2015-05-11 10:33:00

Ujumbe wa Papa Francisko kwa Patriaki Tawadros II


Jumapili, Papa Francisko  akikumbuka kukutana kwake na  Papa Tawadros II, wa Kanisa la Kikoptiki la Kiotodosi la Alexandria,  miaka miwili iliyopita,  kwa moyo wa urafiki na mshikano wa kiroho , alimpigia simu Papa Tawadros II.  

Mkurugenzi wa Ofisi ya Habari Vatican , Padre  Federico Lombardi, ametaarifu kwamba,  mazungumzo ya viongozi hawa wakuu wa Kanisa, kwa njia ya  simu , yalilenga hasa katika  mada kuu mbili: mapenzi kuendelea katika dhamira yao ya kujenga  umoja  wa Wakristo na mapendekezo kwa ajili ya kuwa na sherehe moja ya Siku Kuu ya Pasaka.

 Papa Francisko  katika maelezo yake alimshukuru Mungu kwa  umoja na urafiki unaounganisha  katika  safari ndefu ya urafiki  kati ya Jimbo la Papa na Jimbo la Mtakatifu Marko, ambayo ni jumuiya ya Wakristo wa Misri na Mashariki ya kati, Wakristo wanaoendelea kuwa mashahidi jasiri wa Ukristo. Na  kwa namna ya kipekee akilitaja kanisa la Kikoptiki ambalo hivi karibuni waamini wake wametoa ushuhuda wa kifodini  kwa ajili ya imani yao. Papa amewaombea  kafara hao wapokelewe katika ufalme wa Mungu .

Na aliendelea kumshukuru Mungu , kwa hatua zilizokwisha pigwa katika njia ya kutembea pamoja kirafiki , wakiwa wameungana katika kifungo cha ubatizo . Na kwamba hata kama umoja huo haujawa kamili, kuna mambo mengi  msingi yanayowaunganisha kuliko yale yanayowatenganisha. Na hivyo akaomba,  wadumu katika  njia hii hadi kufikia umoja kamili na kukua katika upendo na maelewano.

Katika maelezo yake , Papa  kwa namna ya pekee, alionyesha kutiwa nguvu na Tume ya Pamoja ya Kimataifa ya Mazungumzo ya Kiteolojia, kati ya Kanisa Katoliki  na Makanisa ya Mashariki ya Kiotodosi ambayo hivi karibuni imehitimisha rasimu  juu ya  kazi za Umoja katika Maisha ya Kanisa la Mwanzo na athari zake kwa ajili ya kutafuta  ushirika kamili leo hii.  Hivyo akaonyesha matumaini yake kwamba, Papa Tawadros II,  ataweza kutoa mchango wake katika majadiliano haya muhimu kwa ajili ya kutoa matunda mengi mazuri.  Na anafurahi kwamba, Upatriaki wa Jimbo la Mtakatifu Marko,  utakuwa  mwenyeji wa Mkutano ujao wa Tume hiyo  mjini Cairo. 

Na alionyesha kujali mahangaiko na mateso ya Wakristo, akisema  duniani kote wanakabiliwa na changamoto zinazofanana ambazo zinahitaji kufanya kazi kwa pamoja. Na alipokea kwa mikono miwili uteuzi wa mwaka jana wa wajumbe watakao shiriki kaika Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia, Anatumaini ushirikiano katika  suala hili, utaendelea na hasa katika kupata ufumbuzi kwa masuala yanayohusiana na ndoa mseto. 








All the contents on this site are copyrighted ©.