2015-02-18 12:24:42

Maadili na utu wema!


Patriaki Louis Sako wa Kanisa la Babilonia ya Walkadei, katika ujumbe wake kwa Kipindi cha Kwaresima anasema, huu ni muda muafaka uliokubalika mbele ya Mwenyezi Mungu wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa nchini Iraq. Kiwe ni kipindi cha kujisomea, kutafakari na hatimaye kumwilisha Neno la Mungu katika huduma makini kwa jirani, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Ni matumaini ya Patriaki Sako kwamba, wananchi wanaoishi huko Iraq na Mashariki ya Kati, maeneo ambayo kwa sasa yamegeuka kuwa ni uwanja wa vita wataweza kufungua ukurasa mpya wa maisha, kwa kuwa na amani na utulivu, huku utu na maisha ya binadamu yakiheshimiwa na kuthaminiwa kwani hii ni zawadi ambayo haina mbadala.

Wananchi wanaishi katika mazingira hatarishi kiasi kwamba, hawana uhakika wa usalama wa maisha yao. Familia nyingi zimesambaratika na kutawanyika sehemu mbali mbali, utadhani ni umande wa asubuhi na kwamba, kuna idadi kubwa ya wakimbizi na wahamiaji wasiokuwa na mahali pa kujisetiri.

Licha ya magumu haya yote, lakini Patriaki Sako anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kutokata tamaa, bali taratibu kuanza mchakato wa ujenzi wa mshikamano wa udugu na ushirikiano, kwa kuheshimiana ili kujenga misingi ya haki na amani; kipaumbele cha kwanza kiwe ni umoja, msamaha na uptanisho wa kitaifa; tayari kusimamia mafao ya wengi.

Kipindi cha Kwaresima, iwe ni fursa kwa Wakristo kujikita katika tunu msingi za maisha ya kiroho na kimaadili kwa kukazia: ukweli, uwazi na uaminifu; waamini wajitahidi kujenga upendo na mshikamano na wote wanaoteseka na kupondeka moyo kutokana na hali ngumu ya maisha. Wakristo watambue kwamba, wanayo dhamana na utume huko Mashariki ya Kati na kwamba, uwepo wao ni ushuhuda wa matumaini kwa wale waliokata tamaa; imani kwa wale waliokengeuka; mapendo kwa wale wasiothamini wala kuwajali ndugu zao kutokana na tofauti za kiimani. Hakuna haja ya kutaka kufa wala kupondeka moyo, bali kuendelea kuwa na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi, kadiri ya mpango wa Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.