2015-02-23 12:09:27

Kifo cha mwadilifu!


Familia ya Mungu nchini Tanzania, mwishoni mwa Juma, ilikusanyika kwa ajili ya kumsindikiza Marehemu Askofu mstaafu Magnus Mwalunyungu wa Jimbo Katoliki la Tunduru-Masasi aliyefariki dunia hivi karibuni katika usingizi wa amani. Ibada ya Misa Takatifu imeongozwa na Askofu mkuu Damian Dallu wa Jimbo kuu la Songea, katika Parokia Tosamanga, Jimbo Katoliki Iringa, aliyewataka waamini kutoogopa kukabiliana uso kwa uso na Fumbo la Kifo na badala yake wajiandae kikamilifu kwa ajili ya maisha ya uzima wa milele.

Katika mahubiri yake Askofu mkuu Dallu anasema kwamba, Marehemu Askofu Mwalunyungu ameishi kwa muda wa miaka 85 na kati ya hiyo, miaka 55 amelitumikia Kanisa kama Padre na miaka mingine 13 kama Askofu. Baada ya kung'atuka kutoka madarakani aliendelea kumtumikia Mungu kwa njia ya huduma Parokiani, akawa Paroko wa kwanza wa Parokia ya Kidamali, Jimbo Katoliki la Iringa, utume ambao umeufanya kwa miaka minne. Hiki ni kifo cha mwadilifu ambaye kwa sasa anapumzika kwa amani na starehe mbele ya Mwenyezi Mungu.

Ibada hii ya Misa Takatifu imehudhuriwa na Familia ya Mungu nchini Tanzania. Waziri mkuu wa Tanzania, Mizengo Pinda amemwakilisha Rais Jakaya Kikwete ambaye amewataka watanzania kufuata mafundisho yanayotolewa na viongozi wao wa dini, ili kujenga moyo wa uchaji wa Mungu, uadilifu na unyofu.







All the contents on this site are copyrighted ©.