2015-02-24 10:05:20

SECAM kushirikiana zaidi na Umoja wa Afrika


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM limemteua Bwana Berhanu Tamene Woldeyohannes, Mratibu wa Tume ya haki na amani ya SECAM kuwa mwakilishi wa SECAM kwenye Umoja wa Afrika, wenye Makao yake makuu mjini Addis Ababa, Ethiopia. Amekabidhiwa wajibu wa kuharakisha mchakato wa mahusiano kati ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM pamoja na Umoja wa Afrika.

Lengo ni kuliwezesha Kanisa kushiriki kikamilifu katika mchakato unaopania kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Bara la Afrika; kwa kujikita katika uongozi na utawala bora unaosimamia maendeleo endelevu ya Familia ya Mungu Barani Afrika. SECAM inapenda kuchangia katika mchakato wa misingi ya usawa, haki, amani na upatanisho.

Bwana Woldeyohannes atakuwa na dhamana ya kuratibu mahusiano kati ya SECAM na Taasisi mbali mbali zinazoongozwa na kusimamiwa na Umoja wa Afrika, ili kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu Barani Afrika mintarafu mwanga wa Waraka wa kichungaji wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, Dhamana ya Afrika, "Africae Munus".

Bwana Woldeyohannes kwa taaluma ni mwanasheria kutoka Chuo Kikuu cha Addis Ababa Ethiopia ambako alijipatia shahada ya uzamili na baadaye akajiendeleza nchini Harare na huko akajipatia shahada katika Falsafa. Ni mtaalam aliyebobea katika masuala ya ulinzi, usalama na amani. Amewahi pia kufundisha maadili nchini Ethiopia pamoja na kuendeleza shughuli za kichungaji za Kanisa Katoliki miongoni mwa vijana, nchini Ethiopia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.