Ndugu msomaji, tunaongozwa katika tafakari hii na vifungu vifuatavyo kutoka katika
Maandiko Matakatifu! Unaweza kuanza kwanza kwa kujisomea na baadaye tafakari hii itakusaidia
kulifahamu vyema zaidi Neno la Mungu kwa Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Kwaresima,
Mwaka Be wa Kanisa. Mwa. 22;1-2,9a, 10-13, 15-18 Rum. 8;31-34 Mk. 9;
2-10.
Katika Makanisa ya Bizantina huko Ulaya mashariki, sura ya Kristo
huoneshwa kama bwana na mtawala wa muda na wakati wote. Ndiyo tafakari yetu ya leo
– sura kamili ya Kristo inawekwa mbele yetu. Sote twajua kuwa maisha ya Kristo ni
fumbo. Lakini yeye ametuonesha Mungu na hivyo twaweza kuongea juu ya utukufu wa Mungu
uliojionesha kwetu. Hali hii yatuonesha kuwa Yesu alijionesha kwetu na hivyo hakubaki
tu fumbo.
Sikia sauti ya Mungu – huyu ndiye mwanangu mpendwa wangu msikilizeni
yeye. Hilo fumbo limefunuliwa kwetu. Kwa tamko hili urithi wetu kama wana wa Mungu
unawekwa wazi. Leo Mungu ajionesha kwetu. Mt. Yohane wa Msalaba anasema – tangu Baba
alipotamka pale mlimani Tabor – huyu ndiye mwananngu mpemdwa msikilizeni yeye, Mungu
Baba kwa namna moja alikamilisha ufunuo wake, akabaki bubu. Alisema kila kitu. Hana
kitu kingine kipya cha kufunua. Alikamilisha ufunuo wake kwetu.
Alama zilizopo:
a. Mlima - mahali pa agano kati ya Mungu na mtu – sasa yaonekana wazi kuwa mlima mpya
wa Mungu ni Yesu – Yesu ni mahali pa kukutana kati ya Mungu na watu – siyo tena mlimani.
B. Mawingu na kivuli – yaonesha uwepo wa Mungu – mjumber sasa ni Kristo. C. Sauti
ya Mungu; huyu ndiye mwanangu – Mungu anajifunua kwetu, na kusema yeye ni nani - sasa
tuna dunia mpya, namna mpya ya kuelewa ukweli, namna mpya ya kuishi, namna mpya ya
kuishi imani yetu na namna mpya ya kuishi maisha yetu – pamoja na Kristo tunao ufahamu
mkubwa kuhusu Mungu. Yesu ndiye sheria mpya, ni juu zaidi ya sheria za mwanadamu na
manabii.
Kugeuka sura – ni utangulizi wa Pasaka – tunapoitwa sisi sote katika
ushuhuda wa imani yetu ya kila siku – hivyo maisha yetu yahitaji ufunuo wa Mungu hata
katika maisha ya kawaida. Kugeuka sura – huangaza matembezi yetu ya imani-mitume waliona
utukufu wa Mungu. kwa maisha yetu ya kila siku – wengine wanaweza kuuona utukufu wa
Mungu?
Kugeuka sura – huangaza pia maisha yetu ya zamani –mazuri na mabaya
– yale mazuri yanaendelezwa na mabaya yanaachwa. Neno la Mungu leo hii – lazima lituvuruge
katika imani yetu – kile kilichodhaniwa kuwa fumbo sasa si fumbo tena kwa maana ya
kuwa Mungu yu pamoja nasi na ameonekana kwetu na ametuambia wazi kile tutakiwacho
kufanya. Hakika imani yahitaji kusaidiwa na matokeo hai – leo tunapata bahati hiyo.
Ni msukumo na changamoto kwetu sisi kuishi kama watu wa mwanga na si wa giza tena.
Tumgeukie Mungu mwanga wa kweli ili atuangaze na atuongoze. Je, nasi tumegeuka sura
zetu au tumebaki hivyo hata baada ya kukutana na Mungu?