Ibada ya Jumatano ya Majivu, inawaingiza Wakristo katika Kipindi cha Kwaresima, hija
ya siku arobaini inayowachangamotisha waamini kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu
na jirani. Ni wakati uliokubalika kwa waamini kumfungulia Mwenyezi Mungu na jirani
zao, mioyo ya upendo na huruma. Binadamu kwa kupakwa majivu, anakumbushwa kwamba,
yeye ni kiumbe cha Mungu aliyeteolewa kutoka mavumbini na mavumbini atarudi tena!
Hapa Mwenyezi Mungu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na pili ni kumheshimu binadamu
aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano ya Majivu mwaka 2014, kwa kuwataka waamini na
watu wote wenye mapenzi mema: kutubu, kujitakasa na kumwongokea Mungu katika safari
ya maisha yao ya kla siku, tayari kuadhimisha Fumbo la Pasaka, ili kumshangilia Yesu
Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Hii ni hija ambayo inajikita
katika sadaka, majitoleo pamoja na kuubeba Msalaba.
Baba Mtakatifu anasema,
hija ya Kipindi cha Kwaresima inajikita katika mambo makuu yafuatayo: Sala, kufunga
na tafakari ya Neno la Mungu linalomwilishwa katika matendo ya huruma. Mwamini anaalikwa
kudhibiti vilema na udhaifu wake, kwa kuchuchumilia neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi
Mungu kwa njia ya mazoezi ya maisha ya kiroho.
Ikumbukwe kwamba, sala ni
majadiliano kati ya Mungu na mwamini, ni nguvu imara inayomuunganisha mwamini na Muumba
wake, kwa kutambua udhaifu na mapungufu yake, kiasi cha kukimbilia huruma na upendo
wa Mungu. Kwaresima ni kipindi cha Sala inayomwilishwa katika huduma kwa maskini na
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Ni muda wa kufunga na kujinyima na
wala si kulimbikiza kile ulichojinyima, bali hii ni sehemu ya mkakati wa mabadiliko
ya ndani, unaotaka kumsaidia mwamini kuwa na moyo pamoja na huruma kama ya yule Msamaria
mwema, tayari kujisadaka kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani. Hapa waamini wanahamasishwa
kuwa na kiasi na kujinyima kwa ajili ya wengine. Kwaresima ni kipindi cha kutoa sadaka,
kwani inapendeza kutoa kuliko kupokea, waamini wajifunze kutoa kwa ukarimu!
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.