2015-02-20 10:49:12

Yesu anahukumiwa kufa!


Ifuatayo ni tafakari ya Njia ya Msalaba, wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Kipindi cha Kwaresima, muda wa kusali, kutafakari, kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu. Chukua muda kidogo, ili uweze kuitafakari kwa ajili ya ustawi wa maisha yako ya kiroho! Ukitaka mshirikishe pia jirani yako kwa njia za mitandao ya kijamii, kwani kizuri, kinaliwa na wengi!
KITUO CHA KWANZA
YESU ANAHUKUMIWA AFE..
(Matayo 27:11 - 26)
Ee Bwana Yesu Kristo tunakuabudu na kukushukuru....
Pilato anamuhukumu Yesu bila kosa lo lote. Utawala, sera, siasa si msaada kwa Yesu mnyonge. Nasi pia kuna nyakati ambazo mahakama, serikali, familia, utawala au hata rafiki zetu wapendwa na wenzetu wa ndoa waweza kuwa si msaada kwetu. Tutajikuta tupo peke yetu tumetelekezwa na kukosa pa kuegemea. Dunia yote itaninyooshea vidole mimi peke yangu. Utaonja hali ya kuwa mpweke ukawa wewe na Mungu wako tu. Utajiuliza, hata mume wangu wa ndoa au hata mke wangu ananisaliti mbele ya ndugu zake ?
Wangapi wana uchungu moyoni na akilini kwa kubambikiziwa kesi za kusingiziwa mahakamani ? Wangapi tumebeba aibu na machungu ya kuuzwa hivi hivi kama Yusufu Misri na ndugu wa tumbo moja ? (Mwanzo 37:12 - 36). Wangapi tumetendewa vibaya kwa kutopewa nafasi ya kusikilizwa na wenzetu wa ndoa tunapotofautiana ndani ya familia ? Baba anarudi jioni na kufoka tu kama mbogo na kuhukumu kwa dogo nililofanya nyumbani. Huenda nimetoa tu fulana moja iliyochakaa ya baba kwa kijana wa shamba (shamba boy) na moja kwa moja baba anafoka na kusema mimi natembea na kijana huyo. Hadhi yangu yote ya kuwa mimi ni mke wake kwa miaka 15 na kumzalia watoto watatu wazuri inaporomoka kwa dakika moja.
Wangapi tumefukuzwa kazi kiholela makazini bila ya kufuata tararibu, sheria na miongozo ya kazi ? Kazini kumekuwa ni sehemu za kusikiliza majungu tu, au nani wa kwanza kaenda kwa bosi na si kuangalia ukweli wa tatizo. Sisi sote makazini tunajiona ni kama mbuzi wa kafara tu. Kazi zinagawiwa au vyeo vinapandishwa kwa kuangalia dini, ukabila, urafiki, undugu au hata maelekeo yanayoashiria mapenzi na ngono. Hakuna vigezo vya elimu au uzoefu.
Uongozi si dhamana tena kwa niaba ya wanyonge. Viongozi wetu ni kama Pilato. Ni viongozi wa kuangalia upepo au ushabiki wa siku husika kama ule wa Yanga na Simba. Uongozi unaangalia maslahi hewa ya kelele za watu wa wakati husika. Macho ya Pilato yanafumbwa kwa kutoona mbele. Ukweli kwake si kitu chenye mashiko. Anatetea urafiki wa muda na Kaisari. Uongozi hausimamii tena haki, ukweli, bali ni woga mtupu. Pilato na majeshi yake yote anashindwa kusimama kwa miguu yake.
Wapendwa Wagetsemani, siku ya leo katika kituo cha kwanza tusali na kuomba kwa ajili ya wale wanaotendewa ubaya huu wa kuhukuniwa bila kosa.
Tuombe :
Ee Bwana Yesu uliyehukumiwa bila kosa lo lote, wajalie viongozi wetu waweze kusimamia maamuzi yao kwa miguu yao wenyewe. Vijalie vyombo vinavyosimamia sheria na haki, hasa mahakimu na majaji ili waweze kuhukumu kesi mbali mbali kwa haki na ukweli. Jalia familia zetu ziwe na nafasi ya unyenyekevu wa mazungunzano pale panapotokea shida au tofauti ili ukweli uonekane na kufikiwa muafaka wa kindugu na Kikristu.
Kwaresima njema wapendwa,
Fr Benno Kikudo,
Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.