Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Kwaresima
Ninakuleteeni tafakari ya Neno la Mungu, tukitafakari masomo Dominika ya II ya Kwaresima.
Mama Kanisa ametuwekea Neno la Mungu linalotutaka kuimarisha imani yetu kwa Mungu
kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo.
Mpendwa mwana
wa Mungu katika tafakari yetu Dominika ya kwanza ya kwaresima tuliona majaribu dhidi
ya Bwana wetu Yesu Kristu na sasa Dominika hii tumewekewa majaribu dhidi ya Ibrahimu.
Ibrahimu ni Baba mnyenyekevu ambaye kwanza aliambiwa na Mungu aende nchi asiyoijua
na alitii wito huo wa Mungu bila kuangalia usalama wake bali tegemeo katika Mungu
anayemwita. Baadaye katika uzee wake akiwa amempata mtoto, mwanae wa pekee Isaka,
ghafla anaombwa na Mungu akamtoe sadaka ya kuteketezwa na anaitika bila kusita.
Ibrahimu
anakubali ombi la Mungu na anaanza safari kuelekea mlima wa kafara! Mara anapofikia
wakati wa shughuli yenyewe malaika wa Bwana anamwambia usitende jambo hilo, tayari
ninajua unamcha mwenyezi Mungu. Mara kondoo anaonekana kwa ajili ya kafara badala
ya mtoto Isaka! Kwa tendo la imani hii kuu, Mungu anamwahidia Ibrahimu uzao kama nyota
za angani, mchanga wa pwani na baraka tele zisizo na mwisho. Kwa sababu ya imani kuu
ya Ibrahimu Kanisa humwita Baba wa Imani.
Mpendwa mwanatafakari, kwangu mimi
yatosha tu kufurahia matunda ya imani ya Ibrahimu! Kumbe imani inazaa na kujenga upya
utajiri usioisha, kizazi kisichoisha na baraka zisizo na mwisho. Basi tufanye nini?
Ni kusadiki na kujiimarisha katika kutekeleza mpango wa Mungu daima tulioupokea kwa
njia ya ubatizo na hasa wakati huu wa kwaresima. Wote twafahamu kuwa katika kipindi
hipi wapo wakatekumeni wanaojiandaa kwa ubatizo, hawa wanaitwa na Mungu kuacha yote
ya kipagani, chuki, rushwa, ulevi na mambo kama hayo na wanatakiwa kujikabidhi mikononi
mwa yule anayewaita pasipo kuwa mashaka. Wanaalikwa kuiga mfano wa Ibrahimu Baba wa
imani anayejitoa bila kuangalia usalama wake, aliye tayari kutoa sadaka ya mwanae
bila woga bali akiwa na tumaini yakwamba Mungu atatenda yote.
Katika somo la
pili Mtume Paulo anawaandikia Warumi sura ya 8 akiwaimarisha katika imani yao. Anajua
wakati fulani wanapata mateso kwa sababu ya imani hiyo, lakini anawaambia cha msingi
ni kujenga imani kama ya Ibrahimu ili Mungu akae pamoja nao. Na hivi Mungu akiwa upande
wao hakuna nguvu nyingine ya kuweza kuwashinda. Kristu mzaliwa wa kwanza amekuja kwa
ajili ya wokovu, amekufa na kufufuka taji ya ushindi dhidi ya dhambi. Kristu ametuletea
upendo usiokwisha hata kama tunamkosea, yeye hubaki akitupenda bila kurudi nyuma.
Mpendwa
msikilizaji, somo la Injili toka Mwinjili Marko sura 9 linaweka mbele yetu Yesu akiwa
mlimani katika faragha pamoja na Yakobo, Petro na Yohane. Jambo la Bwana kuwa mlimani
ni alama ya uwepo na utukufu wa Mungu. Daima Mungu anaongea na watu wake akiwa mlimani.
Katika mantiki ya kuwa mlimani katika Innjili tunakumbuka mara moja, jinsi Mungu alivyomkabidhi
Musa amri akiwa mlimani Sinai (Kut. 24:15). Ni pale mlimani Mungu anajionesha kwa
Eliya (1Wafalme 19:8). Jambo la pili ni lile la kugeuka sura na mavazi meupe kumetameta.
Weupe ni alama ya Mungu, alama ya furaha na dhihirisho la Kristu aliye Mtakatifu na
Mungu.
Alama ya tatu ni ile ya Musa na Eliya wanapozungumza na Yesu. Hawa ni
viwakilishi vya Agano la kale yaani sheria na Manabii na hivi kazi yao ni kumweka
mbele yetu Bwana na kisha watatoweka. Kutoweka kwao kuna maana yakuwa sasa Agano la
Kale limekwisha na linaanza agano Jipya. Mpendwa msikilizaji, kazi yetu waamini ni
kutangaza ukuu wa Mungu na baada ya hapo kupisha njia ili Mungu daima akue wakati
huo tukipungua.
Mtakatifu Petro anamwomba Bwana wakajenge vibanda vitatu kimoja
cha Bwana, vingine vya Musa na Eliya. Hii ni alama ya sikukuu, kama tujuavyo sikukuu
ya vibanda kwa Waisraeli ilikuwa ya maana sana na hasa ilipowakumbusha vibanda vyao
huko jangwani. Mtume Petro hajaelewa nini hasa mpango wa Bwana, yeye anaona ni sherehe
tu, haoni mateso yaliyo mbele ya Bwana.
Wakiwa bado mlimani linatoka wingu
na kuwafunika na sauti inatoka juu ikisema “Huyu ni mwanangu mpendwa msikieni yeye!
Wingu katika agano la kale liliwaongoza wana wa Israeli kupita jangwani, baharini
kumbe uwepo wa wingu ni uwepo wa Mungu na hivi sauti inapotoka juu katika wingu si
kitu kingine bali Kristu anadhihirishwa kuwa mmoja na Baba, yeye ni wa juu na wala
si wa dunia hii.
Mara hawa Mitume walipotazama hawakuona mtu bali Yesu peke
yake ndiyo kusema wale akina Musa na Eliya hawapo, kama nilivyokwishasema kazi yao
imekwisha na anabaki Bwana mkuu wa Agano Jipya na la milele. Baada ya matukio hayo
yote Bwana pamoja na Mitume wanaanza kushuka chini mlimani na wananaposhuka anawakataza
wasimweleze mtu mpaka Mwana wa mtu atakapofufuka toka wafu.
Hii ni siri ya
kimasiha, hataki wasimulie mambo yake mpaka wawe wameelewa vizuri mpango wake wa wokovu
kwa njia ya msalaba. Daima Mwinjili Marko atajitahidi kumficha Masiha mpaka atakapowekwa
wazi katika sura ya 15 ya Injili yake. Tunatafakari maneno ya akida mpagani anayesema
baada ya Yesu kukata roho “hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu” Mk. 15:39. Wito kwako
wewe unayenisikiliza ni kujifunza vizuri na kumtambua Bwana ni nani, ili utume wako
ulale katika uhakika wa Bwana anayekualika daima kumtumikia kwa uchaji. Kumbuka bila
toba ya ndani si rahisi kupokea mafundisho ya imani, Neno la Mungu na yote mema yatokayo
kwa Mungu.
Mpendwa ninakuageni kwa furaha nikitumaini utaendelea kuongozwa
na Neno la Mungu daima. Utaendelea kuongozwa na Mwana wa Mungu kwa maana ndivyo ulivyoamriwa
katika injili “ Huyu ndiye Mwanangu mpendwa msikieni yeye”. Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.