Biashara ya silaha ni chanzo cha majanga kwa mataifa!
Katika maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kikanisa Cha Mtakatifu
Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumanne tarehe 17 Februari 2015, Baba Mtakatifu Francisko
ametolea nia ya Ibada hii ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Wakristo
waliouwawa kikatili nchini Libya.
Baba Mtakatifu katika mahubiri yake anasema
kwamba, kila mtu ana uwezo wa kutenda mema na kuachana na mabaya. Binadamu anaweza
kugeuka na kuwa mkatili kiasi hata cha kuvuruga mahusiano na udugu kati ya watu; hili
ndilo chimbuko la vita na kinzani mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika uso
wa dunia. Baba Mtakatifu anawashutumu wafanyabiashara wanaoendelea kuuza silaha kwenye
maeneo ya vita, ili kuchuma faida kubwa kwa gharama ya maisha ya watu wasiokuwa na
hatia.
Baba Mtakatifu anasema, binadamu ana uwezo wa kuharibu kazi ya uumbaji
ambayo amekabidhiwa na Mwenyezi Mungu kuilinda, kuitunza na kuiendeleza kwa ajili
ya mafao ya sasa na yale ya kizazi kijacho. Ni kutokana na kiburi na majivuno ya mwanadamu,
mauti imeingia duniani kama ambavyo Liturujia ya Neno la Mungu ilivyoonesha. Mwanadamu
anataka kujikweza na kudhani kwamba, anaweza kuwa ni sawa na Mungu.
Baba Mtakatifu
anasema, Sura kadhaa kutoka katika Kitabu cha Mwanzo zinaonesha udhalimu na dhambi
inavyojikita katika moyo wa mwanadamu, kiasi hata cha Kaini kumwangamiza ndugu yake
Abeli kutokana na wivu usiokuwa na mashiko, hapa ukawa ni mwanzo wa chuki, uhasama
na vita kati ya watu. Baba Mtakatifu anasema kwamba, leo hii asilimia kubwa ya habari
zinazotawala katika vyombo vya habari ni kuhusiana na majanga ya: vita, mauaji na
kinzani za kijamii. Hapa Baba Mtakatifu anajiuliza ni jambo gani ambalo haliendi sawa
katika moyo wa mwanadamu?
Hapa Mwenyezi Mungu anapenda kumwonesha mwanadamu
kwamba, moyo wake umejeruhiwa vibaya sana, kiasi cha mwanadamu kujitafutia uhuru usiokuwa
na mipaka hata kama ni kwa ajili ya maangamizi yake! Biashara ya silaha ni kati ya
mambo yanayochochea vita na kinzani za kijamii, kiasi hata cha kupandikiza mbegu ya
kifo ili kujipatia faida kubwa inayotokana na damu ya watu wasiokuwa na hatia.
Baba
Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuchagua kutenda mema
na kuachana na maovu; kuachana na wivu, masengenyo na uchoyo usiokuwa na mashiko kwa
ustawi na maendeleo ya watu. Hali hii imejitokeza hata miongoni mwa mitume wa Yesu,
wakaanza kusigana kwa vile walisahau kuchukua mkate!
Baba Mtakatifu anawataka
waamini kuachana na chachu ya Mafarisayo ambao ni wanafiki na Herode ambaye ni katili
na muuaji na badala yake watambue kwamba, wokovu ni neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Waamini wajitahidi kuchagua na kutenda mema kama alivyofanya Mama Theresa wa Calcutta
kwa kujisadaka kwa ajili ya maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa
jamii. Wazazi na walezi wawasaidie watoto wao kukua katika fadhila na utu wema bila
kusahau kusali na kumwomba Mwenyezi Mungu ili awaepushe na mitego ya Shetani.
Yesu
Kristo anawakumbusha wafuasi wake kwamba, amemwaga Damu yake Azizi kwa ajili ya kumkomboa
mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na kumkirimia mwanadamu uweo na nguvu
ya kutembea katika mwanga mpya wa maisha kwa njia ya majadiliano katika maisha ya
kifamilia, kijamii na kitamaduni, ili kujenga na kukuza utamaduni wa upendo na mshikamano.
Baba
Mtakatifu anawakumbusha waamini kwamba, Kipindi cha Kwaresima kinachoanza kwa kupakwa
na majivu ni muda wa neema na baraka, kamwe wasimwachie nafasi Shetani ili aweze kuwalaghai
na kuwapeleka kwenye njia ya upotofu. Waamini wawe imara na thabiti katika maisha
yao ya kila siku.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.