inatambua bandari ni eneo nyeti katika kuinua uchumi na mapato ya nchi lakini pia ni eneo muhimu katika kutengeneza ajira. “Ninapenda niwahakikishie kuwa bado tutaendelea kukagua bandari hadi pawe safi. Hii bandari ni yenu na mtafanya kazi kama kawaida,” alisema.

Mapema, akizumgumza kwa niaba ya mawakala hao, Rais wa Chama cha Mawakala wa Forodha nchini Tanzania (TAFFA), Bw. Stephen Ngatunga alieleza matatizo mbalimbali ambayo wao kama mawakala wa forodha wamekuwa wakikumbana nayo kuanzia ulipaji, utoaji wa mizigo na kuitaka Serikali iongeze nguvu katika kuikabilia sekta hiyo. Alizikosoa baadhi ya sheria ambazo zinaruhusu wamiliki wa bandari kavu kumiliki pia makampuni ya uwakala wa forodha, sheria kadhaa zinazochangia kukwamisha utoaji wa mizigo bandarini, ukaguzi hafifu wa kwenye scanner na uwepo wa vituo vinane vya mizani kuanzia Dar es Salaam hadi Tunduma ambavyo vimegeuka kuwa kero kwa wasafirishaji wa mizigo kwenda nchi jirani.

Wakati huohuo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani amesema Serikali imeamua kuyafungulia makampuni zaidi ya 150 ambayo yalikuwa yamefungiwa kufanya kazi za uwakala wa forodha kutokana na madai ya kuhusishwa na ukwepaji wa kodi. “Hapa tumegundua kuwa wote siyo wasafi iwe ni mawakala, benki ama bandari. Mkurugenzi wa Bandari, kuanzia leo watu hawa waruhusiwe waanze kufanya biashara lakini nyaraka za nyuma zisiguswe hadi CAG atakapokamilisha uchunguzi wake,” alisema kuibua kelele za shangwe kwenye ukumbi huo.

Na Ofisi ya Waziri Mkuu,

Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.