2015-02-26 11:07:02

Utu na heshima ya wafungwa magerezani!


Magereza panapaswa kuwa ni mahali ambapo mkosaji anapata fursa ya kuweza kujirekebisha kutokana na mapungufu yake, ili anapohitimisha adhabu yake, aweze kurudi tena ndani ya jamii na kuendelea vyema na maisha. Kwa miaka mingi mageregza nchini Malawi yalikuwa yanatisha kwa kutozingatia haki msingi za binadamu, utu na heshima yao, lakini hali kwa sasa imeanza kubadilika na kuboresha kutokana na changamoto kubwa iliyotolewa na Rais Arthur Peter Mutharika wa Malawi wakati alipokuwa anafunga mafunzo ya Askari Magereza 731 hivi karibuni.

Katika hotuba yake, Rais Mutharika aliwaambia Askari Magereza wamepewa dhamana ya kusaidia kurekebisha mwenendo wa wafungwa ili waweze kuchangia katika ustawi na maendeleo ya nchi na wala si kwa ajili ya kuwashikisha adabu. wachunguzi wa mambo wanasema, mambo yanabadilika pengine ni kutokana na ukweli kwamba, hata Rais mwenyewe alikwishawahi kuonja suluba ya kukaa Lupango", akashuhudia jinsi ambavyo magereza yalivyokuwa yamefurika kiasi cha kutishia usalama na maisha ya wafungwa na Askari Magereza wenyewe.

Sheria na marekebisho ya magereza ni mambo ambayo yanapokelewa kwa mikono miwili na wananchi wengi wa Malawi, hii ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wafungwa kutumikia vifungo vyao nje ya magereza kwa kufanya shughuli mbali mbali za kijamii badala ya kukaa muda wote magerezani. Hapa wachunguzi wa mambo wanasema, Serikali pia haina budi kuangalia mishahara na mazingira ambamo Askari Magereza wanafanyia kazi, ili kufanya maboresho makubwa zaidi katika kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.