2015-02-24 09:58:57

Mtakatifu Gregori wa Narek, Mwalimu wa Kanisa


Baba Mtakatifu Francisko, hivi karibuni baada ya kufanya mazungumzo na Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu, ameridhia uamuzi uliofanywa na wajumbe wa Baraza hili la kipapa la kumtangaza Mtakatifu Gregori wa Narek, kuwa Mwalimu wa Kanisa.

Mtakatifu huyu alikuwa ni Mtawa, aliyezaliwa huko Andzevatsik, wakati huo ukijulikana kama Armenia ambayo ndiyo nchi ya Uturuki kwa sasa. Ni mtawa na mwanataalimungu mahiri, aliyejipambanua kwa maandishi na mtunga mashahiri maafuru; alikuwa mwaminifu na mtiifu kwa Mapokeo ya Mama Kanisa, akaonesha bidii na heshima kubwa kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu. Inasadikiwa kwamba, Bikira Maria alimtokea Mtakatifu Gregori.

Kati ya kazi zake kuu ambazo wengi wanazikumbuka ni kuhusu "Hotuba ya Masifu kwa Bikira Maria" pamoja na Sala 80 ambazo zilipewa jina, "Kutoka katika undani wa moyo wangu, majadiliano na Mama wa Mungu". Sehemu hii ya sala inaonesha jinsi ambavyo Mtakatifu Gregori baada ya kukabiliwa na magumu pamoja na machungu ya maisha yaliyomkatisha tamaa, mwishoni alifanikiwa kuona upendo kutoka kwa Bikira Maria, akatambua msaada wake wa daima. Gregori wa Narek alifariki dunia kunako mwaka 1005.

Kanisa nchini Armenia kwa miaka mingi lilikuwa linamtambua kuwa ni Mwalimu wa Kanisa. Alitambulika na Mama Kanisa kutokana na utakatifu uliojikita katika mafundisho makuu ya imani kama anavyokumbukwa katika Orodha ya Watakatifu wa Kanisa, tarehe 27 Februari. Baba Mtakatifu Francisko wakati wowote kuanzia sasa anaweza kumtangaza rasmi kuwa ni Mwalimu wa Kanisa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.