2016-01-28 09:11:00

Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu yawatie shime kusimamia haki jamii


Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa ni sehemu ya maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu kwa Kanisa kuangalia kwa namna ya pekee juu ya Fumbo la Ekaristi Takatifu: chanzo na lengo la maisha na utume wa Kanisa. Kongamano hili limefunguliwa rasmi tarehe 25 Januari na litahitimishwa tarehe 31 Januari 2016.  Katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kazi ya ukombozi iliyo tekelezwa na Kristo Yesu inadhihirika sanjari na kuonesha uwepo endelevu wa Kristo kati ya watu wake.

Mababa wa Kanisa wanakumbusha kwamba, Ekaristi Takatifu ni chanzo na lengo la maisha na utume wa Kanisha. Hii ni Sakramenti ya upendo, alama ya umoja na mshikamano wa dhati na dhamana ya ukarimu kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Maadhimisho haya yanafanyika Barani Asia kama nafasi ya kutafakari kuhusu maisha na utume wa Kanisa Barani Asia unaopaswa kujikita katika majadiliano ya kidini, kitamaduni na maskini.

Kanisa linapenda kukuza na kudumisha utume miongoni mwa vijana wa kizazi kipya, kwani Kanisa linatambua kwamba, vijana ni udongo wenye rutuba nzuri katika maisha na utume wa Kanisa. Ili vijana waweze kutekeleza vyema dhamana na utume wao, wanapaswa kupewa malezi bora na endelevu. Mababa wa Kanisa wanatambua nafasi na mchango wa Bikira Maria katika maisha na utume wa Kanisa. Bikira Maria ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili. Kumbe, Bikira Maria ni mfano na Mama wa Kanisa. Huu ni mwaliko wa kujifunza kutoka katika shule ya Bikira Maria ili Kanisa liweze kujikita zaidi katika mchakato  wa Uinjilishaji mpya unaojikita katika ushuhuda, ari na mwamko wa kimissionari.

Waamini wanakumbushwa kwamba, Kristo ndani wao, tumaini la utukufu. Hii ni mbegu ya Umissionari inayoshuhudia utukufu wa Mungu unaofumbatwa katika Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Huu ndio ushuhuda endelevu wa utukufu wa Mungu ambao unajionesha kwa mtu mzima na kwamba, maisha ya binadamu ni taswira ya Mungu. Upendo na huruma ya Mungu inawakumbatia na kuwaambata binadamu wote.

Kardinali Charles Maung Bo, Mwakilishi wa Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa katika mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya ufunguzi wa maadhimisho haya anasema, dunia iko kwenye mapambano makubwa dhidi ya umaskini, magonjwa na baa la njaa duniani. Ni mapambano yanayolenga kuwapatia watoto heshima na hadhi yao kwa kuwapatia chakula na malezi bora badala ya Makampuni ya Kimataifa kujikita katika uzalishaji na usambazaji wa silaha zinazopandikiza utamaduni wa kifo dhidi ya Injili ya uhai.

Kardinali Maung Bo anawataka waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete, kulinda, kutetea na kushuhudia haki jamii ikitekelezwa kwa dhati sanjari na kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kwa njia ya matendo ya huruma yanayotiliwa mkazo na Baba Mtakatifu Francisko wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu.

Kardinali Charles Maung Bo anakaza kusema, takwimu za UNICEF zinaonesha kwamba, kuna idadi kubwa ya watoto wanaopoteza maisha yao kila siku kutokana na utapiamlo wa kutisha, hali ambayo inaweza kuonekana kuwa kama ni mauaji ya kimbari. Ulimwengu wa leo unakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa usawa katika mapambano dhidi ya baa la umaskini duniani. Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu ni changamoto kwa waamini kuambata haki jamii, kwani kuna uhusiano mkubwa kati ya Ekaristi Takatifu na umaskini.

Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu yanampatia mwamini hadhi na utu unaomwezesha kushiriki Mkate wa uzima wa milele, Kristo Yesu aliyeshuka kutoka mbinguni ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Hapa waamini wanapaswa kuwa ni Ekaristi kwa jirani zao kwa kutangaza na kushuhudia Injili ya uhai dhidi ya utamaduni wa kifo unaojikita katika sera za utoaji mimba na kifo laini au eutanasia.

Waamini wanayo Ibada kubwa kwa Ekaristi Takatifu, lakini haitoshi anakaza kusema Kardinali Charles Maung Bo, kwani Kristo anawataka wafuasi wake kumfuasa kwa kubeba Misalaba yao; tayari kujisadaka katika mapambano dhidi ya umaskini; unyonyaji, udhalimu, ukandamizaji na badala yake kujenga mshikamano wa upendo na huruma kwa kujitahidi kumwilisha matendo ya huruma: kiroho na kimwili kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko wakati huu  wa Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu.

Ibada ya Misa takatifu kwa ajili ya ufunguzi wa Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa limehudhuriwa na viongozi wengi wa Kanisa pamoja na familia ya Mungu kutoka ndani na nje ya Ufilippini. Maadhimisho haya yanayongozwa na kauli mbiu “Kristo ndani yenu, tumaini letu la utukufu”.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.