Askofu Giovanni Innocenzo Martinelli, mwangalizi wa kitume wa Jimbo la Tripoli, Libya
ambaye kwa miaka zaidi ya arobaini amekuwa akiishi na kutekeleza utume wake nchini
Libya anasema, hata katika hali tete kiasi hiki ambako maisha ya wananchi wengi wa
Libya yako hatarini, ataendelea kubaki nchini Libya hadi kieleweke!
Anasema
ataendelea kubaki na kushikamana nao, tayari kushuhudia imani yake kwa Kristo na Kanisa
lake, hata kama itambidi kutoa sadaka ya maisha yake. Lengo ni kuwatia shime pamoja
na kuendelea kuwahudumia wagonjwa na majeruhi, kazi inayofanywa na watu wa kujitolea
wanaosimamiwa na Kanisa mahalia, wengi wao ni wahamiaji kutoka Barani Asia.
Kamwe
hataogopa kuendelea kushikamana na Wakristo ambao kwa sasa wanatishiwa maisha na wanajeshi
wenye misimamo mikali ya kiimani wanaoendelea kuvuruga Libya. Wanajeshi wa Jihadi
tayari wamekwisha tua nanga mjini Tripoli, changamoto ya kusimama kidete katika misingi
ya imani, tayari kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kina kwa njia ya ushuhuda wa
maisha bila ya kukata tamaa, ili kujenga utamaduni wa kuwapenda na kuwathamini wengine,
tayari kushirikiana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.
Vita hii inayoendelea
kutikisa ulimwengu anasema Askofu Martinelli, nyuma yake kuna sababu za kiuchumi,
wajanja wanataka kuchukua mafuta kutoka Libya pamoja na kuendelea kufanya biashara
haramu ya silaha na binadamu; jambo ambalo kwa sasa lina faida kubwa kwa watu ambao
dhamiri zao zimekufa. Kuna haja ya kuwa na ujasiri wa kushutumu njama hizi pamoja
na kuanza mchakato wa majadiliano yanayojikita katika ukweli na uwazi, ili hatimaye,
kujenga utamduni wa udugu na mshikamano.
Hii ni changamoto kubwa kwa Nchi
za Falme za Kiarabu na Jumuiya ya Kiislam, kusaidia mchakato wa kujenga na kudumisha
misingi ya haki na amani kati ya watu kwani vita haina macho wala pazia. Watu wengi
wanajiuliza, Je, ni nani ambaye anawakingia kifua hawa wanajeshi wa Jihadi, ni nani
anayewapatia fedha kiasi cha kuwa na jeuri ya kuua watu bila hata chembe ya huruma?
Bila shaka anasema Askofu Martinelli, hii ni fedha ya damu kutoka katika visima vya
mafuta huko Mashariki ya Kati.
Wakristo wahamiaji wanaoishi nchini Libya hata
katika ukimya wao wanaendelea kushuhudia imani katika matendo, kwa kuwaonjesha huruma
na mapendo, wale wote wanaoteseka kutokana na vita na kinzani za kijamii. Askofu Martinelli
anatambua fika changamoto kubwa iliyoko mbele yake na kwamba, maisha yake yako hatarini,
lakini kama Mchungaji mwema anaendeleo kuonesha ujasiri, moyo mkuu na mshikamano na
wale wanaoteseka.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.