2015-02-25 10:10:30

Msiendekeze "vidumu"!


Amani, utulivu, maendeleo na maridhiano ndani ya Jamii yanategemea kwa kiasi kikubwa ubora wa maisha ya ndoa na familia. Hiki ndicho kiini cha ujumbe wa Askofu Maurice Piat wa Jimbo Katoliki la Port-Louis, nchini Mauritius katika barua yake ya kichungaji kwa ajili ya Maadhimisho ya Kipindi cha Kwaresima inayoongozwa na kauli mbiu "Jamani familia, Mungu anawapenda".

Licha ya mambo kadhaa yanayohatarisha mshikamano na mfungamano wa maisha ya ndoa na familia, bado Wakristo na watu wote wenye mapenzi mema hawana budi kujifunga kibwebwe ili kusimama kidete kulinda, kutetea na kutangaza Injili ya Familia kwa njia ya ushuhuda wa maisha yenye mvuto na mashiko; maisha yanayojikita katika tunu msingi za maisha ya ndoa na familia!

Wanafamilia watambue changamoto zilizoko mbele yao ili kweli waweze kuzikabili kwa imani, matumaini na mapendo, kwa kumegeana na kuonjesha uzuri wa maisha ya kuishi na kushibana kwa pamoja kama wanandoa. Pale wanandoa wanapokosa muda na nafasi ya kuonana, kusaidiana na kufarijiana, hapo kasoro na cheche za majanga ya maisha ya ndoa na familia zinaanza kuojionesha. Wanandoa wawe na ujasiri wa kushirikishana magumu na matumaini ya maisha, katika ukweli na uwazi, ili kuponya madonda na majeraha yanayoweza kuwa yamejitokeza katika hija ya maisha yao.

Askofu Maurice Piat anasema kinzani kati ya Baba na Mama ndani ya familia na hatimaye kutalakiana, ni mambo ambayo yanaacha kurasa chungu katika maisha, malezi na makuzi ya watoto. Pale baba wa familia anapoamua kuchukua "kidumu" au kung'ang'ania kwenye "nyumba dogo" hapo majanga yanaanza kuingia katika maisha ya kifamilia na kwamba, mwelekeo kama huu unaweza kumfanya mama pia kutaka kumkomoa mwenzi wake wa ndoa kwa "kwenda chocho", mambo ambayo yanahatarisha, amani, ustawi na maendeleo ya maisha ya ndoa na familia.

Inasikitisha kuona kwamba, kuna idadi kubwa ya familia tenge, zinazosimamiwa na kuendeshwa na mzazi mmoja na mara nyingi ni mwanamke ambaye anajikuta akilazimika kuwahudumia watoto wake, hata kama ni kwa shida kubwa. Ni wanawake wanaojitaabisha kuwaelimisha watoto wao na kuhakikisha kwamba, wanapata maisha mazuri kama watoto wengine, lakini wakati mwingine, wanashindwa na kuelemewa na mzigo wa malezi na makuzi ya watoto; matokeo yake watoto wanajisikia kutokuwa na ulinzi na usalama, hivyo wanaweza kujikuta wanaishi katika mazingira magumu na hatarishi.

Askofu Maurice Piat anasema kwamba, kuna mambo ambayo yanafumbatwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia; mambo ambayo yanaathari kubwa kwa maisha na utume wa ndoa na familia, ikiwa kama hayataweza kuangaliwa kwa umakini mkubwa. Si familia zote zinazoweza kuridhisha matakwa na matamanio ya watoto wao; jambo hili lisipoeleweka, kuna hatari ya amani na mfungamano wa maisha ya kifamilia kutoweka.

Wazazi wajitahidi kujenga utamaduni wa kuwa karibu zaidi na watoto wao hasa wakati huu wa kipindi cha mpito kuelekea utandawazi usiojali wala kuguswa na masuala ya imani, maadili na utu wema. Wanandoa wajifunze kujikita katika ukweli na uwazi kwa njia ya majadiliano, ili kutambua hali halisi ya maisha.

Askofu Maurice Piat katika ujumbe wake wa Kwaresima anasema kwamba, Mapadre, Watawa na Waamini walei wanayodhamana ya kulinda, kutetea na kudumisha misingi bora ya maisha ya ndoa na familia, ndiyo maana Kanisa halina budi kuwa karibu na familia zinazoogelea katika shida na mahangaiko makubwa, kwa kuzionjesha upendo, mshikamano na matumaini. Utume huu unaweza kutekelezwa vyema zaidi kwa njia ya Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo.

Waamini wafahamishwe maana na umuhimu wa mafundisho tanzu ya Kanisa kuhusu ndoa na familia, ili wawezwe kuyamwilisha katika uhalisia wa maisha yao, tayari kuwatangazia Watu wa Mataifa, Injili ya Familia, vinginevyo watu wanaweza kuwa na ufahamu hasi kuhusu Kanisa, kiasi cha kuwaachia madonda ya kudumu katika hija ya maisha yao ya kila siku.

Kanisa halina budi kuhakikisha kwamba, linawatangazia Watu wa Mataifa, Habari Njema ya Wokovu, tayari kutoka ili kuwaendea wale wote wenye kiu na njaa ya kutaka kusikiliza Injili ya Kristo, tayari kukumbatia wokovu unaoletwa na Yesu Kristo. Hawa ni watu wanaopaswa kusikilizwa na kusaidiwa katika ukweli na uwazi; katika imani, mapendo na matumaini, ili waweze kukutana na Yesu Kristo mchungaji mwema, mwingi wa huruma na mapendo; aliyekuja si kwa ajili ya kuwahukumu watu, bali kutoa maisha yake, ili yaweze kuwa ni fidia ya wengi.

Askofu Maurice Piat katika barua yake ya kichungaji wakati huu wa Kwaresima, anawaalika viongozi wa Serikali kutoa kipaumbele kinachostahili katika sera na mikakati yao ya maendeleo, kwa kutambua kwamba, familia ni rasilimali muhimu sana katika mchakato wa kukoleza na kukuza uchumi na maendeleo ya kijamii. Wananchi waelimishwe umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha, maadili na utu wema; wafundwe umuhimu wa kujisadaka kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi; waoneshe upendo na ukarimu kwa jirani, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii na kwamba, familia ni shule ya utakatifu, haki, amani na maridhiano ndani ya jamii.

Askofu Maurice Piat anahitimisha ujumbe wake wa Kwaresima kwa kukumbusha kwamba, amani, utulivu na haki jamii ni mambo yanayotegemea kwa kiasi kikubwa ubora wa maisha ya kifamilia. Ni wajibu wa Serikali na wadau mbali mbali kuweka mikakari na sera makini kwa ajili ya kuenzi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Mama Kanisa kwa upande wake, ataendelea kuchangia katika mchakato wa ustawi na maendeleo familia kwa kushirikiana na kujadiliana na wadau mbali mbali, ili kweli familia iweze kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya jamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.