2015-11-28 17:32:00

Mamlaka ya Mapato Tanzania kunawaka moto!


Serikali ya awamu ya tano imewasimamisha kazi watumishi watatu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambao Siku ya Ijumaa tarehe 27 Novemba 2015 iliamriwa kwamba watahamishiwa mikoani. Watumishi hao ni Bw. Anangisye Mtafya, Bw. Nsajigwa Mwandengele na Bw. Robert Nyoni. Uamuzi huo umetolewa Jumamosi, Novemba 28, 2015), na Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa ili kupisha uchunguzi zaidi wa tuhuma zinazowakabili. Kama ilivyo kwa wenzao sita waliosimamishwa kazi Ijumaa (akiwemo aliyekuwa Kamishna Mkuu), nao pia hawaruhusiwi kusafiri kwenda nje ya nchi hadi uchunguzi utakapokamilika.

“Kazi ya kuwachunguza ilianza Ijumaa ileile na sasa, tumeona hawa watu wanapaswa kuwa nje ya utumishi ili kupisha uchunguzi ufanyike kwa uhuru zaidi,” alisema Waziri Mkuu.  Pia Waziri Mkuu amemuagiza Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Dkt. Philip Mpango atekeleze maagizo hayo kwa kuwaandikia barua watumishi hao. Jana mchana, Waziri Mkuu alifanya ziara ya kushtukiza kwenye bandari ya Dar es Salaam akiwa na nia ya kukagua namna shughuli zinavyoendelea kwenye bandari hiyo hasa kwenye maeneo ya kupokelea mizigo kutoka nje ya nchi.

Katika kikao kilichofanyika bandarini hapo na kuhudhuriwa na baadhi ya viongozi wa Serikali, Waziri Mkuu aliamua kuwasimamisha kazi maafisa watano na TRA kutokana na ‘upotevu’ wa makontena 349 yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 80/-. Waziri Mkuu alisema upotevu huo unasababishwa na mchezo unaofanyika baina ya wafanyabiashara na watumishi wa TRA ambao wanaruhusu makontena kupita bila kulipiwa ushuru na hivyo kuikosesha Serikali mapato halali.

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU.








All the contents on this site are copyrighted ©.