Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia
Salamu za Pongezi Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (T.E.C) na Askofu wa
Jimbo Katoliki la Iringa, Mhashamu Baba Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, kufuatia uteuzi
uliofanywa na Baba Mtakatifu Francisko, wa Monsinyo Liberatus Sangu wa Jimbo Katoliki
Sumbawanga kuwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki la Shinyanga.
Askofu Mteule Liberatus
Sangu aliyekuwa Afisa mwandamizi katika Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu mjini
Vatican, anatarajiwa kuwekwa wakfu na kusimikwa rasmi kuwa Askofu wa Jimbo la Shinyanga
tarehe 12 Aprili, 2015. “Nachukua fursa hii kukupongeza kwa dhati kabisa kwa mafanikio
ambayo Kanisa Katoliki hapa nchini limeendelea kuyapata, kufuatia kuteuliwa kwa Monsinyo
Liberatus Sangu kuwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki la Shinyanga.
“Hii inadhihirisha
wazi kutambuliwa kwa mchango mkubwa wa Padre Sangu katika kuwatumikia kikamilifu Kondoo
wa Bwana hususan kupitia Idara nyeti ya Uenezaji wa Injili kwa Mataifa aliyokuwa akiitumikia
akiwa mjini Vatican ambako ndiyo Makao Makuu ya Kanisa Katoliki Duniani”, amesema
Rais Kikwete katika pongezi zake.
Rais Kikwete amemuomba Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa
kumfikishia Salamu zake za Pongezi kwa Askofu Mteule Liberatus Sangu kwa kuteuliwa
kwake, na amemtakia mafanikio zaidi katika Wadhifa wake Mpya wa Askofu katika kulitumikia
Kanisa Katoliki na Wamini wa Kanisa hilo kwa ujumla hapa nchini, hususan katika Jimbo
Katoliki la Shinyanga alikopangiwa kwenda kufanya kazi.