2016-02-10 12:22:00

Ujumbe wa Kwaresima kutoka kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania 2016


Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Kwaresima kutoka kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwa Mwaka 2016. Katika ujumbe huu, Maaskofu wanachambua kwa kina na mapana huruma ya Mungu, ufunuo wa huruma ya Mungu kwa binadamu; Kanisa na huruma ya Mungu hapa kwa namna ya pekee Maaskofu wanakazia wajibu wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu, Umuhimu wa kupokea Sakramenti za Kanisa, Matendo ya huruma: kiroho na kimwili; Bikira Maria Mama mwenye huruma na mwisho wanahitimisha ujumbe huu kwa kuhimiza toba na wongofu wa ndani; upendo wa Kristo na wajibu wa waamini, ili kweli waweze kuwa ni mashuhuda na vyombo vya huruma ya Baba wa mbinguni!

UTANGULIZI

Fadhili za Bwana nitaziimba milele (Zab 89:1)

Wapendwa Mapadri, Watawa, Waamini Walei na watu wote wenye mapenzi mema: “Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana wetu Yesu Kristo”(1Kor 1:3). Tukiwa bado tunaendelea kuiishi tafakari ya zawadi ya maisha ya familia na maisha ya wakfu ya watawa, sisi Maaskofu wenu tunawandikieni barua yetu ya kusindikiza tafakari yetu ya mfungo wa Kwaresima. Tunaungana na Kanisa zima kutafakari juu ya fumbo la mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo, fumbo lililo kielelezo dhahiri cha huruma ya Mungu kwa wanadamu wote. Kama mjuavyo, tangu tarehe 08 Desemba 2015 Baba Mtakatifu Francisko alifungua rasmi Jubilei ya pekee ya Huruma ya Mungu itakayoendelea mpaka tarehe 20 Novemba 2016, siku ya Sherehe ya Bwana wetu Yesu Kristo Mfalme. Tumependa tafakari ya Kwaresima ya mwaka huu iendane na wazo la Jubilee hii kwasababu huruma ni “daraja linalomuunganisha Mungu na mwanadamu,na kufungua mioyo yetu katika tumaini la kupendwa daima licha ya ukosefu wetu”1. Kwa kuwa Mungu Baba yetu ametupenda na kututunza yatupasa sisi watoto wake kuhurumiana kama Baba yetu alivyo na huruma kwetu.

SURA YA KWANZA

HURUMA YA MUNGU

Katika sala ya ufunguzi ya Dominika ya ishirini na sita ya mwaka tunasali hivi: “Ee Mungu, wewe unaonyesha enzi yako kuu hasa kwa kusamehe na kutuhurumia”. Kuhurumia na kusamehe ni matendo ya Mungu ambaye ni mwenyezi. Na kimsingi Mungu ni huruma yenyewe. Katika Maandiko Matakatifu Mungu wetu anatambulika kuwa ni “Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli, mwenye kuwaonea huruma watu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe” (Kut 34:6-7). Huruma yake kwa viumbe wake haina mipaka. Mungu anawaonea huruma wanadamu “si kwa sababu wanamjua, bali ili wamjue; wala si kwa sababu ni wanyofu, bali ili wapate kuwa wanyofu.”2 Na huruma yake ni mada inayokutwa katika marefu na mapana ya Maandiko Matakatifu ikidhihirishwa kwa namna mbalimbali: kwa njia ya maneno yake, matendo yake, ishara na mifano mbalimbali.

Jicho lake li kwao wamchao

Mtunga zaburi anatufundisha kuwa jicho la Bwana lililo kwao wamchao kuwa ni Mungu mwenye kujua yote, mwangalifu na mwenye ulinzi wa daima (Zab 33:18). Pamoja na mwanadamu kumuasi Mungu mara kwa mara, jicho lake linabaki juu ya kiumbe wake likiendelea kumlinda, kumtunza na kumwalika aache njia mbaya apate kuishi: “Walakini jicho langu likawahurumia nisiwaangamize kabisa wala sikuwakomesha kabisa jangwani” (Ez 20:17).

Hutufariji mfano wa mama kwa mwanae

Manabii Isaya na Hosea wanafafanua huruma ya Mungu kwa lugha ya picha ya mama anayemfariji mwanae. Nabii Isaya anatueleza kuwa ingawa mama anaweza kumsahau mtoto wake anyonyae, Mungu kamwe hatatusahau, na kwa sababu hiyo amemchora kila mmoja wetu katika viganja vyake ili kumtazama na kumtunza daima. “Je, mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyae, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kumsahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu, kuta zako ziko mbele zangu daima” (Isa 49:15-16). Nabii Hosea anatuletea picha ya Mungu wetu mwenye huruma kwa sura ya Mlezi mwenye uvumilivu mkubwa kwa mwana anayekosea tena na tena(Rej. Hosea 11:1-8).

Hutulinda kama Tai alindavyo watoto wake

Ulinzi wa Mungu kwa mwanadamu unaelezwa kwa mfano wa tai anayelinda watoto wake. Hujenga kiota, huwafunika na kuwachukua kwa mbawa zake; “Mfano wa Tai ataharikishaye kiota chake, na kupapatika juu ya makinda yake; alikunjua mbawa zake, akawatwaa, akawachukua juu ya mbawa zake” (Kumb 32:11). Ndivyo Mungu mwenyezi alivyo kwa wana wake. Mwanadamu akitambua huruma ya Mungu isiyo na mipaka hujaribu kutumia lugha yake isiyojitosheleza,ili kueleza jinsi anavyopata malezi, kinga na matunzo bora na ya uhakika.Kanisa linatufundisha kuwa “baada ya dhambi ya Israeli aliyejitenga na Mungu na kuabudu ndama ya dhahabu, Mungu anayasikiliza maombi ya Musa na anakubali kutembea kati ya taifa lisiloaminifu akionyesha hivyo upendo wake.”3 Hivyo Mungu wetu daima anadhihirisha upendo wake usio na mipaka kupitia tendo la huruma yake kwa kuwahurumia wanadamu wote. Hata hivyo ingawa “Mungu alituumba bila sisi, lakini hakutaka kutuokoa bila sisi. Kupokea huruma yake hatuna budi kukiri makosa yetu. Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo ndani mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”

SURA YA PILI

UFUNUO WA HURUMA YA MUNGU KWA MWANADAMU

Mungu alimuumba mwanadamu katika hali ya neema ya utakaso. Hata hivyo mwanadamu hakubaki katika hali hiyo, alivunja amri aliyopewa na Mungu na kutaka kufanya alichotaka na siyo alivyotaka Mungu. Ingawa Mungu alimwadhibu mwanadamu kwa kosa lake, bado alimhurumia. Kwanza alimwahidi mwanadamu kumletea mkombozi. Mungu anamwambia adui wa mwanadamu, shetani, akisema “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa na wewe utamponda kisigino” (Mwa 3:15). Kwa maneno hayo Mungu aliahidi kuwaletea wanadamu Mwanae ili awakomboe na dhambi zao. “Hatua hiyo ya kitabu cha “Mwanzo” imeitwa “Injili ya kwanza” kwa sababu inatangaza kwa mara ya kwanza Masiha na Mkombozi, mapambano kati ya shetani na mwanamke na ushindi wa mwisho wa mzao wake.” Utekelezaji wa ahadi hiyo ya Mungu umedhihilika katika nafsi ya Yesu Kristo, Mwana pekee wa Mungu, aliye Mungu nafsi ya pili ya Utatu Mtakatifu. Katika masimulizi ya historia ya wokovu, Agano la Kale linatusimulia jinsi Mungu alivyojifunua kwa mwanadamu hatua kwa hatua kuwa ni mwenye huruma.

Kwanza Mungu aliandaa taifa la Israeli kwa njia ya Mababu wa taifa hilo, ili toka taifa la Israeli Mungu afahamike kwa mataifa yote, na toka taifa hilo atokee mkombozi. Alimwita Ibrahimu na kwa ahadi zake kwa Isaka na Yakobo aliweka Agano na taifa la wana wa Yakobo mlimani Sinai baada ya kuwatoa utumwani Misri akijitambulisha kuwa yeye ni “Mungu mwingi wa huruma mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli” (Kut 34:6). Kwa njia ya vivywa vya manabii wake, Mungu alinena na watu wake akijifunua kwao. Aliwapa ujumbe wake, na mwongozo wa maisha. “Maana unabii haukuletwa popote kwa mapenzi ya mwanadamu bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu”(2Pt 1:21). Hivyo “matokeo (Kujionyesha kwa Mungu) yanaangaza njia ya ahadi, kutoka mababu hadi Musa na kutoka Yoshua mpaka maono yanayoanzisha utume wa manabii wakubwa”. Ingawa mwanadamu alionekana kumkosea Mungu tena na tena; bado Mungu aliendelea kumhurumia. Mara nyingi mwanadamu alimuasi Mungu na kuvunja uaminifu wa Agano alilofanya na Mungu. “Maana historia yote ya binadamu imejaa mapambano magumu dhidi ya nguvu za giza. Mapambano haya yalianza tangu mwanzo wa dunia, nayo yataendelea, asemavyo Bwana, mpaka siku ya mwisho. Binadamu akiwa katika vita hivi, lazima apambane bila kukoma, ili aweze kuambatana na mema; wala hataweza kuufi kia umoja wake wa ndani, bila juhudi kubwa, pamoja na msaada wa neema ya Mungu.”

Kristo Mwana wa Mungu alizindua nyakati za Agano jipya. Kwa tendo la umwilisho wake, Mwana wa Mungu alifanyika mtu kwaajili ya kuifi kisha kwa wanadamu huruma ya Mungu katika ukamilifu wake na kumpatanisha mwanadamu na Mungu. Kwa njia hii ya huruma kuu ya Mungu mwanadamu anaalikwa kuutambua na kuupokea upendo huu mkuu wa Mungu, kupitia Kristo aliye kielelezo chetu cha utakatifu na anayetufanya washiriki wa tabia ya uungu. Kristo, akifungua utume wake,ananukuu kitabu cha nabii Isaya akisema, “Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri masikini habari njema, amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa” (Lk 4:18-19/Isa 61:1-3). Tangazo hilo liliambatana na mafundisho, matendo yake na miujiza mbalimbali,jambo lililofanya sura ya huruma Mungu ijidhihirishe na upendo wa Mungu ushikike. Hali inayofanya kila mtu, katika kila hali na nafasi, aonje kukubalika na kupendwa na Mungu ambaye upendo na huruma yake havifungwi na hali zetu. Huo unabaki kuwa utume wa Kanisa, utume wa kueneza huruma na upendo wa Mungu: “Yesu aliwaita watu kumi na wawili wamfuate kwa karibu zaidi na washiriki katika kazi yake. Yesu aliwapa watu hao jina mitume. Walishuhudia huduma mbalimbali zilizofanywa na Yesu, walihifadhi akilini mwao yale waliyoona na kuyasikia.

Katika mafundisho yake Yesu akifuatwa na makundi kwa makundi, aliwalisha wenye njaa, aliwaponya wagonjwa, aliwafukuza pepo na kuwafufua wafu”9. Huu unaendelea kuwa utume wa kila mwanakanisa, maana, kama anavyofundisha Baba Mtakatifu Francisko, “Yesu anathibitisha kwamba huruma siyo tendo la Baba tu, bali ni kigezo cha hakikisho la wana wake kweli. Kwa kifupi tunaitwa kuonesha huruma kwasababu tumeonewa huruma kwanza”10. Huruma ya Mungu kwetu inaonekana pia katika tunza yake kwetu, akitulinda na kutuneemesha, ili tuishi kwa furaha na amani. Kilele cha ufunuo wa huruma ya Mungu kwa mwanadamu ni tukio kuu la fumbo la Pasaka. Tukio la mateso, kifo na ufufuko wa Kristo ni kilele cha tendo la huruma na upendo wa Mungu kwetu. Yesu Kristo alitoa nafsi yake iwe fi dia ya dhambi. Kwa sababu hiyo kila mkosefu amechangia katika mateso na kifo cha Yesu Kristo, na mateso, kifo na ufufuko wa Kristo ndio sababu ya wokovu wa kila mkosefu. Hivyo sura halisi ya upendo wa Mungu ni huruma yake, na huruma “ni jina la pili la upendo.”11

SURA YA TATU

KANISA NA HURUMA YA MUNGU

Kanisa kama Taifa na Familia ya Mungu ni wakala pia wa upendo na huruma ya Mungu. Huruma sio tu namna ya kutenda ya Mungu bali ni kigezo cha kutambua nani ni wana wa Mungu kweli. Sura ya Mungu anayehurumia inapaswa kuwa ndiyosura halisi ya Kanisa linaloendeleza fumbo la Pasaka la Kristo. “Kanisa linakiri huruma ya Mungu, Kanisa linaiishi katika mang’amuzi yake, na tena katika mafundisho yake, likimtafakari Kristo daima, likijikusanya kwake, katika maisha yake na Injili yake, katika msalaba wake na ufufuko wake, na katika fumbo lake zima…Kanisa huwaleta watu karibu na kiini cha huruma ya Mwokozi, ambaye ndiye mdhamini na mgawaji wa huruma hiyo.”12 Aidha Kanisa linapokiri juu ya huruma ya Mungu linatangaza pia kuongoka na kumgeukia Mungu. Kumgeukia Mungu ni matunda ya kujitambua na kung’amua huruma ya Mungu.“Yesu Kristo ametufundisha kwamba mtu hapokei tu na kuizoea huruma ya Mungu, bali anaitwa pia kuwatendea wengine huruma.”13 Kristo ametufundisha hilo katika hotuba yake ya mlimani (Rej. Mt 5:1-12), mfano wa mwana mpotevu (Rej. Lk 15:11-32) na zaidi ya yote kwa mateso na kifo chake msalabani. Kristo anatufundisha kuwa yale tunayowatendea wengine hasa waliowanyonge, tunamtendea yeye mwenyewe (Rej. Mt 25:31- 40) na tunayoacha kuwatendea wengine tunaacha kumtendea yeye mwenyewe (Mt 25:41-46).

Sisi Maaskofu wenu tunapenda kuwakumbusha tena mambo yafuatayo, ili kwa pamoja tuweze kutangaza huruma ya Mungu na kujipatia sisi wenyewe huruma yake.

Wajibu wakutangaza Habari Njema

Kwa ubatizo wetu, sisi sote tunashiriki kazi ya unabii ya Kristo. Wajibu wetu ni kumtangaza Kristo popote katika mazingira yetu ili afahamike, apendwe na kufuatwa. Tunawatia shime wale wengi wenu ambao mnaonyesha juhudi kubwa ya kujifunza imani yetu na kuwashirikisha wengine. Wahudumu wa Daraja Takatifu, Watawa na Makatekista wanafanya jitihada kubwa ili kumpeleka Kristo na ujumbe wake wa huruma kwa watu. Hata hivyo bado inaonekana kuwa jitihada hizo si kubwa katika ngazi ya familia. Bado watoto na vijana wengi hawapati mafundisho ya msingi na ya kawaida toka kwa wazazi au walezi wao. Wazazi na walezi hawakai na watoto wao na kuwaeleza habari njema ya Kristo Bwana wetu. Tujue kuwa Mapadre, Watawa na Makatekista wetu bado ni wachache, hawawezi kumfikia kila mmoja kwa wakati na kwa kina.

Tunapenda kuwaalika waamini wote; wazazi na walezi kutumia muda wenu nyumbani kuuishi na kuwafundisha watoto ujumbe wa Kristo. Tukumbuke kuwa familia ni jumuiya na kanisa la kwanza ambamo misingi ya imani na ya utu inajengwa. Hali ya jumuiya hiyo, huathiri jumuiya zingine kubwa. Tabia za mwanzo za wanadamu zinajengwa katika familia,maana “mtoto umleavyo ndivyo akuavyo”. Wazazi na walezi wanawajibu wa kuwapatia watoto wao elimu na kuwarithisha imani na maadili (Rej. Kumb 6:20-25). Watoto wanawajibu wa kuwaheshimu wazazi wao, kuwatunza wazazi wao, hasa uzeeni, katika ugonjwa na ulemavu, kuwatii na kuwaombea wazazi, na kuwazika wakifa (Rej. Ybs 3:1-6). Wazazi jengeni mahusiano bora ili kuimarisha familia zenu. Salini pamoja, mfanye kazi pamoja kwa juhudi na kwa maarifa,mkipendana na kuheshimiana(Rej. Efe 5:22-25). Jitahidini kuishi maagano ya ubatizo wenu ili kutoa mfano bora wa maisha ya kikristo kwa watoto na wale ambao bado hawajamfahamu Kristo ili wapate kumfahamu. Tukiyaishi haya tunakuwa tunadhihirisha huruma na upendo wa Mungu unaoendelezwa katika maisha yetu ya kila siku. Huruma na upendo huenda pamoja.

Kupokea Sakramenti za Kanisa

Kristo Bwana wetu, ametuachia sakramenti ili tukizipokea vema tujipatie neema zake. Sakramenti ni kielelzo kingine cha upendo na huruma ya Mungu inayobubujika kutoka katika Fumbo la mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Kanisa, ambalo ni mama na mwalimu, linawapokea katika familia ya wanakanisa watu wote kwa njia ya Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu. Kwa njia ya Kanisa na Sakramenti za Kitubio na mpako mtakatifu Kristo ananyoosha mkono wake wa uponyaji kwa wagonjwa wa mwili na roho. Kristo ameweka pia Sakramenti za Ndoa na Daraja Takatifu kwa ajili ya kutoa huduma. Tunawahimiza wapendwa wakristo kuzishiriki kwa ari kubwa Sakramenti hizi za Kanisa inavyostahili ili kujipatia neema za Mungu. Huruma ya Mungu inajidhihirisha katika Sakramenti za Kristo katika Kanisa.

Tukumbuke kuwa, “mwaliko wa Kristo wa wongofu unaendelea kusikika katika maisha ya wakristo. Wongofu wa pili ni kazi ya kudumu ya Kanisa lote linalowakumbatia wakosefu kifuani mwake, nalo ni takatifu na papo hapo linaitwa kujitakasa na kufuata daima njia ya toba na kujifanya upya. Bidii hii ya kuongoka si kazi ya kibinadamu tu. Ni msukumo wa moyo uliovunjika, unaovutwa na neema, kuitikia mapendo yenye huruma ya Mungu aliyetupenda sisi kwanza.”14 Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu hutuwekea misingi yote ya maisha ya kikristo.

Tukiwa bado katika safari hapa duniani tunaelemewa na mateso, magonjwa, na dhambi. Kristo Mganga wetu hutusamehe dhambi na kuturudishia afya kwa sakramenti za Kitubio na Mpako Mtakatifu wa wagonjwa. Hatimaye sakramenti za Daraja takatifu na Ndoa zinatupatia nafasi ya kutoa utume wakuhudumia ujenzi wa Taifa la Mungu.Tukiziishi Sakramenti hizi tunakuwa tunadhihirisha huruma na upendo wa Mungu unaoendelezwa katika maisha yetu ya kila siku kupitia sakramenti za Kanisa. Huruma na upendo huenda pamoja.

Matendo ya huruma

“Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma”. Kristo Bwana wetu anatufundisha na kututaka kuwatendea wanadamu wote kwa mapendo na huruma. “Kama Baba yenu”. Hiki ndicho kipimo. Mungu ndiye kipimo cha upendo na huruma ambao wanadamu wanaalikwa kuudhihirisha katika maisha yako. Tunapowatendea wenzetu matendo ya huruma tunamtendea Kristo mwenyewe anayetueleza uwepo wake kwao. “Kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitenda mimi (Rej. Mt 25:40). Mapendo na huruma yakikristo si ya vionjo bali ya hitaji. Mungu anatupenda sisi sikwasababu tunavutia, bali tunavutia kwasababu anatupenda nakutuhurumia daima (Rej. Kum 6:5, Law 19:8). Hivi tunapopendana kuhurumia jirani zetu, tunawafanya wavutie na kupendeza natunaufanya uumbaji uvikwe kwa sura yake ya uhalisia wa awali inayovutia.

Mapendo kwa jirani yana msingi wake katika kumpenda Mungu. Ndiyo maana Yesu anasisitiza kuwa, kumpenda Mungu kuende sambamba na kumpenda jirani (Rej. Mt 22:39). Jirani ni mtu yeyote, mhitaji. Mfano wa Msamaria mwema unasisitiza fundisho hilo (Rej. Lk 10:25-37). Na sheria yote na manabii inategemea amri hiyo ya Mapendo (Rej. Mt 22:40). Kumpenda Mungu ina maana pia kupenda vyote vinavyopendwa na Mungu. “Kwahiyo, huruma kwa masikini na wagonjwa, vilevile matendo ya huruma ya ujima, yenye lengo la kupunguza kila aina ya dhiki za wanadamu, yanaheshimiwa na Kanisa kwa namna ya pekee… Utendaji wa huruma leo waweza kuwaelekea watu wote kabisa na mahitaji yao, na lazima uwe wa namna hiyo. Kila mahali wapo watu wenye kukosa chakula, na kinywaji, mavazi, makao, madawa, kazi na elimu, na vifaa vinavyohitajika ili kuweza kuishi maisha yaliyo kweli ya kiutu. Wapo wanaohangaika katika dhiki au kwa sababu ya kukosa afya, wanaoteseka mbali na makwao au walio kifungoni, na hapo mapendo ya Kikristo lazima yawatafute na kuwapata, kuwaliwaza kwa uangalizi mkarimu na kuwainua kwa kuwapatia msaada.”15

Tunapenda basi kuwakumbusha tena mafundisho ya Kanisa letu juu ya matendo ya huruma ya mwili na ya roho. Mapokeo ya Kanisa letu yanatufundisha juu ya matendo saba ya mwili, ambayo Kanisa limechota toka maandiko Matakatifu (Rej. Mt 25:36; Tobit 1:17).

(i) Kuwalisha wenye njaa

(ii) Kuwanywesha wenye kiu

(iii) Kuwavika wasio na nguo

(iv) Kuwakaribisha wasio na makazi

(v) Kuwatembelea wagonjwa

(vi) Kuwatembelea wafungwa

(vii) Kuwazika wafu.

Tukifanya hivyo, huruma ya Mungu itakuwa wazi kwetu na kwao. “Katika parokia zetu, jumuiya zetu, vyama vyetu vya Kitume na vikundi, katika maana kwamba popote alipo Mkristo; kila mmoja apate chemchemi ya huruma.”16 Kusoma, kutafakari na kusikiliza Neno la Mungu ni msaada mkubwa katika kutembea kwenye njia ya huruma. Pamoja na matendo hayo ya huruma ya mwili mapokeo ya Kanisa yanatufundisha pia kutenda matendo ya huruma ya roho yanayotupeleka kuwajibika katika:

(i) Kuwashauri wenye mashaka

(ii) Kuwafundisha wasiojua

(iii) Kuwafariji wenye huzuni

(iv) Kuonya wakosefu

(v) Kusamehe makosa

(vi) Kuvumilia wasumbufu

(vii) Kuombea wazima na wafu

Jamii yetu inajumuisha watu wenye uwezo mkubwa na wenye uwezo mdogo. Wengine ni wazee, watoto, wagonjwa na walemavu, n.k. Tunawahimiza walio na uwezo kuwasaidia wasio na uwezo. Haya ni makundi ya watu wanaotuzunguka kila siku na huu ni uhalisia wa maisha. Tujifunze kumwona Yesu katika wahitaji hawa na tutambue kuwa kila tunapowahudumia tunakuwa tunaliboresha hekalu la Roho Mtakatifu. Tukitumie kipindi cha Kwaresima mwaka huu kama fursa ya kujikumbusha mapokeo haya ya Kanisa na kiwe kipindi cha kuadhimisha na kung’amua huruma ya Mungu. Tukiyatenda matendo haya ya huruma tutakuwa tunadhihirisha huruma na upendo wa Mungu unaoendelezwa katika maisha yetu ya kila siku kupitia ukarimu wa kikristo. Huruma na upendo huenda pamoja.

Toba ya kweli

Mungu wetu ni mwingi wa huruma na mtakatifu. Ingawa anachukia dhambi, hamchukii mkosefu. Anatupokea kila tunaporudi kwake na kutubu. Tunawahimiza kuikimbilia Sakramenti ya Kitubio ili kila mkosefu anayetubu ajipatanishe na Mungu na Kanisa. Sakramenti ya Kitubio inatuwezesha kuugusa utukufu wa huruma ya Mungu. Toba ya kweli inatudai kujirekebisha na kubadilika, kuacha dhambi na kuepuka nafasi ya dhambi. Ili kupokelewa katika ufalme wa Mungu, mwanadamu ni lazima ageuke na kuachana na njia zake mbaya na kushikamana na tangazo la Yesu la ufalme wa Mungu. Hivyo toba ni dai la kwanza la Yesu kwa wale wanaotaka kushiriki katika utawala wa Mungu (Rej. Mt 21:28 – 32). Toba ni nafasi ya kubadili hali na misimamo yetu mibovu; kama vile dhuluma, uonevu kwa wanyonge, mauaji na rushwa inayopoteza matumaini ya wanyonge. Tusikilize sauti za wanyonge na maisha yao, kwa haki na upendo.

Tujue kuwa dhambi zetu hata zile nyepesi zinatuletea shida. Dhambi nyepesi zinadhoofi sha mapendo na kuzuia maendeleo ya kiroho katika zoezi la fadhila na maisha mema.Tuziungame nazo hizo pia! Tendo la upendo wenye huruma linakuwa na huruma kweli kweli, pale tunapojiridhisha na kujiaminisha kwamba wakati tunalitenda, vilevile, tunapokea huruma kutoka kwa watu wale tunaowatendea. Kama sifa hii ya kutoa na kupokea haipo,matendo yetu yatakuwa hayajastahili kuitwa matendo ya huruma; wala ule wongofu ambao Kristo alituonyesha kwa maneno na maisha yake, hata kufa msalabani, utakuwa haujakamilika; wala tutakuwa hatujashiriki katika chanzo cha ajabu cha upendo wenye huruma ambao yeye alitufunulia.”17

SURA YA NNE

BIKIRA MARIA MAMA MWENYEHURUMA

Mapokeo ya Kanisa letu yanatupatia sala ya “Salamu Malkia” inatutafakarisha huruma ya Mungu kwa kumuangalia Mama yetu Bikira Maria, aliye tulizo katika mahangaiko yetu. Yeye aliepushwa na kila doa la dhambi; alikuwa wa kwanza kati ya wote na kwa namna ya pekee alifaidi ushindi ulioletwa na Kristo juu ya dhambi: alikingiwa kila doa la dhambi ya asili, na katika maisha yake yote ya hapa duniani, kwa neema ya pekee ya Mungu, hakutenda dhambi yoyote.19 Mama huyu alitumia vizuri uhuru wake akakubali kuwa Mama wa Mwana pekee wa Mungu, Yesu Kristo Bwana wetu. Kwa maisha yake amemwimbia Mungu sifa daima. Anatukumbusha pia kuwa huruma ya Mungu kwetu sisi wanadamu “hudumu kizazi hata kizazi” (Lk 1:50).

Mama Maria ameshiriki mpango wa ukombozi kwa kutustahilia uzima mpya wa Roho zetu. Maana “Bwana mwenyewe amekuja kumkomboa binadamu na kumtia nguvu akimwumba upya ndani yake na kumfukuza mkuu wa ulimwengu huu, aliyekuwa amemfunga katika utumwa wa dhambi.”20 Tunawahimizeni nyote kwa maombezi ya mama Bikira Maria kujibidisha kutenda mema ili kujijengea fadhila na kujipatia majina yenye sifa njema katika maisha. Tumuombe mama Bikira

Maria mwenye huruma awe msaada na mwombezi wetu katika juhudi zetu. Tujue kuwa Mama Bikira Maria ni mfano wetu wa namna ya kuwa mfuasi mwaminifu wa Kristo. 22. Tuombe msaada wa maombezi ya Mama Bikira Maria ili tuweze kuwa wafuasi waaminifu wa kuonesha huruma ya Mungu kwa watu wote. Mtakatifu Bernardo anatuasa kumkimbilia Mama huyu akisema; “Ikiwa tunahofu kuikimbilia huruma ya Baba, tumgeukie Yesu Kristo aliyetwaa mwili wetu na Kaka yetu Mwenye Huruma. Na ikiwa kwa Yesu tunahofi a ukuu wa enzi ya Umungu wake, tunaweza kumkimbilia Maria Mama yetu na mtetezi wetu mwenye huruma, awasikilizae wanae kama Baba amsikilizavyo Mwana.”21

HITIMISHO

Wapendwa Taifa la Mungu, kipindi cha Kwaresima ni cha kuitayarisha mioyo yetu kwa toba, kufunga, kusali, kutoa sadaka, na kutenda matendo mema ili kujiandaa kukumbuka Fumbo la Pasaka: yaani, mateso, kifo, na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo.Tukumbuke pia kwa kushiriki msalaba wake, na kwa neema yake tutashirikishwa pia utukufu wa ufufuko wake. Ni kipindi cha kutafakari zaidi zawadi ya fumbo la ukombozi wetu na namna tunavyoshiriki upendo wa Kristo katika suala zima la ukombozi, kwa mjibu wa ubatizo wetu. Tuombe neema ili tujivike fadhila ya unyenyekevu tuweze kutenda vema na kiaminifu katika utumishi wetu. Yafaa tumwombe Mungu atujalie fadhila ya unyenyekevu ambayo inatusaidia kujitambua kuwa tu wadhambi na tukishajitambua hivyo yatupasa tufanye toba mara.Tunahitaji msaada wa Kristo aliye Bwana wetu mwenye huruma tukimkimbilia atusaidie. Tukaze nia ya kuishi kama watumishi wenye huruma.

 

Ni sisi Maaskofu wenu,

1. Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Iringa

Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania

2. Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya, Ofm Cap, Dodoma

Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania

3. Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Dar es Salaam

4. Askofu Mkuu Josaphat Lebulu, Arusha

5. Askofu Mkuu Paul Ruzoka, Tabora

6. Askofu Mkuu Yuda Th addaeus Ruwa’ichi, Ofm Cap, Mwanza

7. Askofu Mkuu Damian Dallu, Songea

8. Askofu Telesphor Mkude, Morogoro

9. Askofu Bruno Ngonyani, Lindi

10. Askofu Anthony Banzi, Tanga

11. Askofu Agapiti Ndorobo, Mahenge

12. Askofu Evaristo Chengula, IMC, Mbeya

13. Askofu Severine NiweMugizi, Rulenge-Ngara

14. Askofu Augustino Shao, CSSp, Zanzibar

15. Askofu Damian Kyaruzi, Sumbawanga

16. Askofu Desiderius Rwoma, Bukoba

17. Askofu Method Kilaini, Askofu Msaidizi, Bukoba

18. Askofu Ludovick Minde, ALCP/OSS, Kahama

19. Askofu Alfred Leonard Maluma, Njombe

20. Askofu Castor Paul Msemwa, Tunduru-Masasi

21. Askofu Michael Msonganzila, Musoma

22. Askofu Issack Amani, Moshi (Ap.Adm. Mbulu)

23. Askofu Almachius Rweyongeza, Kayanga

24. Askofu Eusebius Nzigilwa, Askofu Msaidizi, Dar es Salaam

25. Askofu Salutaris Libena, Ifakara

26. Askofu Rogath Kimaryo, CSSp Same

27. Askofu Renatus Nkwande, Bunda (Ap.Adm, Geita)

28. Askofu Gervas Nyaisonga, Mpanda

29. Askofu Bernadin Mfumbusa, Kondoa

30. Askofu John Ndimbo, Mbinga

31. Askofu Titus Mdoe, Mtwara

32. Askofu Joseph Mlola ALCP/OSS, Kigoma

33. Askofu Prosper Lyimo, Askofu Msaidizi, Arusha

34. Askofu Liberatus Sangu, Shinyanga

35. Askofu Edward Mapunda, Singida

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, S.L.P 2133, Dar es Salaam

Simu: +255 22 2851077, Faksi: +255 22 2850295, Email: info@tec.co.tz

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.