2015-02-16 14:50:47

Ushuhuda wa pamoja ni muhimu!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu, tarehe 16 Februari 2015 amekutana na kuzungumza na ujumbe wa Kanisa la Scotland uliomtembelea mjini Vatican kwa kuendelea kukazia umuhimu wa Wakristo kujikita katika Injili pamoja na kuendeleza umoja wa Wakristo, kwa kutambua kwamba, Scotland ni nchi ambayo ina utajiri mkubwa wa kitamaduni na kihistoria, kwa kuwa na watakatifu pamoja na mashuhuda wengi wa Kikristo.

Hali ya mchakato wa majadiliano ya kiekumene nchini Scotland inaonesha kwamba, kuna mambo mengi ambayo yanawaunganisha Wakristo kuliko hata yale yanayowagawa na kuwatenganisha, changamoto kwa Wakristo kuvuka kikwazo cha kudhaniana vibaya na kuanza kutafuta njia mpya za maelewano na ushirikiano, ili kwa pamoja kuweza kukabiliana na changamoto zinazoibuliwa katika ulimwengu mamboleo; kwa kuwa na sauti moja kwa mambo yale yanayowagusa kama Wakristo.

Katika ulimwengu wa utandawazi ambamo unaonekana kuchanganyikiwa, kuna haja kwa Wakristo kuonesha ushuhuda wa pamoja kama kikolezo cha uinjilishaji makini kwa kutambua kwamba, wote wanafanya hija ya pamoja, changamoto kubwa ni kuaminiana ili kwa pamoja kama mahujaji waweze kuutafuta uso wa Kristo. Imani na ushuhuda wa Kikristo vinakabiliwa na changamoto nyingi kiasi kwamba, umoja na mshikamano ndiyo njia pekee itakayowawezesha Wakristo kuihudumia vyema Familia ya Mungu sanjari na kumwezesha Kristo kuwafikia watu wengi zaidi.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, hija ya upatanisho na amani kati ya Makanisa haya mawili itawasaidia kuyaunganisha na kuyaweka kwa pamoja, ili kumwezesha Roho Mtakatifu kuwasaidia kuwapatia watu wengi maisha na kuzaa matunda mengi. Baba Mtakatifu anawaalika wajumbe hawa kuendelea kusindikizana katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia ya sala.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.