2015-02-23 09:01:15

Sala, maskini na amani!


Chansellor Angela Merkel baada ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican, mwishoni mwa juma, alikwenda kutembelea Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao makuu yake mjini Roma na kupokelewa na viongozi wakuu wa Jumuiya hii ambayo imekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Chansellor Angela Merkel amezungumza kwa kina na mapana na viongozi hawa kuhusu mikakati ya amani na maridhiano kati ya watu wa mataifa; tatizo na changamoto kwa wahamiaji wanaoendelea kuwasili kwa wingi Barani Ulaya kupitia bahari ya Mediterrania ambako wengi wao wanazidi kupoteza maisha au kutumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu. Viongozi hawa wamegusia pia hali ya Bara la Ulaya na changamoto zake zinazogumisha mshikamano na mfungamano wa kijamii kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.
Kwa upande wake, Bwana Marco Impagliazzo, Rais wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, katika hotuba yake ya kumkaribisha Angela Merkel, amegusia mafanikio ya upatikanaji wa amani huko Msumbiji, Guatemala na Burundi. Wanampongeza kwa juhudi zinazofanywa na Serikali ya Ujerumani ii kusitisha vita na kuanza mchakato wa ujenzi wa amani nchini Ukraine, ili watu waanze tena kujikita katika maendeleo na ustawi wao baada ya vita. Juhudi za kujenga na kudumisha amani ni kati ya vipaumbele vya kwanza vinavyofanyiwa kazi na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio sehemu mbali mbali za dunia kwani wanatambua kwamba, vita na kinzani ni mama wa umaskini.
Jumuiya ya Mtakatifu Egidio inatambua na kuthamini juhudi za kidiplomasia katika kutatua migogoro na kinzani mbali mbali kwani juhudi hizi ni mwanga na matunda ya kitamaduni na kiutu yanayojikita katika imani na kwamba, matokeo yake ni amani ya kudumu. Jumuiya hii imekuwa ikijielekeza zaidi katika majadiliano ya kidini na kiekumene; kisiasa na kitamaduni kwamba, amani inachangia kwa kiasi kikubwa ustawi na maendeleo ya watu.
Dini mbali mbali duniani zina dhamana ya kuendeleza mchakato wa amani na maridhiano kati ya watu; kwa kukuza na kudumsiha tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu, ili kweli amani iweze kuzama katika maisha na vipaumbele vya watu, changamoto kubwa katika ulimwengu mamboleo. Wananchi wengi wa Bara la Ulaya wanaogopa kukutana na kuchangamana na watu kutoka katika Mabara mengine, Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, inawasaidia kuvuka mwono huu finyu.
Jumuiya hii inajikita katika mambo makuu matatu: sala, maskini na amani na inatekeleza dhamana na utume wake katika nchi 73 duniani. Inapania kumwilisha Injili ya Furaha, Amani, Ukarimu na Matumaini kwa wale waliokata tamaa pamoja na kukosa uhuru ambao kimsingi ni haki yao sanjari na kukumbatia mafao na furaha ya wengi.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.