2015-02-24 10:16:58

Waonjesheni Injili ya Furaha!


Kardinali Andrè Vingt-Trois, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Paris, Ufaransa katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa mwaka 2015 anawahimiza waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanawashirikisha jirani zao ile furaha inayobubujika kutoka katika imani kwa Kristo na Kanisa lake; kwa kuwamegea na kuwaonjesha maskini matendo ya huruma na mapendo pamoja na kuwashirikisha vijana matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi.

Kuwashirikisha wengine ile furaha ya Injili inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake kuna maanisha ya kuwatangazia Watu wa Mataifa kuhusu: Yesu Kristo aliyezaliwa, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Hii ndiyo changamoto kubwa ambayo Baba Mtakatifu Francisko anaibainisha katika Waraka wake wa kichungaji Furaha ya Injili, "Evangelii gaudium".

Hapa waamini wanachangamotishwa kusimama kidete na kamwe wasikubali wajanja wachache kuwapoka ari na nguvu ya kimissionari, bali wahakikishe kwamba, kila wakati wanaendelea kujipyaisha, ili kuwafikia watu wengi zaidi, ili kuwaonjesha Injili ya Furaha na Matumaini; kwa njia ya ushuhuda wa maisha yenye mashiko na mvuto!

Kardinali Andrè Vingt-Trous anasema vijana ni jeuri na matumaini ya Kanisa, kwani wanaweza kutangaza, kushuhudia na kuwashirikisha wengine tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kijamii. Ndiyo maana kuna haja kwa familia na shule kushirikiana kwa dhati kabisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya vijana wa kizazi kipya, kila upande ukitekeleza dhamana na wajibu wake barabara.

Vijana warithishwe tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili, zitakazowasaidia kuwajibika barabara kwa maneno na matendo yao. Vijana wasigeuzwe kuwa ni madodoki ya kupokea kila takataka inayotolewa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

Vijana wajengewe utamaduni wa kujisadaka na kutoa huduma kwa ajili ya jirani zao; wawe ni wajenzi badala ya kugeuzwa kuwa ni walaji wa kupindukia. Kwa Wakristo, vijana washirikishwe tangu mwanzo cheche za imani, matumaini na mapendo., kamwe wasikubali imani yao itekwe nyara na wajanja wachache kwa ajili ya mafao yao binafsi.

Kardinali Vingt-Trois, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Paris, Ufaransa anahitimisha ujumbe wake wa Kwaresima kwa kuyaelekeza macho yake kwenye maadhimisho ya mkutano mkuu wa kimataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi unaotarajiwa kufanyika nchini Ufaransa, Mwezi Desemba 2015. Kwa Familia ya Mungu nchini Ufaransa, huu ni wakati muafaka wa kufanya upembuzi yakinifu kuhusu tabia na mtindo wao wa maisha, ili kuhakikisha kwamba, wanakuwa na matumizi bora ya rasilimali za dunia, hali ambayo haina budi kujikita katika mfumo wa maisha.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.