Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milano, Italia, anawaalika waamini
na watu wote wenye mapenzi mema katika kipindi hiki cha Kwaresima kutubu na kumwongokea
Mwenyezi Mungu kwa kuiamini Injili pamoja na kuhakikisha kwamba, kila siku wanajitahidi
kuboresha maisha na utu wao wa ndani kadiri ya mapenzi ya Mungu.
Toba na wongofu
wa ndani ni mwaliko wa kutubu dhambi sanjari na kurekebisha mapungufu ya kibinadamu,
kwa njia ya ushuhuda makini kutoka kwa Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka
katika wafu. Kwaresima ni kipindi kilichokubaliwa mbele ya Mwenyezi Mungu, mwaliko
kwa waamini kuzama katika maisha ya sala, toba, kufunga, kutafakari pamoja na kumwilisha
Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha, kwani hii ndiyo chemchemi ya mapendo kutoka
kwa Mwenyezi Mungu.
Kwaresima ni kipindi ambacho Mama Kanisa anawaalika Wakristo
kupyaisha tena utambulisho wao wa Kikristo kwa njia ya ushuhuda wenye mvuto na mashiko
kwa kukimbilia huruma na upendo wa Mungu, unaomwilishwa katika uhalisia wa maisha
yao ya kila siku. Mapambano kati ya Yesu na Shetani kule Jangwani kwa siku arobaini,
iwe ni changamoto kwa Wakristo kutambua kwamba, wasipokuwa makini, Shetani anaweza
kutumia baa la njaa kuwavuruga. Kwaresima, kiwe ni kipindi cha mshikamano na watu
wanaoteseka kwa baa la njaa duniani.
Waamini wawe macho na kishawishi cha
kupenda mno madaraka, kiasi hata cha kumezwa na malimwengu, bali daima wajitahidi
kumwangalia Yesu Kristo aliyetundikwa pale Msalabani, chemchemi ya upendo, amani na
uhuru wa kweli. Kristo ndiye anayepaswa kuheshimiwa, kuabudiwa na kutukuzwa kwani
kwa njia ya Fumbo la Msalaba ameukomboa ulimwengu.
Mapambano ya maisha ya kiroho
katika kipindi hiki cha Kwaresima yanajikita katika sala na kufunga ili kuratibu na
kurekebisha vilema vinavyomwandama mwamini katika hija ya maisha yake hapa duniani.
Waamini washinde kishawishi cha uvivu pale wanapoweza washiriki hata Ibada ya Misa
Takatifu kati kati ya juma, bila kusahau umuhimu wa Njia ya Msalaba. Kwaresima ni
kipindi cha kukikimbilia upendo na huruma ya Mungu katika maisha kwa kujipatanisha
na Mungu pamoja na jirani kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.