Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Haki na amani, Kardinali Peter Turkson, Jumatatu hii alitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Michaeli cha Toronto, ambamo amezungumzia juu ya waraka wa Papa Francisko wa” Laudato Si”chini ya Hoja ya Maendeleo.Hotuba ya Kardinali Turkson, ililenga hasa katika maana ya kweli ya maendeleo ya kijami, akianisha na waraka huo, ambao unaonyesha haja ya kufanya mapitio ya kina kwa sera zilizopo za maendeleo, ili kweli, watu wote wafanikishwe kusonga mbele kimaendeleo na wakati huohuo kudumisha uhai kwa viumbe wote.
Kardinali pamoja na kutambua maendeleo yaliyoletwa na viwanda, pia ameonyesha kujali matokeo mengine hasi yenye kuathiri maisha ya binadamu na viumbe. Amelaumu mtazamo finyu katika teknolojia wenye kupunguza thamani ya viumbe na kufanya kama vile ni bidhaa au vitu vya kawaida, kwa saababu za uroho wa kutafuta faida binafsi na bila kuzingatia maadili. Katika hotuba yake amesisitiza kwamba, juhudi zote za maendeleo ni lazima kuweka kipaumbele cha kwanza katika kuhifadhi mazingira ya asili kwa ajili ya vizazi vya sasa na baadaye na pia kudumisha maadili ya msingi ya kijamii.
Ameendelea kufafanua kuwa katika waraka huu wa ”Laudato Si”, Papa Francisko , ameonyesha kuhofia uharibifu dhahiri wa mazingira leo hii huku akitaja jukumu la binadamu katika kudumisha viumbe. Na kwamba Papa Francisko ametaka uwepo wa ukomo katika nyenzo za maendeleo , kama pia ilivyoelezwa na Mtakatifu Yohana Paulo II katika waraka wake uliotathmini uwiano wa maendeleo. Baba Mtakatifu Francisko, amejadili umuhimu ikolojia katika nafasi ya bindamu duniani na uhusiano wa binadamu na mazingira yake , akitoa wito kwa watu wote kutenda na kufungua milango yote ya majadiliano kwa uaminifu. Kardinali Turkson ameonya kwamba, nia Papa Francisko katika waraka huu si kuzorotesha maendeleo, lakini maendeleo ya teknolojia na uchumi ni lazima vilenge katika kuwa na ulimwengu ulio bora na mshikamano wa hali ya juu katika maisha.
Na alikumbusha kwamba, dunia yetu ina watu wengi wenye kuwa na tamaduni mbalimbali, na hivyo watu huishi katika mitindo mbalimbali ya kimaisha. Na alikumbusha kwamba, ardhi ni zawadi kutoka kwa Mungu kwa wabtu wote wakiwemo watu asilia ambao wameipokea toka kwa mababu zao. Kwa hiyo si halali watu wa jadi kulazimishwa kuondoka katika maeneo kwa sababu za kupisha maendeleo . Amesema kuna haja ya kufanya mabadiliko makubwa katika njia za uchumi wa dunia ili kusiwe na binadamu anayedhulumiwa kwa saabu za Maendeleo. Kanisa daima upande wake, pamoja na kuomba msamaha kwa makosa lililofanya siku za nyuma, pia linatumaini kwa ajili ya uponyaji, kutafuta njia mpya za kufanya kazi pamoja ili dunia iwe kweli ni nyumbani pa watu wote.
All the contents on this site are copyrighted ©. |