2015-12-05 15:23:00

Sherehe ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili!


Mpendwa mwanatafakari, tukiwa bado katika safari ya hija ya wokovu, maandalizi ya roho zetu kumpokea Mtoto Emanueli, Mwana wa Mungu, Mama Kanisa haachi kutuwekea zawadi kichocheo cha imani, furaha na matumaini ya mioyo yetu. Zawadi hii ni fumbo la kukingiwa dhambi ya asili Bikira Maria, Mama wa Mungu.Siku kuu kwa mwaka huu ina umuhimu wa pekee kabisa kwani ni mwanzo wa uzinduzi wa Mwaka Mtakatifu wa Jubilei kuu ya huruma ya Mungu,

Mpendwa, tunatambua kabisa kwamba, kwa njia ya Adamu tumeingia duniani, na katika hali ya kawaida twajua kuwa roho ikiungana na mwili lazima ipate madhara ya mwili na hivi kwa jambo hili dhambi ya asili. Je, inawezekanaje Mama huyu asipate dhambi hii? Swali hili limekuwa likiulizwa tangu karne za kwanza za Kanisa mpaka hivi leo. Mama Kanisa akisali sana na kujikabidhi mbele ya Mungu akitazama Neno la Mungu na mapokeo (tradition) anaweka wazi ufunuo wa Mungu mwenyewe akifundisha ulio ukweli wa ufunuo na kutangaza kuwa Bikira Maria ni Mkingiwa dhambi ya asili.

Mama huyu anakingiwa dhambi ya asili kwa sababu lazima awe makao stahili ya Mwana wa Mungu aliye mtakatifu, asiye na doa la dhambi. Ndiyo kusema kwa vile Mwana wa Mungu ni mtakatifu asingeweza kuingia mahali pasipo patakatifu. Kumbe kukingiwa dhambi ya asili kwa Mama Bikira Maria ni zawadi ya Kristo mwenyewe kwa Mama yake, na anaitoa zawadi hii mapema kwa mastahili ya msalaba atakaoupokea baadaye. Tunafundishwa hilo na Yohane Duns Scotus katika kipindi cha zama za kati cha Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume.

Mpendwa mwana wa Mungu, wazazi wetu wa kwanza walidanganywa na nyoka, wakaanguka katika dhambi ya kwanza, wakapoteza utakatifu. Kukingiwa dhambi ya asili kwa Bikira Maria ni alama ya nguvu ya Mungu juu ya dhambi iliyowaangusha wazazi hawa. Kumbe kwa fundisho hili la imani tunaamini na kupata tumaini jipya kuwa kwa kuungana na Kristu, dhambi na mwovu vitapatilizwa na mwanadamu kuwa huru. Mama Kanisa anasherehekea sherehe hii kila tarehe 8 mwezi wa kumi na mbili kila mwaka. Sherehe haitukuzi tu usafi, uzuri na utakatifu wa Mama yetu Maria bali ni fundisho la imani ambalo twapaswa kuliamini kina. Fundisho hili lilitangazwa na Baba Mtakatifu Pio IX mnamo tarehe 8 Desemba mwaka 1854 kuwa FUNDISHO LA IMANI.

Mama Kanisa anaposherehekea sherehe hii anataka kila mmoja wetu akumbuke mwanzo wa ukombozi wetu. Mama huyu alikingiwa dhambi ili aruhusu Mwana wa Mungu kutungwa mimba katika mji usio na doa na hivi nasi katika utakatifu huo tunaweza kukombolewa. Kwa hakika hatuwezi kukombolewa na awaye yote aliyeguswa na doa la dhambi bali tunakombolewa na asiyeguswa na doa la dhambi naye ni Kristu Masiha, Mwana wa Mungu. Mama Bikira Maria alizaliwa kama ambavyo Mungu alikuwa amekusudia mwanadamu awe tangu mwanzo. Fikiria juu ya Adamu na Eva kabla ya kutenda dhambi yao ya kwanza, walikuwa watakatifu lakini kwa tamaa tamaa ya ulimwengu na kiburi kinzani wakaharibu utakatifu wao. Kinyume nao Mama Maria anatunza utakatifu aliokabidhiwa katika neema ya Mungu. Anakuwa tunda la kwanza la ukombozi. Anakuwa tabernakulo ya kwanza kumbeba Masiha.

Mpendwa, kwa sherehe hii si tu tunakumbuka mwanzo wa ukombozi wetu bali pia mwisho wa maisha yetu. Ndiyo kusema tunamwomba Mama atuombee tuweze nasi kuonja matunda ya kazi ya mwanae, tuweze kuishi bila dhambi tukilenga daima maisha ya utakatifu. Mama huyu ni mfano wa maisha bora, ni taa ambayo inaendelea kuwaka anapojitokeza tena na tena katika maeneo mbalimbali akileta ujumbe wa mwanae kwa mataifa. Ombi kwako mwana wa Mungu, ebu jaribu kufanya safari ya hija katika maeneo mbalimbali ambayo Mama Kanisa ameyaratibisha ukaonje mapendo ya Mama huyu. Baadhi ya maeneo hayo ni Lurdi-Ufaransa, Fatima-Ureno, Pompei, Loreto-Italia, Nyakijoga Bukoba Tanzania na mengineyo mengi.

Mpendwa tukiendelea kusali kwa kujitayarisha kwa ajili ya majilio, tunawaombea wale wote waitwao Imakulatha wakashike vema utauwa wao, wakamwite Mama Maria Bikira akawaimarishe katika utumishi wao kwa umma na kwa Kanisa. Tunawaombea Masista wote wanaotimiza miaka 25, 50 ya utawa, wanaoweka nadhiri za muda na za milele wakaimarishwe na Mama Bikira Maria Msaada wa Daima, Mama wa Huruma na matumaini. Tunaziombea Parokia zote na mashirika yote ya kitawa waliojiweka chini ya ulinzi wa Mama Bikira Mkingiwa wa dhambi ya asili wakaimarike na kuwa safina ya umoja, upendo na ustawi wa kiroho na hasa katika maisha ya sakramenti.

Tumsifu Yesu Kristo na Maria. Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.