Waamini wanahamasishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, kweli wanakuwa ni mashahidi
wa Kristo na Kanisa lake, kwa kuendelea kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya kanuni
msingi za maisha ya Kiinjili, ili kuonesha umuhimu wa imani inayomwilishwa katika
maisha na mikakati ya watu na wala si jambo la kuwekwa pembezoni mwa maisha!
Hii
ni changamoto ambayo imetolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Benjamin Ndiaye, wakati
wa Ibada ya kumsimika kuwa Askofu mkuu mpya baada ya Kardinali Theodore Adrein Sarr,
kung'atuka kutoka madarakani hivi karibuni. Ibada hii imehudhuriwa na umati mkubwa
wa Familia ya Mungu kutoka Senegal. Askofu mkuu Ndiaye, amewataka waamini kuimarisha
imani yao kwa Kristo na Kanisa lake pamoja na kuendelea kuwasaidia na kuwahudumia
maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Waamini watambue mafundisho tanzu
ya Kanisa kama yanavyofafanuliwa katika: Biblia, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki
na Mafundisho Jamii ya Kanisa.
Waamini wajenge na kuimarisha umoja na mshikamano
hata katika tofauti zao za karama na vipaji; waimarishe ukarimu kwa wageni na maskini;
mambo msingi ambayo, Maaskofu Katoliki Senegal, walikumbushwa na Baba Mtakatifu Francisko
wakati wa hija yao ya kitume inayofanyika walau kila baada ya miaka mitano hapa mjini
Vatican. Familia ya Mungu Jimbo kuu la Dakar, ishikamane katika umoja na udugu; katika
huduma na ibada, ili Mwenyezi Mungu aweze kupewa sifa na utukufu na mwanadamu kupata
ustawi na maendeleo ya kiroho na kimwili.
Kwa upande wake, Askofu mkuu Luis
Mariano Montemoyor, Balozi wa Vatican nchini Senegal amewataka waamini kuendeleza
na kudumisha majadiliano katika ukweli na uwazi na waamini wa dini ya Kiislam pamoja
na taasisi mbali mbali nchini humo, ili kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa;
kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; kusimama kidete kwa ajili ya kutafuta
na kudumisha mafao ya wengi.
Wakristo na Waislam nchini Senegal wanapaswa
kuheshimiana na kushirikiana licha ya changamoto za utengano na kinzani zinazoendelea
kuoneshwa sehemu mbali mbali za dunia.
Naye Kardinali Thèodore Adrian Sarr,
Askofu mkuu mstaafu wa Jimbo kuu la Dakar, Senegal mara baada ya maadhimisho ya Ibada
ya Misa Takatifu, ameishukuru Familia ya Mungu nchini Senegal kwa ushirikiano waliomwonesha
wakati alipokuwa kiongozi mkuu wa Jimbo kuu la Dakar, anawataka sasa kuendelea kujielekeza
katika kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na maridhiano ndani ya jamii, kwa
kujikita katika majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kuimarisha umoja na mshikamano
wa kitaifa kwa ajili ya mafao na maendeleo ya wengi.
Na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.