2016-03-10 09:00:00

ACERAC yaomba sura ya haki na maridhiano katika Mkoa wa Afrika Kati.


Baraza linalo waunganisha  Maaskofu Katoliki katika Mkoa wa Afrika Kati( ACERAC) limeomba amani, maelewano na umoja wakati wote wa michakato ya uchaguzi wa Rais, kipindi kinachopita sasa katika nchi nyingi za mkoa huo.  Baraza hilo huunganisha  Maaskofu Katoliki  kutoka  Cameroon, Congo Brazzaville, Gabon, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad, Guinea ya Ikweta. Habari inabaini , ombi la  ACERAC , lilitolewa mwishoni mwa  Mkutano wa Baraza hilo,  uliofanyika mjini Brazzaville, mji mkuu wa Jamhuri ya Kongo.

Taarifa tokea baraza hilo inaendelea kusema,  Maaskofu,wamepokea kwa  mikono miwili na shukurani nyingi  kwa mwenendo wa amani uliyoonekana katika uchaguzi wa hivi karibuni katika Jamhuri ya Afrika ya Kati na wamemshukuru Papa Francisko , kwa mchango wake alioutoa kwenye mshikamano wa kitaifa , wakati wa ziara yake ya mwezi  Novemba mwaka jana. ACERAT,  inahimiza  juhudi hizi zilizofanyika Car pia iwe ni somo kwa mataifa mengine ya Afrika Kati. Na wameonyesha kujali hali za wasiwasi na vitisho vinavyojionyesha katika baadhi ya mataifa kwa kadri siku za uchaguzi zinavyokaribia. Wameendelea kuomba ujasiri wa kushinda changamoto zinazowakabili kwa njia y amani na maelewano badala ya kutumia vurugu. Wameonyesha pia kutambua kwamba, kuna matatizo yanayokera raia , mfano tatizo la ukosefu wa ardhi na mgogoro wa kiuchumi na kifedha, na  hali zingine zenye kusababisha maisha magumu kwa watu wengi wakati wachache kati yao wakineemeka na utajiri wa  kitaifa.  

Pamoja na matatizo hayo , bado ni muhimu kuandaa uchaguzi wenye kuheshimu demokrasia na sheria , kama uhakika wa kuwa na usawa na fursa ya wote kushiriki  kama haki yao ya  kikatiba.  Kwa hili, wamekumbusha  umuhimu na haja ya kuangalia maslahi ya umma na kukuza manufaa ya wote,. Hivyo wameomba amani, umoja na maelewano kwa  watu wote, wake kwa waume katika Mkoa wa  Afrika ya Kati na majirani zake.  








All the contents on this site are copyrighted ©.