2015-11-19 14:56:00

Achana na Dr. Magufuli! Kassim Majaliwa, Waziri mkuu!


Baada ya kuteuliwa na Rais John Pombe Magufuli, Mheshimiwa Kassim Majaliwa amethibitishwa na wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Waziri Mkuu kwa kupata kura za ndio 258 sawa na asilimia 73.5% ya kura zote 351 zilizopigwa. Kura za hapana ni kura 91 sawa na asimilia 25 ya kura zote, na kura zilizoharibika ni 2. Mheshimiwa Majaliwa amemshukuru Rais Magufuli kwa kumwamini na ameahidi kuwatumikia watanzania wote bila kujali itikadi zao za vyama. Kabla ya uteuzi huu na hatimaye kuthibitishwa na Bunge, Mheshimiwa Majaliwa katika awamu ya Serikali ya nne alikuwa ni Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri mkuu, TAMISEMI, elimu. Wengi wanamtaja kuwa ni kiongozi hodari, mwadilifu, mchapakazi na mtu asiyependa makuu!

Wakati huo huo, Mwanasheria Mkuu Apinga Hoja za UKAWA...Asema Dr. Shein ni Rais Halali wa Zanzibar na atahudhuria Uzinduzi wa Bunge la 11

Mwanasheria mkuu wa serikali, George Masaju amepinga hoja zilizoibuliwa na UKAWA kuhusu uhalali wa rais wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar, Dkt Shein, kuhudhuria kwenye uzinduzi wa Bunge. Masaju ametumia ibara ya 102 ya katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania kupangua hoja hizo ambayo inaeleza kuwa, kutakuwa na serikali ya Zanzibar itakayo julikana kama serikali ya mapinduzi ya Zanzibar ambayo itakuwa na mamlaka katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo mambo ya muungano kwa mujibu wa masharti ya katiba hii.

Pia ametumia ibara ya 103 ibara ndogo ya kwanza ya katiba ya jamhuri inayosema kuwa, kutakuwa na kiongozi wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar ambae ndiye atakuwa rais wa Zanzibar na mkuu wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na vilevile mwenyekiti wa baraza la mapinduzi. Baada ya Ibara hizo, akajielekeza kwenye katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 katika Ibara yake ya 26 ambayo inasema, kutakuwa na rais wa Zanzibar ambae atakuwa mkuu wa nchi ya Zanzibar, kiongozi wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar.

Hali kadhalika akanukuu Ibara ya 27 ambayo inaeleza namna rais wa Zanzibar atakavyo patikana ambayo inasema kwamba, rais atachaguliwa kufuatana na katiba hii na kwa mujibu wa sheria yoyote itakayotungwa na baraza la wawakilishi kuhusu uchaguzi wa rais na mwenyekiti wa baraza la mapinduzi na uchaguzi wa rais utafanyika katika tarehe itakayowekwa na tume ya uchaguzi (ikiwa na maana ya ZEC). Aidha, alinukuu Ibara ya 28 (a) ya katiba ya Zanzibar ambayo inaeleza kwamba, kufuatana na katiba hii, mtu ataendelea kuwa rais mpaka:a. Rais anaefata ale kiapo cha kuwa Rais.

Baada ya hoja hizo akahitimisha kwa kusema, kwa kuwa tayari tume ya uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) imefuta uchaguzi, na kwa kuwa tayari tume hiyo imetangaza tarehe ya kufanyika uchaguzi mkuu mwingine visiwani Zanzibar, na kwa kuwa hakuna mtu yeyote alieapa kiapo cha urais tofauti na rais wa sasa wa Zanzibar, Dkt Shein. Hivyo Dkt Shein anatambulika kama rais wa Zanzibar na ana uhalali wote wa kuhudhuria katika uzinduzi wa Bunge la 11.

Na mwandishi maalum, Dodoma.

 








All the contents on this site are copyrighted ©.