Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko, Jumanne tarehe 17 Februari 2015 majira ya jioni amekutana na kuzungumza
na ujumbe wa Kikosi cha Uokoaji cha Wanamaji kutoka Italia, waliokuwa wameambatana
na viongozi wa Serikali ya Italia.
Wanajeshi hao wamemshirikisha Baba Mtakatifu
Francisko ushuhuda, changamoto na matatizo wanayokabiliwa nayo wakati wa kutoa huduma
ya uokoaji kwa wahamiaji na wakimbizi wanaojikuta wako kwenye Bahari ya Mediterrania,
huku wakipambana na kifo! Ujumbe huu wa watu wanane, umesimulia ushuhuda unaogusa
undani mwa mwanadamu katika maisha yake, kwa kuona jinsi watu wanavyopambana na kifo
maji, jambo la kutisha na kutia huruma.
Baba Mtakatifu, baada ya kusikiliza
kwa makini, amewashukuru na kuwapongeza wanajeshi hao kwa niaba ya wenzao, wanaoendelea
kujisadaka kwa ajili ya kuwaokoa wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta hifadhi ya maisha
yao Barani Ulaya, kiasi hata cha kuthubutu kujisadaka katika tumbo la Bahari ya Mediterrania.