Mfuateni Kristo katika uhalisia wa maisha yenu, ndiyo kauli mbiu iliyoongoza maadhimisho
ya Jubilee ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa Parokia ya Bikira Maria, Kitgum, Jimbo
kuu la Gulu, Uganda, iliyofanyika hivi karibuni na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa
Familia ya Mungu nchini Uganda. Hizi ni juhudi za Wamissionari wa Comboni zilizoanzishwa
kunako mwaka 1911, kwa kupandikiza mbegu ya Ukristo, leo hii matunda yanaonekana,
lakini hayana budi kuimarishwa na kutolewa ushuhuda wa maisha.
Katika mahubiri
yake, Askofu mkuu Michael Augustin Blume, ameitaka Familia ya Mungu nchini Uganda
kumkumbatia Kristo katika maisha na vipaumbele vyao, kwa njia ya ushuhuda wa maisha
ya Kikristo, ili kuliwezesha Kanisa kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza
katika medani mbali mbali za maisha. Changamoto hizi ni zile zinazojikita katika utandawazi
na maendeleo ya sayansi na teknolojia bila kusahau ukanamungu.
Kanisa nchini
Uganda halina budi kuwekeza zaidi katika sekta ya elimu, ili kusaidia mchakato wa
kuwafunda vijana tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni. Kuna haja ya
kuachana na mila pamoja na desturi zilizopitwa na wakati na zile ambazo kimsingi zinasigana
na tunu msingi za Kiinjili, kiasi cha kuwapotosha watu.
Yesu Kristo ndiye
Mkombozi wao, changamoto na mwaliko kwa vijana kukumbatia maisha ya Kisakramenti kwa
kuthubutu kupokea Sakramenti ya Ndoa Takatifu, ili kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Familia, kwa njia ya ushuhuda wa tunu msingi
za maisha ya ndoa na familia. Vijana wahakikishe kwamba, wanajitafutia ajira ili kujipatia
mahitaji yao msingi.
Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda ndiye aliyekuwa
mgeni rasmi katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa Parokia
ya Bikira Maria, Kitgum, Jimbo kuu la Gulu. Rais Museven amechangia millioni 30 za
Uganda, ili zisaidie mchakato wa maendeleo kwa Familia ya Mungu Parokiani hapo. Ameliomba
Kanisa nchini Uganda kushirikiana na Serikali katika mapambano dhidi ya baa la umaskini
kwa kuwajengea waamini wake uwezo wa kujitegemea na kujiendeleza. Viongozi wa Kanisa
wawe ni mfano bora katika mapambano dhidi ya umaskini. Sherehe hizi zimehudhuriwa
na umati mkubwa kutoka ndani na nje ya Uganda, kwani kwa hakika miaka 100 si haba!