2015-12-25 10:20:00

Familia za Kikristo ziwe ni chemchemi ya fadhila za Kimungu!


Mpendwa mwana wa Mungu, leo tunasherehekea na kushangilia sherehe ya familia Takatifu. Masiha amezaliwa ndani ya familia hii. Ndani ya familia hii kuna majukumu ya kutekeleza ili Mwana wa Mungu akae mahali stahili na kwa namna hiyo atufundisha namna ya kutenda na kuishi kwenye familia zetu. Mwaka huu kwa namna ya pekee kabisa, Kanisa linaadhimisha Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu baada ya maadhimisho ya Sinodi ya Familia na kwa sasa maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu, changamoto kwa familia kuwa kweli ni chemchemi ya huruma ya Mungu kwa ndugu na majirani!

Somo la kwanza toka kitabu cha Hekima ya Yoshua bin Sira linaweka mbele yetu fahari na heri ya kuwaheshimu wazazi na kuwatunza katika uzee wao. Heri ambazo ziko wazi kadiri ya somo hili ni kuwa na uzao, na si uzao tu bali kufurahia uzao huo. Kuwa na maisha marefu na uzee wa kusifika. Kwa kuwatunza wazazi na kuwapa heshima stahili mmoja afanya malipizi ya dhambi zake. Kwa hakika somo hili lasisitiza na kuweka mkazo juu ya amri ya nne ya Mungu: Waheshimu baba na mama upate miaka mingi na heri duniani.

Mtakatifu Paulo anapowaandikia Wakolosai anafafanua namna ya kuishi na kupendana katika familia.  Ameweka wazi fadhila ambazo zajenga maisha ya familia yaani, unyenyekevu, utu wema, rehema na msamaha kwa kila mwanafamilia.  Kilainisho cha fadhila hizi ni UPENDO kifungo cha ukamilifu. Kama familia na hasa kila mwanafamilia ataweza kuitikia mwaliko huu wa Mungu, basi familia nzima itakaa katika utulivu, usalama na amani ya kweli yaani inayokuza mshikamano.

Mtume Paulo haishii tu kwenye upendo bila kuweka jambo la kutuweka pamoja yaani kusikia na kusikiliza sauti ya Mungu kwa njia ya Neno lake. Kwa kutafakari Neno la Mungu tunajiweka tayari siku zote kukaa na Bwana aliye Neno wa Milele, aliye nuru angavu tuliyoipokea wakati wa siku ya Noeli. Pamoja na fadhila nyingine fadhila ya utii yatufaa kwanza kwa kutii Neno la Mungu na pili kutii mamlaka iliyowekwa na Kristu katika familia. Baba ni mkuu wa familia yafaa kumtiii na kumheshimu lakini yeye mwenyewe lazima aige mfano wa Kristu Mchungaji mwema anayewahangaikia kondoo wake. Ndiyo kusema aoneshe daima fadhila ya upendo kwa mke wake, watoto wake na watu wote .

Katika Injili ya Luka tunapata mfano wa familia iliyo na utii kwa sheria za kidini. Ni lazima wakampeleke mzaliwa wa kwanza hekaluni. Yesu Mwana wa Mungu atufundisha kujitoa kabisa kwa Mungu anayetuagiza daima kutimiza mapenzi yake kwa njia ya Kanisa. Kwa kumpeleka Yesu Kristu huko hekaluni wanaonesha pia wajibu wa kumwelisha mtoto katika elimu ya dini na wajibu kijamii. Ndiyo kusema wewe mzazi unapaswa na unawajibika kutoa mafundisho msingi ya kikristu na unawajibika kutafuta shule itakayomkuza mwanao vema katika utu, ukristu na malezi kijamii.

Jambo jingine tunaloliona katika Injili ni lile la Simeon kumchukua mtoto Yesu toka mikono ya wazazi wake na baadaye kumtoa kwa watu wote. Kwa jambo hili Simeon anawakilisha taifa la Israeli lililokuwa likisubiri ujio wa Masiha na sasa amefika na kumtoa kwa wote maana yake Masiha si wa Israeli tu bali ni kwa ajili ya mataifa. Simeon katika maisha yake alikuwa akisubiri bila manunguniko, ni alama ya wazee wa sasa ambao wanajikabidhi mikononi mwa Mungu wakisali na kuimba daima na kungojea fadhili za Bwana huku wakitimiza wajibu wao wa kujenga hekima katikati ya familia na watu.

Katika Injili pia kuna binti mwanamke aitwaye Anna, huyu ni mfano wa unyenyekevu na uwajibikaji katika kutimiza kazi ya Bwana. Ni mfano wa wale ambao wametayarisha njia ya Bwana na mapito yake. Anatoka katika ukoo mdogo wa Asheri ambao mbele ya Waisraeli ni bure na maskini, lakini toka hapo Anna anampokea Bwana kwa furaha. Hii ni habari ya furaha, kwako wewe mwamini katika udogo wako na utauwa wako kuna matunda makubwa ya neema za Mungu. Hawa tuliowasikia katika Injili wakitenda kazi ya Bwana wanakuwa kichocheo cha wanafamilia kutenda vema katika familia zao daima wakilenga utukufu wa Kristu uliokwishafunuliwa kwetu na Bwana mwenyewe.

Ninakutakieni heri tele wewe uliyemdau wa familia na hasa unapoweka nguvu yako kukuza tunu bora za familia, ukiangazwa na Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Heri tena kwa jumuiya zote, parokia zote, mashirika ya kitawa mliojiweka chini ya usimamizi na ulinzi wa familia takatifu. Tumsifu Yesu Kristo Maria na Yosefu. Tafakari hii imeletwa kwako toka Pd Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.