Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali, Jumatatu jioni, tarehe 16 Februari
2015 ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican,
kwa ajili ya kumwombea na kumsindikiza Marehemu Kardinali Karl Josef Becker, S.J.
aliyefariki dunia hivi karibuni. Hata katika majonzi na simanzi ni siku ya kumshukuru
Mwenyezi Mungu, aliyemwita Kardinali Becker kumfuasa Kristo katika maisha ya Ukuhani
na sasa amemwita kwake, ili kumshirikisha huruma yake.
Baba Mtakatifu Francisko
mara baada ya adhimisho la Misa Takatifu, alihitimisha kwa Ibada ya Maziko kwa ajili
ya Kardinali Becker, kielelezo cha mshikamano wa umoja na mapendo hadi dakika ya mwisho,
pamoja na kuendelea kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa shukrani kwa kazi kubwa iliyofanywa
na Marehemu Kardinali Becker katika kufundisha na kuwafunda vijana wa kizazi kipya,
lakini zaidi kwa ajili ya kuwanoa Wakleri katika maisha na utume wao. Marehemu Kardinali
Becker alijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa Kanisa la Kiulimwengu.
Kardinali
Sodano katika mahubiri yake anasema, kwa wale waliobahatika kumfahamu Marehemu Kardinali
Becker wataendelea kumkumbuka kwa kuwa kweli ni jaalim la hekima ya Kikristo, aliyoifundisha
kiasi kwamba iliangaza akili na kuupasha joto moyo wa mwanadamu, ili kufungua malango
ya maisha kwa Kristo, Mwalimu na Bwana. Ni kiongozi aliyewafunda watu mambo na upendo
wa Kimungu, ili kuweza kujiandaa barabara kukutana na Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma
na mapendo.
Kardinali Sodano anaendelea kusema kwamba, huu ndio ukweli wa
imani kwa mtu anayeamini, imani ambayo imedhihirishwa na Marehemu Kardinali Becker
katika mafundisho yake, alipokuwa anawashirikisha wanafunzi wake imani katika Fumbo
la Utatu Mtakatifu na imani katika Fumbo la Ekaristi Takatifu; sasa Marehemu Kardinali
Becker anamwona Mwenyezi Mungu uso kwa uso kama ilivyokuwa hamu ya moyo wake.
Kardinali
Sodano anawataka waamini kukesha na kuwa macho, kwa kuhakikisha kwamba, taa za maisha
yao ya kiroho daima zina mafuta ya kutosha, tayari kumpokea Bwana arusi anapokuja.
Hii ni taa ya imani ambayo daima haina budi kuwa inawaaka bila kuzimika. Marehemu
Kardinali Becker ni mfano wa kuigwa kwani anasema, onjeni na mwone jinsi Bwana alivyo
mwema na heri yake mtu yule anayemkimbilia Bwana ili kutafuta hifadhi kwake.
Ibada
hii imehudhuriwa na umati mkubwa wa Makardinali ambao wengi wao walikuwa bado wako
mjini Vatican baada ya kuhitimisha mkutano wa Makardinali pamoja na kuwasimika Makardinali
wapya ishirini waliotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.