Mashirika ya Kimataifa yanayoshughulika na masuala ya watu na pia yale ya utabiri wa hali ya hewa, katika taarifa zake za hivi karibuni, yameonya kwamba, wakati huu wa kufurahia siku kuu ya Kristmas na ujio wa Mwaka mpya 2016, ni lazima pia watu wawe makini katika matumizi ya vile walivyo navyo hasa chakula kilichopo. Onyo hilo limetolewa kutokana na hali halisi zinazoonyesha kwamba, mwaka 2016 unaweza kuwa mwaka mgumu katika upatikanaji wa mahitaji ya lazima hasa chakula na maji kutokana na mwelekeo wa uwepo wa hali ya hewa ya ukame katika baadhi ya maeneo na maeneo mengine kukabiliwa na mafuriko, hali ya la Nino na el Nino.
Richard Choularton, Mkuu wa Utabiri wa hali ya hewa kwa ajili ya uzalishaji wa chakula wa Mpango wa Chakula wa Dunia(WFP), hivi karibuni ameonya kwamba, kwa mwaka huu kuna zawadi ya Kristmas isiyotakiwa ya El Niño , inayoletwa na ongezeko la joto katika ukanda wa Tropikali katika bahari ya Pacific, inayosababisha katika baadhi ya maeneo, ukame na upande mwingine mafuriko ambavyo kilele chake kinaweza kuwa mwishoni mwa mwezi huu, lakini athari zake zitaendelea kuonekana katika mfumo wa hali ya hewa duniani kote katika misimu ya 2016.
Nalo Shirika la Uratibu wa Misaada la Umoja wa Mataifa OCHA, limeonya kwamba, Mwaka huu El Niño imeonekana kupata nguvu kwa kasi zaidi tangu Machi, na kusababisha mamlioni ya watu, kuhitaji nyongeza ya msaada hasa wa chakula. Ripoti ya OCHA, imerejea hali halisi mbili zilizo onekana barani Afrika, eneo la Kusini mwa Afrika na baadhi ya sehemu katika nchi za Pembe ya Afrika , Eritrea Djibout , Somalia na Ethiopia, zikikabiliwa na ukame , wakati pia sehemu zingine katika mataifa hayohayo, nchi za Afrika Mashariki, kuwa na mvua nyingi zenye kusababisha mafuriko na uharibifu mkubwa wa mazao, wakati maeneo mengine ya Afrika, hali zake zikiwa hazieleweki eleweki. Hali hii inatia simanzi hasa kwa Afrika ambako asimilia 80 ya wakazi wake, hutegemea kilimo. Wengi hawana namna ya kuweza kukabiliana na hali hizi iwe mafuriko au ukame wa kukithiri.
Hivyo hali hii inakuwa ni mtihani mkubwa kwa wana wa Afrika, ambo wengi wao wanaishi tayari katika mazingira magumu na sasa yanazidi kuwa magumu na hali hii ya el nino.
OCHA linaendelea kuonya kwamba, zaidi ya watu milioni 30 tayari wanakabiliwa na uhaba wa chakula. Hii pia ikiwa na maana ya afya zao kuwekwa hatarini kama matokeo ya mavuno haba na umaskini zaidi. Kwa mfano uzalishaji wa mahindi nchini Afrika Kusini, ambacho ni chakula kikuu cha kijadi kimepungua kwa kiwango kikubwa kutokana na ukame uliotokea katika mikoa mitano, ukisababisha pia pato lake limeshuka kwa asilimia 30. Kwa hali hiyo, ni wazi hata hifadhi ya mahindi kwa dharura imepungua, na bei yake kupanda. Ukame unaosababisha Afrika Kusini , kuandaa mpango wa kuagiza tani 750,000 za mahindi ili kukidhi mahitaji yake.
Nchi zitakazoathirika zaidi na Ukame huu kwa mwaka 2016, zimetajwa kuwa ni pamoja na Angola, Afrika Kusini, Botswana, Zambia, Zimbabwe, Lesotho, Swaziland, na Msumbiji. Choularton wa WFP, ametoa wito kwa serikali na kila mtu katika mataifa hayo, kujiandaa kukabiliana na hali hiyo mbaya ya chakula inayotabiriwa kwa mwaka 2016.
Na kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Save the Children, uhaba wa mvua pia umekumba sehemu kubwa za mataifa ya Eritrea, Djibout, Sudan , Somalia na Ethiopia. Ukame unaotajwa kuwa mbaya kama ule uliotokea miaka 50 iliyopita . Na kwamba kwa mwaka 2016 watu zaidi ya milioni 15 watapambana na uhaba wa chakula hadi kufikia kipindi cha mavuno mwezi June 2016.
Na wakati huohuo utabiri unaonyesha uwepo wa mavua kubwa na mafuriko katika eneo la Bonde la Kusini na Mashariki mwa Ethiopia. Mvua zitakazo sababisha mafuriko makubwa katika bonde la Mto Shebelle , na kuathiriwa wakazi wa bonde hilo wasiopungua laki tatu, kama pia itakavyokuwa katika eneo la Kusini mwao Somalia na Putland ambako watu karibia milioni moja wataathirika, katika taifa hilo ambako mpaka sasa hata bila uwepo wa el Nino , watu zaidi ya milioni tatu wanahitaji chakula cha msaada kuokoa maisha yao.
Mamlaka ya utabiri wa hali ya hewa Kenya, pia inasema hali ya el Nino na la Nina, inayo shamirishwa na ongezeko la joto katika bahari ya Hindi, ukanda wa pwani ya Afrika Masharik, itasababisha msimu wa mvua za masika kuwahi. Kwa mwelekeo huo , serikali ya Kenya imetahadharishwa kuchukua hatua za kidharura, kuhamisha watu, karibia milioni moja wanaoishi katika maeneo yenye hatari ya kukumbwa na mafuriko. Aidha kunahimiza maandalizi ya mpango wa kusaidia utoaji wa mbegu kwa wakulima wadogowadogo , kutokana na hitaji la kupanda mbegu mara kwa mara na kutoa ruzuku kwa pembejeo ya mbolea. Pia kuwa na juhudi za ziada za kutoaji dhdi ya mfumko wa homa ya Bonde la Ufya kwa chanjo kwa watu wengi zaidi.
Vivyo hivyo,nchini Uganda , serikali kutoa wito kwa watu 800,000 wanaoishi katika maeneo yenye hatari za kuwa na maporomoko ya ardhi, maeneo ya miinuko na milima, wahamie katika maeneo salama zaidi. Na kwamba serikali itatoa mkopo wa kusaidia ufanikishaji wa uhamaji huo. Na kwamba tayari kikosi cha Kitaifa cha kujihami na maafa, kimepelekwa katika Mlima Elgon na Mlima Ruwenzori , pamoja na maeneo yenye hatari za kuwa na mafuriko , Mashariki, Kusini Magharibi na Magharibi mwa Uganda.
Wachambuzi wa masuala ya Kijamii, wakitazama kwa kina mabadiliko haya ya tabia nchi wanatumaini kwamba, dunia na hasa viongozi wa kisiasa watatimiza ahadi zao walizotoa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, ahadi walizotoa katika Mkutano wa Paris, mwezi huu, kwa lengo la kupunguza Ongezeko la joto duniani, ambalo linatajwa moja ya sababu za kuwepo wake ni utendaji mbovu wa binadamu.
Katika Mkutano huo wa Dunia wa Paris, imekubalika kushikilia haja ya kupunguza ongezeko la joto kimataifa katika wastani wa chini ya nyuzijoto 2C , na hasa kutafuta jitihada za kupunguza ongezeko hilo hadi nyuzijoto 1.5 C. Ili kufanikisha hili lengo hili, wachambuzi wanasema,ni lazima serikali na makampuni yaitikie maanani azimio lililofikiwa, kupunguza uzalishaji wa gesi chafu mapema iwezekanavyo, na kutambua kwamba itachukua muda mrefu kuleta mabadiliko yanayotarajiwa katika lengo hilo.
Na kwamba juhudi hizo ni lazima zifanywe chini ya mfumo wa ushirikiano wa nchi zote, maana hakuna taifa linaloweza kufanisha lengo hilo kwa kutenda kivyakevyake. Ni muhimu kila taifa kuwa na maamuzi thabiti ya kutoa mchango wake ili kupunguza uzalishaji wa hewa chafu kimataifa kama ilivyokuwabalika katika kiwango cha kila kipindi ila miaka mitano,ingawa ukaguzi wa kwanza kimataifa utafanyika mwaka 2023 na baada ya hapo kila miaka mitano.
Nchi zote, zile zilizo endelea zenye kuwa na viwanda vingi ,ni lazima kuwa na mikakati inayoongoza katika malengo ya kupunguza kile kinachoitwa uchumi mchafu, wakati nchi zinazoendelea zenyekuwa na viwanda vichache, vikitakiwa kuendelea kuimarisha juhudi zakekatika kukabiliana na mabadiliko yanayosababishwa na hewa chafu licha ya uwepo wa juhudi za kukuza viwango vyake vya uchumi wa nchi.
Aidha Wachambuzi pia wanakubali kwamba ni lazima kuwepo mabadiliko makubwa katika mfumo wa fedha wa dunia ili kuzuia uwekezaji wa kiholela usiojali ulinzi wa mazingira.
Baba Mtakatifu Francisko, kupiti hotuba na nyaraka zake nyingi, amekuwa akionya dhidi ya uharibifu wa asili unaofanywa na binadamu, na kuwataka wote kulinda asili , si kama kitendo binafsi, lakini kama haitaji la lazima katika mshikamano na ujenzi wa amani na wengine . Mshikamano wenye kuongozwa na hisia za kuheshimiana na kuwa na huruma kwa wengine. Kupendelea zaidi kuhudumia wengine kuliko kutafuta faida binafsi. Na ndivyo ilivyo katika kipindi hiki cha Kristmas na mwaka mwaka, Papa katika ujumbe wake kwa ajili ya Siku ya Kuombea amani Dunia, hapo tafrehe Moja Januari,pia amekumbusha umuhimu wa kujali kutunza mazingira kwa manufaa ya wote, kama pia alivyoeleza kwa kirefu katika waraka wake juu ya utunzaji wa Asili, waraka alioutoa chini ya jina “Laudato Si”. Papa ameasa tusiihi kwa kukumbatia rushwa na ufisadi, na kufinyanga haki za asili, bali kutetea na kudumisha maumbile asili kwa mahufaa ya wote.
All the contents on this site are copyrighted ©. |