Maendeleo makubwa yaliyofikiwa na Shirikisho la vyama vya ushirika nchini Italia ni
sehemu ya mchango uliotolewa na Kanisa nchini Italia na ni mkakati wa kupambana na
ukosefu wa fursa za ajira na athari katika maisha ya kijamii; na huu ukawa ni mwanzo
wa Mafundisho Jamii ya Kanisa yanatoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya
binadamu, ili kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu yanayojikita katika mshikamano
unaoongozwa na kanuni auni. Huu ni utajiri mkubwa unaofumbatwa katika maisha na utume
wa Kanisa kama alivyobainisha Papa Leo wa kumi na tatu.
Hii ni sehemu ya hotuba
iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi tarehe 28 Februari 2015 alipokutana
na kuzungumza na wajumbe wa Shirikisho la vyama vya ushirika nchini Italia kwa kuwataka
kuangalia mbele kwa imani na matumaini; kwa kuwajibika sanjari na kuibua vyama vya
ushirika, ili kupambana na utandawazi usiojali wala kuguswa na mateso na mahangaiko
ya watu kutokana na sera na mikakati potofu ya masuala ya uchumi na fedha.
Utandawazi
usiojali utu na heshima ya binadamu umepelekea kuibuka kwa wimbi kubwa la watu wasiokuwa
na ajira, umaskini wa hali na kipato; utu na heshima ya mwanadamu vimewekwa rehani
badala ya utandawazi kukoleza mshikamano kama alivyotamani kuona Papa Leo wa kumi
na tatu. Hii inapaswa kuwa ni changamoto endelevu kwa vyama vya ushirika kuhakikisha
kwamba, vinashirikisha: uzoefu, mbinu na mafanikio ili kujenga matumaini mapya katika
mifumo ya kiuchumi inayokatisha tamaa.
Wanachama wa vyama vya ushirika waendelee
kuwa ni Manabii kwa kuzingatia tunu msingi za kimaadili na utu wema. Wasaidie kufufua
na kuendeleza sekta ya kilimo; wawekeze katika ujenzi wa makazi ya watu pamoja na
kutoa mikopo nafuu itakayowasaidia watu kujikwamua na athari za myumbo wa uchumi kimataifa
kwa kuzingatia mambo makuu yafuatayo:
Kwanza kabisa, Baba Mtakatifu anavihamasisha
vyama vya ushirika kuwa ni chachu ya maendeleo miongoni mwa maskini, ili kutengeneza
fursa za ajira kwa wasiokuwa na kazi, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa vijana wa
kizazi kipya, kwani ukosefu wa ajira unavuruga matumaini yao bila kusahau kuwajengea
wanawake uwezo wa kiuchumi pamoja na kuokoa makampuni yanayokufa na hivyo kusababisha
hasara kubwa katika jamii.
Pili, Baba Mtakatifu anawaalika wajumbe wa vyama
vya ushirika kuwekeza katika sekta ya huduma ya afya na jamii, kwani kutokana na
kupanda kwa gharama ya maisha na kushuka kwa hali ya maisha, kuna kundi kubwa la watu
ambalo halina uwezo wa kugharimia huduma za afya ya jamii. Kwa kuwekeza katika huduma
kama hii ni mchakato wa kumwilisha upendo kati ya watu na kuwatuliza; hii ndiyo kanuni
ya auni kadiri ya Mafundisho Jamii ya Kanisa. Huu unaweza kuwa ni mnyororo wa upendo
na mshikamano na Kanisa katika utoaji wa huduma, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa
binadamu!
Tatu, Baba Mtakatifu anasema, sera na mikakati ya kiuchumi haina
budi kusaidia mchakato wa kuendeleza haki jamii, utu na heshima ya binadamu, ili kujenga
na kuimarisha uwajibikaji wa kijamii badala ya mtindo wa sasa wa kujielekeza katika
soko kwa kujikita katika ubinafsi na faida kubwa: mchakato wa uzalishaji na huduma
uwahusishe watu wengi zaidi, hiki ndicho kiini cha vyama vya ushirika katika asili
ya mzizi neno!
Nne, Baba Mtakatifu Francisko anawashauri wanaushirika kuwekeza
zaidi katika ustawi na maendeleo ya familia; kwa kufanya mlingano sawia kati ya kazi
na familia; wanawake wapewe fursa ya kutekeleza wajibu na dhamana yao ya kimama pamoja
na kukuza karama na vipaji vyao, lengo ni kuendeleza mafao ya wengi kwa ajili ya ustawi
na maendeleo yao, kwa kuweka pamoja rasilimali na kuonesha uwezo wa kuitekeleza nia
hii njema katika matendo. Kwa njia hii, utu na heshima ya binadamu vtadumishwa na
kuendelezwa; amani na utulivu vitashamiri ndani ya jamii pamoja na kuendelea kuwekeza
zaidi.
Fedha na mali visiwafanye watu kuwa watumwa wa Shetani, kwani hapa
ndio mwanzo mwa majanga kwa binadamu. Fedha isaidie kumhudumia mwanadamu katika ukweli
na haki, ili kujenga uchumi unaosimikwa katika ukweli kwa ajili ya mafao ya wengi.
Vyama vya ushirika vijitanue zaidi na zaidi kwa kushikamana na vyama vingine ili kupata
mwelekeo wa kimataifa. Huu ni mwaliko anasema Baba Mtakatifu Francisko kushirikiana
kwa karibu zaidi na Parokia pamoja na Majimbo yao; kwa kuheshimu karama na tofauti
zilizopo, lakini daima kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu wote.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.