Ifuatayo ni taarifa ya uchunguzi wa awali kumhusu Ndugu Eliakim C. Maswi, Katibu mkuu, Wizara ya Nishati na Madini kuhusiana na sakata ya Escrow iliyotibua hali ya hewa kisiasa, kidini na kijamii nchini Tanzania.
Utangulizi
Katika mkutano wake wa 16 na 17, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja
na mambo mengine, lilijadili Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali
iliyotokana na Taarifa ya Ukaguzi wa Akaunti ya Tegeta Escrow uliofanywa na Mdhibiti
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Baada ya majadiliano, Bunge lilipitisha maazimio
kadhaa yaliyoelekezwa kwa Serikali kwa ushauri na utekelezaji. Mojawapo ya maazimio
hayo yalimtaja Ndugu Eliakim C. Maswi, ambaye ndiye Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati
na Madini, kuwa amehusika kijinai au kimaadili katika miamala iliyotokea katika akaunti
ya Tegeta Escrow.
Wakati anahutubia Taifa kupitia Wazee wa Dar es Salaam tarehe 22 Desemba, 2014, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alisema ifuatavyo:- “Kuhusu Katibu Mkuu wa Wizara
ya Nishati na Madini, kwa vile ni Mtumishi wa Umma, anatawaliwa na Sheria na Kanuni
za Utumishi wa Umma. Hivyo, nimeshaelekeza Mamlaka kuchunguza tuhuma zake na hatimaye
ikibainika ana makosa hatua za kinidhamu zitachukuliwa.”
Tuhuma dhidi ya Ndugu Eliakim C. Maswi zimeshughulikiwa katika ngazi mbili tofauti.
Amechunguzwa na Sekretarieti ya Maadili ya Umma, kisha baada ya hapo alichunguzwa
pia na Kamati ya Uchunguzi wa Awali iliyoundwa na mamlaka yake ya nidhamu.
Sekretarieti ya Tume ya Maadili
Kifungu 18 (2) (c) na (3) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kinaipa Sekretarieti
ya Maadili ya Viongozi wa Umma mamlaka na uwezo wa kuchunguza tuhuma yoyote ya kuvunjwa
kwa maadili ya uongozi wa umma yanayotawaliwa na Sheria hiyo. Tuhuma dhidi ya Ndugu
Eliakim C. Maswi zilizomo kwenye maazimio ya Bunge zinatawaliwa na Sheria hiyo.
Katika kutekeleza majukumu yake, Sekretarieti ya Maadili ya Umma ilifanya uchunguzi
wa awali na kisha kumhoji Ndugu Eliakim C. Maswi tarehe 19 Desemba, 2014. Sekretarieti
ya Maadili ya Viongozi wa Umma haijabaini kuwepo kwa maslahi binafsi katika uamuzi
uliofanywa na Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini wa kuruhusu fedha za Akaunti
ya Tegeta Escrow kutolewa. Aidha, hawakubaini ukiukwaji wowote wa maadili ya viongozi
wa umma uliofanywa na Ndugu Eliakim C. Maswi. Waliona kuwa yote aliyoyafanya yalizingatia
matakwa ya Sheria, ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na ridhaa ya TANESCO.
Hivyo, Sekretarieti ya Maadili haikuona msingi wowote wa kuendelea na shauri la Ndugu
Eliakim C. Maswi, na wamelihitimisha.
Kamati ya Uchunguzi wa Awali ya Mamlaka ya Nidhamu: Kwa mujibu wa Kifungu 4(3) (d)
cha Sheria ya Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002 (kama ilivyorekebishwa) Katibu
Mkuu Kiongozi ndiye Mamlaka ya Nidhamu ya Makatibu Wakuu.
Kwa kuzingatia Azimio husika la Bunge, na kwa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Katibu Mkuu Kiongozi aliunda Kamati ya Uchunguzi wa Awali dhidi ya Ndugu
Eliakim C. Maswi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, chini ya Kifungu cha
36 cha Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003 kinachotamka ifuatavyo:-
“Where it is necessary to institute disciplinary proceedings against a public servant,
the disciplinary authority shall make preliminary investigations before instituting
disciplinary proceedings.”
Kwa mamlaka aliyonayo chini ya Kanuni 35(2)(b) na Kanuni 37 ya Kanuni za Utumishi
wa Umma za mwaka 2003, Katibu Mkuu Kiongozi alimpumzisha Bwana Eliakim C. MASWI kutekeleza
majukumu yake ya kazi ya Katibu Mkuu ili kupisha uchunguzi wa awali. Uchunguzi wa
awali ulifanyika chini ya Kanuni ya 36 ya Kanuni za Utumishi wa Umma zilizotajwa,
pamoja na Kifungu 4(3) (d) cha Sheria ya Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002, kama
ilivyorekebishwa.
Kwa mamlaka aliyonayo chini ya Kanuni zilizotajwa kwenye ibara 3.3 hapo juu, Katibu
Mkuu Kiongozi aliteua Kamati ya Uchunguzi wa Awali na kuipa Hadidu za Rejea zifuatazo:
3.4.1 Kubainisha wajibu na madaraka halisi ya Katibu Mkuu, Wizaraya Nishati na Madini,
kwenye uendeshaji wa TANESCO kwa ujumla, na hususan kwenye kufungua, kuendesha na
hatimaye kufungwa kwa akaunti ya Tegeta Escrow.
3.4.2 Kubainisha na kupata maelezo ya kina juu ya kuhusika kwa Bwana Eliakim C. Maswi
katika mchakato na mtiririko mzima wa akaunti ya Tegeta Escrow, tangu kufunguliwa
hadi kufungwa.
3.4.3 Kubainisha na kupata maelezo ya kina iwapo kuna jambo lolote ambalo Bwana Eliakim
C. Maswi alilifanya au ambalo alipaswa kulifanya lakini hakulifanya, linalomstahilisha
achukuliwe hatua za nidhamu.
3.4.4 Kubainisha na kupata maelezo ya kina iwapo katika hatua yoyote ya mchakato na
mtiririko wa tangu kufunguliwa hadi kufungwa kwa akaunti ya Tegeta Escrow, Bwana Eliakim
C. Maswi alifanya jambo lolote linalodhihirisha matumizi mabaya ya mamlaka yake kama
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, kwa namna iliyosababisha hasara ya aina
yoyote ile kwa Taifa la Tanzania.
Kubainisha na kupata maelezo ya kina iwapo katika hatua yoyote tangu akaunti ya Tegeta
Escrow ilipofunguliwa hadi ilipofungwa, Bwana Eliakim C. Maswi hakuchukua tahadhari
ya kutosha kulinda maslahi ya umma na kusababisha kupotea kwa fedha za umma kwa uzembe
au matumizi mabaya ya madaraka.
Kubainisha iwapo kuna mahali popote katika mchakato wa akaunti ya Tegeta Escrow ambapo
Bwana Eliakim Chacha Maswi alifanya jambo lolote linaloashiria kitendo cha kijinai,
au kukiuka maadili ya viongozi wa umma.
Kuandaa taarifa ya uchunguzi wa awali kwa msingi wa Hadidu za Rejea zilizomo humu
na kuiwasilisha kwa Katibu Mkuu Kiongozi. Taarifa hiyo, pamoja na mambo mengine, ipendekeze
hatua za kuchukuliwa kwa kila eneo ambalo Kamati itabaini umuhimu wa hatua kuchukuliwa.
Mapendekezo ya Kamati ya Uchunguzi wa Awali
Kamati haijabaini kosa lolote ambalo linaweza kusababisha Ndugu Eliakim Chacha Maswi,
Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini, kufunguliwa mashtaka ya kinidhamu kwa kukiuka
Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298 ikisomwa pamoja na Kanuni zake za mwaka 2003 kwa
kuruhusu Benki Kuu ya Tanzania kutoa fedha zilizokuwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow.
Hitimisho la Uchunguzi wa Awali
Uchunguzi wa Awali uliofanywa na Sekretarieti ya Maadili umebaini kuwa Ndugu Eliakim
C. Maswi hana makosa yoyote ya kimaadili katika mchakato wa fedha za akaunti ya Tegeta
Escrow. Hali Kadhalika Uchunguzi wa Awali uliofanywa na Kamati ya Uchunguzi wa Awali
iliyoundwa na Katibu Mkuu Kiongozi umebaini kuwa Ndugu Eliakim C. Maswi, “hakutenda
au kuhusika na jambo lolote linaloashiria vitendo vya jinai au kukiuka Maadili ya
Viongozi wa Umma”.
Ushahidi wa vielelezo uliotolewa kwenye Sekretarieti ya Maadili na kwenye Kamati ya
Uchunguzi wa Awali umejitosheleza kuthibitisha kwamba Ndugu Eliakim C. Maswi alitenda
kazi yake kwa kiwango kinachoridhisha kwa kufanya mawasiliano na mamlaka mbalimbali
na kwa nyakati tofauti kwa lengo la kuhakikisha na kujiridhisha kwamba kufungwa kwa
Akaunti ya Tegeta Escrow kunafanyika kwa usahihi.
Hakuna ushahidi wowote kuwa Ndugu Eliakim C. Maswi alikuwa miongoni mwa waliopata
mgao wa fedha au fadhila yoyote kutokana na kufungwa Akaunti ya Tegeta Escrow.
Kwa nafasi yake ya mamlaka ya nidhamu Katibu Mkuu Kiongozi, ameridhika kuwa Ndugu
Eliakim C. Maswi hana makosa yoyote aliyoyafanya katika mchakato wa akaunti ya Tegeta
Escrow yanayostahili adhabu. Hivyo, mchakato wa kinidhamu, kimaadili na kijinai dhidi
yake umefikia mwisho wake. Mwenye mamlaka ya uteuzi atatafakari taarifa hizi na kuamua
cha kufanya kuhusu ajira yake baadaye.
All the contents on this site are copyrighted ©. |