2015-02-21 16:06:05

"Njaa ni mwanaharamu.."


Amani na utulivu kamwe havitaweza kupatikana katika uso wa dunia, ikiwa kama baa la njaa halitaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu na Jumuiya ya Kimataifa. Kuna kundi la watu wachache wanaokula na kusaza kiasi hata cha kutupa chakula na wakati huo huo kuna bahari ya watu wanaoteseka na kunyanyasika kutokana na baa la njaa na utapiamlo wa kutisha duniani. Hii ni changamoto inayotolewa na Baraza la Kipapa la haki na amani katika hati inayojulikana kama "Dunia na Chakula" iliyotiwa mkwaju na Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani. RealAudioMP3

Baraza la Kipapa la haki na amani linabainisha kwamba, kuna haja ya kufanya marekebisho makubwa katika mfumo mzima wa uzalishaji, ugavi, matumizi ya rasilimali pamoja na mtindo wa maisha. Kadiri ya Mafundisho Jamii ya Kanisa, chakula ni haki msingi ya binadamu, kwani ina mahusiano makubwa na maisha ya mwanadamu, kwani pasi na chakula, maisha ya mwanadamu yako hatarini, ndiyo maana Waswahili wanasema, eti "Njaa ni mwanaharamu..."

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kukazia matumizi bora ya rasilimali ya dunia kama kikolezo cha kupambana na baa la umaskini, linaloendelea kudhalilisha utu na heshima ya binadamu; hali ambayo kimsingi inahitaji usawa na haki, ili kweli baa la umaskini liweze kupewa kisogo.

Hati hii imegawanyika katika sehemu kuu tatu: Sehemu ya kwanza inasema hali inatisha. Baraza la Kipapa la haki na amani linafafanua kwa kina na mapana mambo yanayoendelea kuchangia uwepo wa baa la njaa licha ya uzalishaji mkubwa wa mazao ya chakula.

Sehemu ya pili ya Hati hii inazungumzia mchango wa Kanisa katika kufanikisha mchakato wa maboresho katika sekta ya kilimo, kwa kuangalia vifungu vya Maandiko Matakatifu pamoja na Mafundisho mbali mbali yaliyokwishawahi kutolewa na Mababa wa Kanisa kuhusiana na mada hii. Baraza la Kipapa la haki na amani linabaianisha kanuni msingi katika tafiti na sera zinazoweza kutumika katika kupambana na baa la njaa duniani. Sehemu ya tatu inazama zaidi katika kutoa majibu muafaka kwa changamoto zinazoikabili sekta ya kilimo kwa kujikita katika mwelekeo wa kitamaduni na sera ambazo, kama zikitumika kwa usahihi zinaweza kuwa ni "Mwarobaini" wa baa la njaa duniani.

Takwimu zilizotolewa na Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO zinaonesha kwamba, katika kipindi cha mwaka 2012 hadi mwaka 2014 kumekuwepo na zaidi ya watu millioni 805 waliokuwa wanakabiliwa na baa la njaa na utapiamlo wa kutisha, kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Hili ni janga la kimataifa na wala hapa hakuna utani kwani maisha ya watu wengi yako hatarini kutokana na baa la njaa.

Inasikitisha kuona kwamba, dunia inaweza kuzalisha chakula cha kutosha kulisha watu wote duniani, lakini kutokana na ubinafsi, uchoyo na utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya wengine kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko, leo hii bado kuna watu wanafariki dunia kwa kukosa chakula! Kumekuwepo na mahitaji ya chakula hasa kutoka katika Nchi zinazoendelea duniani, lakini bado hakuna majibu yanayotosheleza mahitaji haya.

Hapa kuna haja ya kuwa na mtazamo mpana zaidi wa kuchambua na kuangalia mambo, kwani kuna mambo mengi yanayoendelea kuchangia uwepo wa baa la njaa duniani. Kwa mfano: vita na kinzani za kijamii na kisiasa; ongezeko la bei ya mazao ya chakula; maafa asilia kama vile ukame na mafuriko; rushwa na ufisadi. Bado Jumuiya ya Kimataifa haija fanikiwa kutoa chakula cha kutosha kwa kila mwanadamu kutokana na kushindwa kufanya mageuzi katika miundo ambayo imechangia uwepo wa baa la njaa duniani.

Matumizi mabaya ya ardhi ni jambo ambalo linaendelea kusababisha ukosefu mkubwa a chakula duniani na hata wakati mwingine, ardhi ambayo inafaa kwa kilimo cha mazao ya chakula, imegeuzwa na sasa inatumika kwa ajili ya kuzalisha nishati uoto. Ukosefu wa mvua za kutosha na maji kwa ajili ya kilimo cha umwagaliaji ni mambo ambayo pia yanachangia uwepo wa baa la njaa mwaka hadi mwaka. Uchafuzi wa mazingira pamoja na athari za mabadiliko ya tabianchi bado ni kikwazo kikubwa katika uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.

Kumekuwepo na ukataji miti ovyo pamoja na mashirika ya biashara ya kimataifa kuendelea kuneemeka kwa kupewa maeneo makubwa ya ardhi kwa ajili ya kilimo cha kisasa, lakini wakulima wadogo wadogo, wakiondolewa kutoka katika maeneo ambayo walikuwa wanayatumia kwa ajili ya kuzalisha mazao ya chakula na biashara kwa ajili ya familia zao, huu ni ukoloni mamboleo.

Mtakatifu Yohane Paulo II, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI pamoja na Papa Francisko ni kati ya viongozi wa Kanisa ambao wamechangia kwa kiasi kikubwa katika kuwahamasisha walimwengu umuhimu wa kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo kama sehemu ya mapambano dhidi ya baa la njaa na utapiamlo wa kutisha; utandawazi unaojikita katika ubinafsi, uchu wa mali na faida kubwa. Baadhi ya wafanyabiashara wanaona mazao ya chakula kuwa kama bidhaa inayoweza kuwaingizia faida kubwa na kusahau kwamba, chakula ni haki msingi ya binadamu.

Baraza la Kipapa la haki na amani linabainisha kwamba, Mwenyezi Mungu baada ya kumuumba mwanadamu alimkabidhi ardhi ili aweze kuitumia na kuiendeleza. Kumbe, rasilimali ardhi ni kwa ajili ya mafao ya wengi; inayopaswa kutumiwa kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini, kwa kuzingatia kanuni ya auni, haki, utu na heshima ya binadamu.

Sehemu ya tatu ya Hati ya Baraza la Kipapa la haki na amani kuhusu Dunia na Chakula inabainisha sera na mikakati inayoweza kutumiwa na Jumuiya ya Kimataifa katika kuendeleza kilimo bora kinachozingatia na kuheshimu maisha ya mwanadamu, ili kupambana kufa na kupona na baa la njaa ambalo linaendelea kunyanyasa na kudhalilisha utu na heshima ya binadamu. Ekolojia na maendeleo ni mambo yanayopaswa kuwa na mlinganyo mzuri, ili kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu ya binadamu.

Baraza la Kipapa la haki na amani, linahamasisha uwekezaji bora katika sekta ya kilimo, ili kupunguza athari za ukosefu wa usalama wa chakula katika eneo husika sanjari na kuchangia ustawi na maendeleo ya watu. Haki msingi za binadamu zinapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza kwa kuhakikisha kwamba, maisha yanalindwa na kudumishwa; watu wanapata chakula bora na maji safi na salama; wanafundishwa mbinu za kilimo bora na cha kisasa linachoheshimu na kutunza mazingira.

Wananchi washirikishwe katika kupembua na kufanya maamuzi kuhusu hatima ya maisha yao; wapewe mikopo na taasisi za elimu zijengewe uwezo wa kufanya tafiti na matokeo yake kuwasilishwa kwa wahusika, ili yaweze kufanyiwa kazi. Hapa kuna haja ya kuachana na kasumba ya kufanya tafiti na baadaye kuzifungia kwenye makabati ofisini.

Njia za mawasiliano ya kibiashara hazina budi kuboreshwa; kudhibiti matumizi mabaya ya chakula na raslimali ya dunia; kuwafunda na kuwaelimisha wawekezaji katika sekta ya kilimo; kuwasaidia wafanyabiashara na wanasiasa kuweza kutekeleza dhamana na wajibu wao barabara.

Baraza la Kipapa la haki na amani linabainisha kwamba, Kanisa Katoliki linashiriki kikamilifu ili kuhakikisha kwamba, watu binafsi, taasisi na Jumuiya ya Kimataifa katika ujumla wake, zinajifunga kibwebwe ili kuweza kuwa na uhakika wa usalama wa chakula. Kanisa linatekeleza dhamana hii kwa kutumia Mashirika yake ya misaada kimataifa na kitaifa, Mabaraza ya Maaskofu Katoliki na miundo yake pamoja na kuendelea kuwekeza kwa waamini walei, ili wasaidie mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Kanisa pale linapoweza linatoa pia msaada na mikopo nafuu kwa ajili ya kukuza maendeleo ya watu.

Kwa njia ya majiundo makini ya kulinda na kutunza mazingira, kwa kuwekeza kikamilifu katika kilimo cha kisasa na endelevu; kwa kuwapatia wakulima mtaji na pembejeo za kisasa sanjari na kuzingatia haki zao msingi, Jumuiya ya Kimataifa inaweza kuwa na uhakika wa usalama wa chakula na maendeleo ya watu. Kanisa litaendelea kuwekeza katika huduma kwa maskini kama sehemu ya utekelezaji wa utume wake kwa maskini na kwa ajili ya maskini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.