Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasaidizi wake wa karibu, Ijumaa asubuhi tarehe
27 Februari 2015 wamehitimisha mafungo ya maisha ya kiroho baada ya kukaa "Jangwani"
kwa muda wa siku saba, huku wakisali na kufunga, wakitafakari na kujipatanisha na
Mungu pamoja na jirani zao. Mafungo haya yameongozwa na Padre Bruno Secondin, Jaalim
mstaafu wa tasaufi mamboleo kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian, kilichoko
mjini Roma. Mafungo haya yameongozwa na maneno ya Nabii Eliya.
Baba Mtakatifu
kwa niaba ya wanamafungo wenzake, amemshukuru na kumpongeza Padre Bruno Secondin,
Mkarmeli kwa kazi nzuri aliyoifanya kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya maisha yao
kiroho na kimwili. Baba Mtakatifu anakiri kwamba, si rahisi kutoa mafungo ya maisha
ya kiroho kwa Mapadre, kwani viongozi hawa wakati mwingine ni "watata", lakini Padre
Secondin amefanikiwa kupandikiza mbegu ya Neno la Mungu.
Ni matumaini ya Baba
Mtakatifu kwamba, Mwenyezi Mungu atawasaidia ili mbegu hii iweze kukua na kuzaa matunda
yanayokusudiwa, huku wakitoka katika mafungo haya kwa kujivika Joho la Nabii Eliya,
mikononi mwao, lakini zaidi mioyoni mwao!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.