Ifuatayo ni taarifa ya uchunguzi wa malalamiko yaliyotolewa kutokana na utekelezaji wa Operesheni tokomeza ujangiri iliyopania kupambana na ujangili unaotishia urithi wa Tanzania hususan: Tembo, Faru, Nyati, Twiga na Pundamilia. Operesheni hii ililalamikiwa na baadhi yaw a Bunge, Serikali ikaunda Tume maalum, haya ndiyo matokeo yake.
Kasoro nyingine ni askari wengi kuingia kwenye nyumba kwa wakati mmoja. Aidha,
Tume imebaini walalamikaji wengine waliongeza chumvi katika ushahidi wao kuhusu idadi
ya mali na fedha zilizopotea au kuibiwa na hivyo ushahidi wao kutoaminika au kuthibitika.
5.6 Tume ilichunguza malalamiko ya kubakwa wakati wa utekelezaji wa Operesheni. Matukio
yaliyochunguzwa na Tume yalikuwa katika Kijiji cha Iputi, Wilaya ya Ulanga, Mkoa wa
Morogoro na Kijiji cha Mwantimba Wilaya ya Bariadi, Mkoa wa Simiyu na Wilayani Sikonge.
Hata hivyo wote waliodai kubakwa hawakujitokeza mbele ya Tume kutoa ushahidi wao,
hivyo Tume haikuweza kuchunguza malalamiko yao. Alijitokeza mlalamikaji mmoja Wilayani
Ulanga, Morogoro, lakini Tume haikuridhika na maelezo yake, ambayo hayakutosheleza
kubainisha kosa kwenye utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
5.7 Tume ilibaini kuwa wapo watuhumiwa waliofikishwa mahakamani na kutiwa hatiani
na wengine kuachiwa. Tume imeona kuwa hatua hii ilikuwa sahihi kisheria. Lakini Tume
ilibaini pia kuwa baadhi ya watuhumiwa hawakufikishwa mahakamani. Badala yake maafisa
wa Operesheni walijichukulia mamlaka ya kutoa adhabu kwa watuhumiwa kama vile kukamata
na kuzuia mali zao, kuchoma moto nyumba na mali zilizokuwa kwenye maeneo ya hifadhi,
kuua au kujeruhi mifugo iliyokutwa kwenye maeneo ya hifadhi au kuuza kwa mnada ng’ombe
waliokamatwa kwenye maeneo ya hifadhi. Hatua nyingine inayolalamikiwa ni kuchukua
bunduki zinazomilikiwa kisheria.
5.8 Tume imebaini kwamba katika baadhi ya maeneo askari wa Operesheni walichoma nyumba
moto kwa madai ya nyumba hizo kujengwa kwenye hifadhi. Malalamiko hayo yalitoka katika
Wilaya za Mlele na Mpanda, Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Momba, Mkoa wa Mbeya; Wilaya
za Nkasi na Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa; na Wilaya ya Simanjiro, Mkoa wa Manyara. Katika
uchunguzi wa matukio haya Tume imebaini yafuatayo:
Wanakijiji hawakupewa taarifa ya kutosha kuhamisha mali zao kabla ya kuchoma nyumba
zao;
Baadhi ya wanakijiji walipoteza vyakula na mali zao katika zoezi hilo la uchomaji
moto;
Kuna vijiji vilivyosajiliwa lakini sehemu ya vitongoji vyake viko ndani ya Hifadhi
za Taifa; Kuna maeneo ya hifadhi au ushoroba (buffer zone) ambayo hayana alama za
mipaka kati ya hifadhi au ushoroba na vijiji husika; Kuna nyumba ambazo hazikuwa kwenye
eneo la hifadhi au ushoroba na hivyo zilichomwa moto kinyume cha sheria. Baadhi ya
matukio na malalamiko ya kuchomewa moto nyumba yalitokea kabla ya Operesheni.
5.9 Uchunguzi wa Tume umebaini kuwepo kwa tatizo kubwa la wafugaji kutoka nje ya nchi
na wafugaji wenyeji kuingiza mifugo yao katika Mapori ya Akiba, Hifadhi ya Misitu,
Maeneo Oevu na Hifadhi za Taifa. Maeneo yaliyoathirika sana na tatizo hili ni Hifadhi
ya Taifa ya Serengeti, Pori la Akiba la Kigosi – Moyowosi, Pori la Akiba la Maswa,
Mapori ya Akiba ya Biharamulo – Burigi – Kimisi na Pori la Akiba la Kijereshi.
Katika baadhi ya maeneo imethibitika kwamba wapo ng’ombe waliouawa kwa kupigwa risasi
baada ya kukutwa ndani ya hifadhi. Aidha, Tume imeridhika kwamba kuna ng’ombe wa walalamikaji
waliokamatwa na kuuzwa kwa mnada. Uuzaji wa ng’ombe katika tukio hili haukuzingatia
utaratibu wa kisheria.
5.10 Tume ilipata ushahidi kwamba katika maeneo mbalimbali askari wa Operesheni walikamata
au kuchukua bunduki, risasi pamoja na vitabu vyake hata kwa silaha zinazomilikiwa
kihalali. Maeneo ambayo yalikuwa na malalamiko ya watu kuchukuliwa silaha zao ni mikoa
saba (7) ambayo ni Katavi, Mbeya, Lindi, Morogoro, Tabora, Manyara na Pwani ambapo
jumla ya watu sitini na mbili (62) walijitokeza mbele ya Tume kulalamika tukio hili.
6.0 Hatua Zitakazochukuliwa na Serikali
6.1 Baada ya kupitia kwa kina taarifa ya Tume, pamoja na mapendekezo ya Tume, Serikali
itafanya yafuatayo: Hatua za kimashtaka zitaendelea kwa shauri la mauaji ambalo upelelezi
wake umekamilika na hatua za kiuchunguzi zitaendelea kwa mashauri mengine nane (8)
ya mauaji ambayo upelelezi wake haujakamilika;
Hatua za kisheria na kiutawala zitachukuliwa dhidi ya watuhumiwa waliothibitika kuwatesa
watu 15 wakati wa Operesheni; Hatua za kiuchunguzi zinazofanywa na TAKUKURU kuhusu
tuhuma za rushwa na udanganyifu zilizothibitika zitaendelea;
Silaha zinazodaiwa kumilikiwa kihalali zitafanyiwa uhakiki na ukaguzi wa kina kuhusu
umiliki na matumizi yake na endapo hakutakuwa na sababu nyingine za kisheria za kuzuia
urejeshwaji, wamiliki warejeshewe silaha zao kwa mujibu wa sheria na taratibu; Mali
ambazo zimethibitika kuchukuliwa wakati wa Operesheni kwa tuhuma za kuhusishwa na
uvunaji haramu wa mazao ya misitu zirejeshwe endapo hakutakuwa na sababu za kisheria
kuendelea kuzishikilia;
Serikali itafanya uhakiki wa vijiji ambavyo vimesajiliwa na vimo ndani ya hifadhi
ili kutatua migogoro ya ardhi kati ya hifadhi na vijiji. Aidha, Serikali itahakikisha
kunakuwa na ushirikiano wa karibu kati ya Msajili wa vijiji au mamlaka husika na Wizara
ya Maliasili na Utalii ili kuepuka kusajili vijiji ndani ya maeneo ya hifadhi;
Wizara ya Maliasili na Utalii itatayarisha kanuni zitakazoweka utaratibu wa kuwaondoa
watu waliovamia na kujenga makazi katika hifadhi; Sheria zote zinazolinda maeneo ya
hifadhi zitafanyiwa marekebisho ili kuongeza adhabu kwa kosa la kuingiza mifugo kwenye
Hifadhi bila kujali uraia wa wamiliki wa mifugo hiyo;
Kwa vile Tume imejiridhisha na faida kubwa na mafanikio ya Operesheni Tokomeza, Serikali
itaendelea na Operesheni kama hizo kadri itakavyojitajika ili kuokoa maliasili za
Taifa, ikiwemo wanyama, hifadhi na misitu. Hata hivyo ushauri wa Tume juu ya kuboresha
upangaji, usimamizi na utekelezaji wa Operesheni hizo itazingatiwa kikamilifu.
7.0 Mawaziri Waliojiuzulu
Tume ilijiridhisha kuwa Mawaziri wote waliojiuzulu, yaani Mhe. Dkt. Emmanuel J. Nchimbi,
Mb., Mhe. Balozi Khamis Kagasheki, Mb., Mhe. Mathayo D. Mathayo, Mb., na Mhe. Shamsi
V. Nahodha, Mb., hawakuhusika moja kwa moja na makosa yoyote ya utekelezaji kwenye
Operesheni Tokomeza. Hivyo, waliwajibika kisiasa tu na hakuna hatua nyingine inayostahili
dhidi yao.
All the contents on this site are copyrighted ©. |