2015-02-23 08:35:58

Mikakati ya maboresho ya elimu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana limechapisha muhtasari wa mbinu muhimu za kufundishia, ili kuhakikisha kuwa, wananchi wa Ghana wanapata elimu bora zaidi itakayowasaidia kupambana na mazingira, ili yaweze kuwa bora zaidi. Kanisa linapenda kuhakikisha kwamba, wanafunzi wanapohitimu masomo yao, wawe wamepikwa na kuiva barabara tayari kuchangia katika ustawi na maendeleo yao binafsi, familia, jamii na taifa katika ujumla wake.
Hii ni elimu inayomwandaa mwanafunzi kwa ajili ya uwajibikaji na maisha kwa siku za usoni. Muhtasari huu umezinduliwa hivi karibuni na Askofu Mathew Gyamfi, Mwenyekiti wa Tume ya Elimu, Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana, ambaye anakazia kwamba, kuna haja ya Serikali, Kanisa na wadau mbali mbali wa elimu kushirikiana kwa karibu zaidi, ili kuhakikisha kwamba, elimu inayotolewa inazingatia viwango, taaluma na kumhusisha mtu mzima, dhamana inayopaswa sasa kutekelezwa na wadau mbali mbali katika shule, taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu nchini Ghana.
Kanisa limeamua kuivalia njuga sekta ya elimu baada ya kuona kwamba, elimu nchini Ghana ilikuwa inachechemea kiasi cha kukatisha tamaa na kwamba, watu walianza kukata tamaa ya kuendelea na masomo, kwani elimu ilionekana kutokuwa na msaada mkubwa kwa wananchi wengi licha ya jitihada zilizokuwa zinafanywa na wadau mbali mbali.
Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana linapenda kujielekeza zaidi katika huduma ya elimu kwa wanawake ili kuweza kuwaletea ukombozi wa kweli, ili hatimaye, waweze kuchangia katika ustawi na maendeleo ya familia na jamii kwa ujumla wake. Maaskofu wanabainisha mambo msingi ambayo yanapaswa kutekelezwa na walimu kwa kukazia nidhamu, weledi, juhudi, bidii na maarifa yatakayowawezesha kurithisha elimu kwa vijana wa kizazi kipya pamoja na kuwajengea uwezo wa kupenda kusoma na kujiendeleza zaidi kwa kutambua kwamba, elimu ni mkombozi wa maisha ya mwanadamu.
Muhtasari huu anasema Askofu Mathew Gyamfi unapembua mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu nchini Ghana; mafanikio, matatizo, changamoto na jinsi ambavyo Kanisa limefanikiwa kufanya maboresho makubwa katika sekta ya elimu katika shule, taasisi na vyuo vinavyomilikiwa na Kanisa, kwa ajili ya mafao ya wengi. Haya ndiyo mang’amuzi ambayo Kanisa linapenda kuishirikisha Serikali, ili kukoleza mchakato wa mageuzi ya kina nchini Ghana, katika medani mbali mbali za maisha.
Kanisa Katoliki ni mdau mkubwa katika sekta ya elimu, utume ambao umefanywa kwa majitoleo makubwa tangu Wamissionari walipoingia Barani Afrika. Kanisa nchini Ghana linamiliki na kuendesha taasisi 4, 000 za elimu kuanzia elimu ya awali hadi chuo kikuu. Kanisa litaendelea kujielekeza katika maboresho ya sekta ya elimu ili kuwajengea vijana wa kizazi kipya matumaini ya maisha bora kwa njia ya elimu makini, kwa kushirikiana na wadau mbali mbali. Huu ni mradi mkubwa ambao Kanisa limeishirikisha Serikali ya Ghana, ili kushirikiana kwa pamoja katika ustawi, maendeleo na mafao ya wananchi wote wa Ghana.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.