2015-02-27 10:50:29

Yaliyojiri wakati wa ziara ya Rais Kikwete, nchini Zambia


Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mheshimiwa Edgar Chagwa Lungu amesema kuwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete katika maendeleo ya Tanzania na amani ya Bara la Afrika ni mambo yasiyotiliwa shaka tena, akitamani naye apate mafanikio kama Rais Kikwete. Aidha, Rais Lungu amesema kuwa Rais Kikwete ameonyesha kiwango kikubwa na cha juu cha uongozi, ambacho kinathibitishwa na aina ya mafanikio ambayo ameyaleta katika miaka yote ya uongozi wake.

Rais Lungu alifagilia na kusisitiza mafanikio hayo ya Rais Kikwete na uongozi wake kwa nyakati mbili tofauti, Jumatano, Februari 25, 2015, katika siku ya kwanza ya ziara rasmi ya siku mbili ya Rais Kikwete nchini Zambia kwa mwaliko wa Rais Lungu. “Nina mengi ya kujifunza kutoka kwa Mheshimiwa Kikwete ambaye kama mnavyojua anajiandaa kumaliza muda wake wa uongozi. Mimi bado mpya kabisa katika uongozi wa juu na hivyo nina mengi ya kujifunza kutoka kwake kwa sababu amefanikiwa sana katika uongozi wa nchi yake, “ Rais Lungu aliwaambia waandishi wa habari katika mkutano uliohudhuriwa na Rais Kikwete baada ya viongozi hao wawili kumaliza mazungumzo rasmi kati yao.

Akizungumza wakati wa dhifa ya taifa ambayo Rais Lungu alimwandalia Rais Kikwete kwenye Hoteli ya Taj Pamodzi mjini Lusaka, Rais Lungu alirudia kumpongeza na kumsifia Rais Kikwete kwa uongozi bora. “Umeonyesha uongozi wa kutukuka sana ambao unathibitishwa na mafanikio makubwa katika miaka yote ya urais wako. Umeimarisha, umesimamia na kudumisha utawala bora, umepanua sana uhuru wa kila aina katika Tanzania ukiwemo uhuru wa vyombo vya habari. Tunakupongeza kwa mafanikio hayo na baadhi yetu tunaoanza uongozi tunatamani sana kufuata nyayo zao,” alisema Rais Lungu na kuongeza:

“Mchango wako katika kusaka amani katika Bara la Afrika ni jambo la kupongezwa sana na ni chimbuko la heshima kwetu sote na kwa Bara letu lote. Mchango wako katika maendeleo ya Tanzania na Bara la Afrika ni mambo yasiyotiliwa shaka na yoyote. Ni matumaini yangu na nataka kufuata nyayo za uongozi wako.”

Wakati wa dhifa hiyo, Baba wa Taifa la Zambia, Mzee Kenneth Kaunda alikunwa mno na muziki wa Malaika uliokuwa unatumbuizwa na bendi moja kiasi cha kuingia uwanjani na kumkaribisha Rais Kikwete pamoja na Rais Lungu uwanjani na kwa pamoja wakasakata rumba. Rais Kikwete ambaye alikuwa Zambia kwa ziara rasmi kutokana na mwaliko wa Rais Lungu anakuwa kiongozi wa kwanza wa nje kutembelea Zambia rasmi tokea Rais Lungu ashike madaraka ya kuongoza Zambia mwezi uliopita.


Wakati huo huo, Zambia imeomba Tanzania kuiuzia nchi hiyo ya jirani gesi asilia kwa madhumuni ya kuzalisha umeme na kupanua wigo wa uzalishaji wa viwandani. Aidha, Tanzania na Zambia zimekubaliana kuifufua Reli ya TAZARA kati ya nchi hizo mbili kwa kukabiliana ipasavyo na changamoto na matatizo ambayo kwa muda sasa yamekuwa yanakwamisha utendaji bora wa reli hiyo iliyojengwa kwa nia ya kuiwezesha Zambia kupata njia ya kufikia baharini kwa urahisi zaidi na kusafirisha bidhaa zake kwenda nje.

Ombi hilo na makubaliano kuhusu TAZARA yalifikiwa, Jumatano, Februari 25, 2015 wakati wa mazungumzo rasmi kati ya nchi hizo mbili ikiwa ni sehemu ya ziara rasmi ya Kiserikali ya siku mbili iliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete katika Zambia kwa mwaliko wa Rais Edgar Chagwa Lungu. Mazungumzo hayo yalifanyika Ikulu ya Zambia, mjini Lusaka.

Katika mazungumzo hayo yaliyochukua muda mrefu, Rais Kikwete na Rais Lungu waliongoza nchi zao katika majadiliano kuhusu masuala mbali mbali ikiwa ni pamoja na ombi la Zambia kutaka kununua gesi kutoka Tanzania na jinsi ya kufufua Reli ya TAZARA. Wakati wa mazungumzo hayo, Rais Lungu alimwomba Rais Kikwete akubali Tanzania iuzie gesi asilia Zambia, ombi ambalo Rais Kikwete alilikubali bila kusita.

“Hakuna shaka kuwa tuko tayari kuwauzieni gesi asilia ndugu zetu wa Zambia. Linalohitajika ni kwa Zambia kuweza kujenga bomba la kusafirishia gesi hiyo kutoka Tanzania hadi Zambia. Mwambie yoyote ambaye anaweza kutoa mkopo wa ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kuwa Tanzania iko tayari kuwauzieni gesi,”alisema Rais Kikwete wakati wa mazungumzo hayo.

Kuhusu ufufuaji wa Reli ya TAZARA, viongozi hao wawili walikubaliana kuangalia changamoto za kiuongozi na utendaji, changamoto za kiufundi, changamoto za kisheria na changamoto za kimuundo, ambazo zinakwamisha uendeshaji wa ufanisi wa Reli hiyo. Reli hiyo yenye urefu wa kilomita 1,600 inaunganisha Dar es Salaam na Kapiri Mposhi, Zambia, ilijengwa kwa mkopo wa dola za Marekani milioni 500 kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China mwishoni mwa miaka ya 1960 na mwanzoni mwa miaka 1970.

Hata hivyo, Reli hiyo ilikabiliwa na changamoto kiasi cha kwamba sasa inachukua muda wa siku 12 kwa treni kusafiri kati ya vituo hivyo viwili vikuu wakati inachukua kiasi cha siku tano tu kwa magari kusafiri kati ya Dar es Salaam na Kapiri Mposhi. Aidha, Reli hiyo yenye uwezo wa kubeba mizigo tani milioni tano za mizigo, mwaka 2014, ilibeba mizigo yenye uzito wa tani 280,000 tu. Serikali ya China imekubali kimsingi kusaidia kuifufua Reli hiyo lakini baada ya kupokelewa kwa ripoti ya uchunguzi unaofanywa kuhusu chanzo na ukubwa wa matatizo yanayoikabili Reli hiyo.

Rais Kikwete akutana kwa kifungua kinywa na Mzee Kaunda, KK!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete Alhamis asubuhi, Februari 26, 2015, amekutana kwa kifungua kinywa na Mwanzilishi wa Taifa la Zambia na Rais wa Kwanza wa nchi hiyo, Mheshimiwa Kenneth David Kaunda. Aidha, Rais Kikwete ambaye amemaliza ziara rasmi ya Kiserikali ya siku mbili katika Zambia, ameweka shada la maua kwenye kaburi la Mama Betty Muntikhe Kaunda, hayati mke wa Mzee Kaunda.

Rais Kikwete ambaye amekuwa kiongozi wa kwanza wa nje kualikwa kutembelea Zambia kwa ziara rasmi tokea Rais mpya wa nchi hiyo, Mheshimiwa Edgar Chagwa Lungu kushika madaraka ya kuongoza nchi hiyo mwezi uliopita, amewasili nyumbani kwa Mzee Kaunda katika eneo la State Lodge Area, Leopards Hill, kiasi cha kilomita 26 kutoka mjini Lusaka, kiasi cha saa mbili na dakika 40 asubuhi.

Rais Kikwete na ujumbe wake wa watu wachache amelakiwa na Bwana Kaweche Kaunda, mmoja wa watoto wa Mzee Kaunda ambaye amemwongoza hadi kwenye kaburi la mama yake, Betty Kaunda, ambako Rais Kikwete ameweka shada la maua. Rais Kikwete amekaribishwa nyumbani kwa Mzee Kaunda na Mzee mwenyewe ambaye kama ilivyo jadi yake alikuwa ameshikilia kitambaa cheupe mkononi.

Baada ya kuweka saini kwenye kitabu cha wageni, Mzee Kaunda na Rais Kikwete walianza mazungumzo wakati wa kifungua kinywa na kwa saa mbili walizungumzia mambo mengi, hasa yale ya kijamii bila kuingiza siasa sana. Mazungumzo hayo yalihudhuriwa pia na watoto wawili wa Mzee Kaunda, Bwana Kaweche Kaunda wa kiume na Bibi Cheswa Kaunda Silwizya ambaye ni mtoto wa mwisho wa Mzee Kaunda na Hayati Betty Kaunda. Aidha, mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Zambia na Balozi wa Zambia nchini Tanzania.

Rais Kikwete amemwambia Mzee Kaunda: “Wewe ni mmoja wa mashujaa wetu katika Bara la Afrika. Mzee Kaunda wewe ni nyota wa Bara letu, ambaye umehamasisha na kuwatia moyo watu wengi kukabiliana na changamoto za maendeleo. Tunakushukuru sana kwa mchango wako katika maendeleo ya Bara letu na tutaendelea kukuenzi kwa mchango huu. Tunakutakia maisha marefu na afya njema sana.”

Rais Kaunda amemwambia Rais Kikwete kuwa nyumba hiyo ambayo anaishi kwa sasa iliyoko katika mazingira yenye mandhari ya kuvutia ya misitu ilijengwa kwa ajili yake na Rais wa tatu wa Zambia, Hayati Levy Mwanawasa. “Nyumba hii nilijengewa na Serikali ya Rais Mwanawasa.” “Rais Mwanawasa alifanya jambo zuri, muhimu na la wajibu kabisa kwa sababu unastahili nyumba yenye hadhi ya namna hii kwa mchango wako kwa wananchi wa Zambia na Afrika katika maisha yako,” Rais Kikwete amemjibu Mzee Kaunda.

Rais Kikwete alipotaka kujua siri ya afya yake nzuri kwa umri wake mkubwa, Mzee Kaunda ambaye anafikisha umri wa miaka 91 katika miezi miwili ijayo, amemjibu: “vegetarian life” akiwa na maana ya kuwa ameishi maisha yake yote akila chakula ambacho huliwa na watu wasiokula nyuma katika maisha yao. “Chakula changu kikuu ni ugali na maharage.”


Rais Kikwete ateta na Watanzania waishio Zambia

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete usiku Jumatano, Februari 25, 2015, amekutana na kuzungumza na mamia ya Watanzania waishio nchini Zambia, ikiwa sehemu ya ziara yake rasmi ya siku mbili ya Kiserikali katika nchi hiyo. Rais Kikwete akifuatana na Mama Salma Kikwete alikutana na Watanzania hao usiku kwenye Ubalozi wa Tanzania nchini Zambia, ambako alipata nafasi ya kujibu maswali yao na kuelezea kwa undani mafanikio ya maendeleo ambayo yanaendelea kupatikana nchini.

Rais Kikwete amekuwa kiongozi wa kwanza wa nje kualikwa kutembelea rasmi Zambia tokea Rais mpya wa nchi hiyo, Mheshimiwa Edgar Chagwa Lungu kushika madaraka ya dola mwezi uliopita, hatua inayoonyesha hali ya uhusiano mzuri katika ya nchi hizo mbili jirani na marafiki.

“Ukisoma magazeti yetu nchini na kufuatilia mijadala kwenye mitandao ya kijamii utadhani kuwa hakuna kinachofanyika na kuwa nchi nzima inaongelea katika siasa tu. Lakini tunaendelea kufanya mambo mengi iwe katika elimu, katika afya, kukabiliana na malaria na magonjwa wengine makubwa, kupambana na ukimwi, kusambaza umeme vijijini, mapambano dhidi ya ujambazi na majambazi, shughuli za miundombinu na ujenzi wa barabara pote tunafanya vizuri sana,”alisema Rais Kikwete na kuongeza:

“Wakati Serikali yangu inaingia madaraka ni asilimia 10 tu ya vijiji vyetu vilikuwa na umeme, sasa tunazungumzia asilimia 45 ya vijiji vya Tanzania vina umeme. Hapa tunazungumzia kiasi cha vijiji 5,000 kati ya vijiji 12,000 vya nchi yetu. Kwa ujumla, asilimia ya usambazaji umeme katika nchi yetu imepanda kutoka asilimia 10 ya mwaka 2006 hadi kufikia asilimia 36 kwa sasa. Siyo mafanikio madogo hata kidogo.”

Kuhusu hali ya ujambazi nchini, Rais Kikwete amesema kuwa upo ujambazi katika Tanzania, kama ilivyo kwa nchi zote duniani. “Lakini, hawa tutapambana nao hawawezi kutushinda nguvu, tutazama nao na tutaibuka nao tu.” Rais Kikwete pia ameelezea upanuzi mkubwa wa sekta ya elimu ikiwa ni elimu ya awali, ya sekondari na ya juu. “Katika elimu ya juu, kwa mfano, wakati tunaingia madarakani idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vyote ilikuwa ni 40,000 tu lakini sasa tunazungumzia wanafunzi 200,000.”

Katika afya, Rais Kikwete ameelezea uboreshaji mkubwa wa hospitali za mikoa na ujenzi wa huduma nyingine za afya zikiwemo zahanati na vituo vya afya katika vijiji na kata nchini. Aidha, Rais Kikwete amezungumzia hatua za kuongeza idadi ya madaktari nchini akisema kuwa kwa sasa idadi ya madaktari wapya kutoka Chuo Kikuu cha Tiba cha Muhimbili wameongezeka kutoka 200 hadi 400 kwa mwaka na kuwa idadi hiyo itakuwa kubwa zaidi wakati ujenzi wa Hospitali ya Mlongazila, nje tu ya Dar es Salaam, utakapokamilika.

Rais Kikwete pia alijibu maswali manane ya Watanzania hao ikiwa ni pamoja na lile kuhusu uraia pacha, misamaha ya kodi kwa Watanzania wanaorejea nyumbani, mikopo kwa wanafunzi wa kike wa Kitanzania ambao wanasomea masomo ya sayansi nje ya nchi, uwezekano wa Benki ya CRDB kufungua tawi katika Zambia, hatua za Serikali kupunguza idadi ya vizuizi vya barabarani, uwezekano wa Watanzania waishio nje kupata nafasi ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu na jinsi gani Serikali ya Tanzania inaweza kuwasaidia Watanzania waishio Zambia kufanya shughuli zao kwa uhuru zaidi.











All the contents on this site are copyrighted ©.