Wanawake Colombia watunukiwa tuzo ya amani kwa mwaka 2015
Chama cha Kimataifa cha amani, Pax Christi, kwa mwaka 2015 kimeamua kuwatunukia tuzo
la amani Mtandao wa wanawake kutoka nchini Colombia kwa kutambua mchango wao katika
tafakari na matendo ambayo yameiwezesha Colombia kuanza tena mchakato wa amani na
utulivu baada ya kuogelea kwa muda mrefu katika vita ya wenyewe kwa wenyewe, iliyosababisha
maafa makubwa kwa watu.
Pax Christi inapenda kuwahamasisha wanawake kuchangia
katika ustawi, maendeleo, amani na utulivu katika familia, jamii na nchi zao, kwani
hawa ni watu wenye uwezo mkubwa na wanaweza kufanikisha azma hii, ikiwa kama watawezeshwa
kikamilifu. Wanawake wamekuwa ni walimu wazuri wa maadili na utu wema ndani ya jamii,
mambo ambayo yameliwezesha taifa la Colombia kuanza mchakato wa msamaha na upatanisho
kwa ajili ya mafao ya wengi. Watu wakijikita katika maadili, amani na utulivu vinaweza
kupatikana.
Mtandao wa wanawake kutoka Colombia ulianzishwa Mwezi Oktoba 2011
ili kuwaunganisha wanawake kutoka katika medani mbali mbali za maisha na dini, ili
kwa pamoja wasaidie kuifunda jamii kujikita katika maadili na utu wema, ili amani
ya kweli iweze kupatikana nchini Colombia. Pax Christi linasema kwamba, hapa tofauti
za kidini, kisiasa na kijamii umesaidia kuwaunganisha watu kwa ajili ya mafao ya wengi
na leo hii amani imepatikana. Kanuni maadili ni nguzo msingi katika kukoleza mabadiliko
ndani ya jamii.
Pax Christi inawapongeza wanawake kwa kujifunga kibwebwe haki
kuhakikisha kwamba, amani na upatanisho vinashika kasi tena nchini Colombia. Yote
haya yamewezekana kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maadili, utu na heshima ya binadamu
pamoja na mafao ya wengi. Pax Christi inawapongeza wanawake kwa mchango wao makini
katika kukuza na kudumisha amani na maridhiano ndani ya jamii.
Mtandao wa
wanawake kutoka Colombia utakabidhiwa tuzo lao hapo tarehe 16 Mei 2015 huko mjini
Bethlehemu wakati Pax Christi itakapokuwa inaadhimisha kumbu kumbu ya miaka 70 tangu
kuanzishwa kwake. Tuzo ya amani ilianza kutolewa na Pax Christi kunako mwaka 1988
ili kutambua juhudi za watu mbali mbali katika kukuza na kudumisha amani duniani.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.