2015-12-02 09:53:00

Kuna mfungamano wa kidugu kati ya Waislam na Wakristo!


Kitendo cha Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kitume kutembelea Msikiti mkubwa wa Bangui, ili kusali na kuwasalimia waamini wa dini ya Kiislam limepokelewa kama kielelezo cha heshima kubwa na waamini wa dini hizi mbili na kwamba, wanachangamotishwa kusimama kidete kulinda na kudumisha mahusiano mema kati yao dhidi ya wajanja wachache wanaotaka kuwagawa na kuwavuruga kwa misingi ya kidini.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na Imam Tidian Mousa Naibi wa Msikiti mkuu wa Bangui wakati alipokuwa anamkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kusalimiana na waamini wa dini ya Kiislam waliokuwa wamefurika msikitini hapo. Anakaza kusema, watu wabaya wanaweza kuchelewesha mchakato wa umoja, amani, upendo na mshikamano kati ya waamini wa dini hizi mbili huko Afrika ya Kati, lakini hawataweza kuvunjilia mbali mfungamano na mshikamano wa kidugu uliomo ndani ya Jumuiya zao.

Waislam na Wakristo wanapaswa kuishi kwa amani huku wakipendana, wakiheshimiana na kusaidiana, kwani wao ni wamoja na kwamba, ili kutekeleza dhamana hii kwa dhati kabisa wanapaswa kuungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa na wala si kuwagawa kwa misingi ya udini! Mshikamano huu umeshuhudiwa kwa namna ya pekee kwa uwepo wa Baba Mtakatifu nchini mwao, lakini zaidi kwa kuwatembelea, kusali na kuzungumza nao kama ndugu.

Ni matumaini ya Imam Tidian Mousa Naibi kwamba, hali tete inayoendelea kujitokeza nchini mwao, iko siku itakoma na wananchi wataweza kurejea tena katika maisha yao ya kawaida, kwani ndani mwao wameshikamana kama ndugu. Hiki ni kipindi kigumu sana cha historia na maisha ya watu wa Afrika ya kati. Jitihada za watu wenye mapenzi mema anasema Imam Naibi, iko siku zitazaa matunda ya haki, amani, usalama na maridhiano kati ya watu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican. 








All the contents on this site are copyrighted ©.