Wakristo Duniani kote, wameanza rasmi adhimisho la Siku Tatu Kuu za Pasaka kwa Ibada ya Misa ya Kubariki mafuta ya Krisma, ambayo hupakwa waamini wakati wa ubatizo,upadrisho, au katika hatari za kifo. Ibada hii pia hujulikana kama ni sherehe ya Mapadre. Baba Mtakatifu Francisco kwa ajili hii , aliongoza Ibada ya Misa katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro la Vatican, na ilihudhuriwa na mamia ya Mapadre.
Katika homilia yake, Papa alilenga kuwatia shime Mapadre ili wasichoshwe na shughuli nyingi zinazowakabili katika utume wao, wajiweke chini ya ulinzi wa Kristo, Kuhani Mkuu., kama Neno la Mungu linavyonena, Mkono wangu utakuwa thabiti kweke na kiganja changu kitamtia nguvu( Zab 89;21) . Papa alitaja bayana kwamba, kipaumbele cha kwanza kwa kazi za Padre ni kupeleka habari njema kwa maskini, kutangaza uhuru kwa wafungwa na kuwaponya walio na upofu wa kiroho . Ni kutangaza habari ya ukombozi kwa waliosetwa na kutangaza habari za neema ya Bwana. Na kama Nabii Isaya anavyoeleza ni kuwafariji waliovunjika moyo kwa taabu na matatizo.
Baba Mtakatifu ameonyesha kutambua kuwa, utume huu si kazi rahisi kama ilivyo ajira nyingine, kama vile kazi za kuendesha ofisi au kusimamia ujenzi wa ukumbi wa Parokia au kutengeneza viwanja vya michezo ya vijana Parokiani....Lakini ni utumishi wenye kuitikia wito wa Yesu wa kuwa mtumishi wa wote, kutumikia kwa huruma inayogusa kiini cha moyo wa mtu, ni kukubali kuongozwa na kushiriki kikamilifu katika kutekeleza wito huo. Ni wito unaodai kila anayeuitikia kama kuhani au Padre, kufurahi na watu wote, iwe wanandoa, watoto wadogo wanaotaka kubatizwa ,vijana wachumba, na familia. Lakini pia Upadre unadai kuteseka na watu katika hali zao mbalimbali , wagonjwa, hasa wlaiopoteza matumaini ya kupona, wale waliopokea Mpako wa wagonjwa wakiwa katika vitanda vyao mahospitali au majumbani, na pia unadai kuomboleza na wale wanaozika mpendwa. Haya yote, Papa anasema , wakati mwingine yanaweza kumchosha Padre .
Papa aliendelea kuwaasa Mapadre kwamba ,ili wasipate kuchoshwa na kazi nyingi, ni muhimu kwao Mapadre, kujua hali ya maisha ya jamii wanayoihudumia, kinachoendelea katika maisha ya watu wao, hasa kinachoendelea katika nyoyo za watu wao, kujua imani yao na udhaifu wa watu wao, hivyo kushiriki katika mateso, hisi na shauku za watu wao. Papa anakiri, kweli bila kuongozwa na kuishi na Kristo, utume huu unaweza kuwa mzito na wa kuchosha,wenye kuurarua moyo wa Padre vipande vipande. Lakini Padre hatakiwa kuchoka kuhudumia wake , daima amatakiwa kuwa na hamu , kuisikia kwa karibu harufu ya kondoo wake na hivyo kuendelea kuhudumia kwa uaminifu,daima akiongozwa na maneno : Pokeeni, Mwili wa Kristo, kunyweni damu ya Kristo. Kwa njia hiyo, maisha ya Kipadre yanajijenga katika msingi wa huduma, kuwa karibu na watu wa Mungu na hivyo daima hawatasikia kuchoka.
Papa aliendelea kuwashirikisha Mapadre aina mbalimbali za hali zinazoweza kuleta uchovu , akibainisha uchovu wa aina mbali, ule unaoletwa na ibilisi na majeshi yake, nyenye kunyemelea kuifisha roho, kwa kuibui hali za kukatisha tamaa, au uchovu wa kishetani, usioonyesha matunda ya kazi zinazofanyika. Wakati huohuo Papa aliekea katika mafundisho ya Injili ambamo mnatajwa uchovu wenye kuzaa matunda mazuri ya furaha na kicheko kamili, kama ilivyokuwa kwa Yesu, watu walimfuata , familia zikimletea watoto kwa ajili ya kupata baraka, wengine wakitafuta kuponywa , watu walioandamana na marafiki zao kwa wingi kumsikiliza mwalimu mkuu, kusikiliza ujumbe wa Mungu wa kusisimua, hata hawakumpa nafasi Yesu ya kula. Kamwe Bwana hakuchoka kuwa kuwahudumia watu , kuwa karibu na watu . Kinyume chake uwepo a watu ulimpa nguvu mpya. Kwa hiyo Papa anasema, shughuli nyingi kwa Padre, ni wakati wa Padre kuchota neema .. Papa alieleza Mapadre akiwatazamisha jinsi watu wanavyowapenda Mapdre wao. Aliwahakikishia watu wana haja ya kuwa karibu na wachungaji wao! Na kwamba waamini ni aminifu kwa Padre wao,na kamwe hawawezi kumwacha Padre wao katika mahangaiko bila msaada labda kama yeye Padre anakuwa ni Padre wa kujifungia ndani ya ofisi au Padre mwenye kufumbia macho matatizo ya wanaparokia wake. Padre mwenye kujikweza na kuvalia mawani ya jua, matatizo ya wanaparokia wake .
Papa Francisko ameendelea kutafakari utume wa Kipadre, akisema Padre hachoshwi na harufu ya kondoo wake , bali huendelea kutoa tabasamu la furaha ya baba kwa watoto wake. Mapadre ni marafiki wa Bwana Harusi, na hiyo ndiyo furaha yao. Iwapo Yesu ndiye Mchungaji miongoni mwao, basi hawawezi kuwa wachungaji wenye kununanuna , walalamishi au wenye uchovu mbaya. Daima wataweza kusikia harufu ya kondoo na kutoa tabasamu la baba .... kama Yesu alivyosema, "Haya, njoni kwangu ninyi nyote , mliobarikiwa na Baba yangu" (Mt 25:34).
Aligeukia tena uchovu meingine alioita “uchovu wa maadui” , unaoletwa na shetani na marafiki zake, ambao kamwe hawalali katika kazi yao ya kuziba masikio, ili neno la Mungu lisiweze kujipenyeza kwa watu. Jeshi hilo hufanya kazi bila kuchoka, kunyamazisha neno hilo , au kupotosha maana yake. Anasema ili Padre aweze kupambana na hili, zaidi sana ni kutenda mema bila kuchoka . Ni kujifunza na kujenga uvumilivu katika jinsi ya kukabiliana nao kujiweka chini ya ulinzi wa Bwana. , kwa kuwa ni Bwana peke yake inayeweza kuwalinda. Hili humsaidia Padre kutoruhusu kujiweka chini ya ulinzi wa mwovu na kejeli za waovu. Katika hali hii ya uchovu, Bwana anasema hivi: "Kuwa na ujasiri! Mimi nimeushinda ulimwengu! "(Yohana 16:33).
Papa alikamilisha akisema, ukuhani hutakatifushwa na Yesu mwenyewe , na hivyo, Makuhani wana haki ya kufurahia kutimiza wajibu wao kwa huru kamili na bila hofu, au kujiona kuwa na hatia, badala yake, wajawe na hamu ya kutaka hata kwenda nje, hata mwisho wa nchi, na kila pembe ya dunia, kupeleka habari hii ya wokovu wa bure kwa binadamu wote, na hasa kwa wanyonge,maskini na waliotekelezwa zaidi , kwa utambuzi kwamba, daima Yesu yu pamoja nao hata katika miisho ya dunia. Papa alieleza na kuwataka Mapadre kutafakari juuya utume wao kwa ajili ya kupata uelewa zaidi, juu ya uchovu chanya, uchovu wenye kuzaa matunda bora na neema katika njia zake bora.
All the contents on this site are copyrighted ©. |