Sera la elimu na mafunzo ya Mwaka 2014 yazinduliwa
Ifuatayo ni hotuba ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete, wa Tanzania kwenye uzinduzi wa sera
ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014, katika Shule ya Sekondari ya Majani ya chai, Dar
es Salaam,
Leo ni siku muhimu katika historia ya maendeleo ya elimu nchini.
Tunakutanishwa kwa ajili ya kufanya jambo kubwa, la kihistoria na la kimaendeleo la
uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014. Uzinduzi wa Sera mpya unaashiria
mwanzo wa ngwe mpya katika safari ya kuimarisha, kuendeleza na kuipaisha elimu nchini
kufikia viwango vya juu vya kukidhi ubora na mahitaji ya taifa. Ni kielelezo cha utashi
na azma yetu ya kuboresha mfumo wetu wa elimu uende na wakati na kuiwezesha jamii
kuzikabili ipasavyo changamoto na maendeleo na maisha yao. Maisha bora kwa Mtanzania
yanaanzia na kutegemea uwezekano wa kila Mtanzania kupata fursa ya kupata elimu iliyo
bora, elimu itakayomuwezesha kutawala mazingira yake na kukabili changamoto za maisha.
Nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Shukuru Kawambwa, Katibu Mkuu, Prof.
Sifuni Mchome pamoja na wataalamu wenu na wadau wengine wa elimu kwa kuongoza na kusimamia
mchakato huu ulioanza kwa kupitia Sera mbalimbali zilizokuwapo katika sekta ya Elimu
na kuzihuisha kwa kuandaa Sera hii. Napenda pia kumtambua Naibu Waziri, Mheshimiwa
Anne Malechela Kilango pamoja na upya wake katika Wizara.
Mheshimiwa Waziri; Nakushukuru
pia kwa uamuzi wenu wa kuzindua Sera hii katika eneo la shule. Tunapata fursa maridhawa
ya kuoanisha kile kilichopo na kile tunachoazimia kutekeleza kwenye Sera. Nimepata
fursa ya kutembelea maabara na kuwaona vijana wetu wanavyopata elimu ya sayansi kwa
vitendo. Aidha, mnanipa nafasi ya kusema na walimu na wanafunzi ambao ndiyo wadau
wakuu wa Sera hii ya Elimu. Ni jambo la faraja kwangu kuona tulipofikia na mafanikio
tuliyoyapata, kama haya niliyoyaona katika shule hii. Inatupa kila aina ya sababu
kuongeza bidii na kasi zaidi ya kufikia malengo makubwa zaidi.
Vilevile, nakushukuru,
Mheshimiwa Waziri, kwa maneno yako ya utangulizi kuhusu Sera hii. Kama ulivyokwishasema,
Sera hii ni matokeo ya mapitio na uhuishaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995,
Sera ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya mwaka 1966 na Sera ya Taifa ya Elimu ya Juu
ya mwaka 1999. Kipindi cha zaidi ya kipindi cha miaka 14 ya utekelezaji wa sera hizo
na maamuzi mengine kuhusu elimu kimekuwa cha mabadiliko mengi ya kijamii, kiuchumi
na teknolojia ndani na nje ya nchi. Uchumi wetu umekua na kutanuka na kuzua mahitaji
mapya ya rasilimali watu na stadi mbalimbali ambazo hazikuhitajika siku za nyuma.
Aidha, mipango mitatu ya miaka mitano ya maendeleo kuelekea mwaka 2025 nayo imezaa
mahitaji mengine. Yote haya pamoja na maoni ya wadau mbalimbali yamezingatiwa katika
Sera hii ya mwaka 2014.
Hali ya Sekta ya Elimu
Mheshimiwa Waziri;Ndugu
Wadau wa Elimu; Elimu ni kitu kinachomgusa na kumhusu kila mtu hapa Tanzania. Sisi
katika Serikali, tunatambua wajibu wetu na nafasi yetu maalum kwa upatikanaji wa elimu
nchini. Kwa ajili hiyo, elimu ni jambo la kipaumbele cha juu, ni la kufa na kupona.
Ukweli wa usemi wangu huo unajihidhirisha katika uwekezaji mkubwa tunaoufanya katika
kuendeleza elimu. Bajeti ya Elimu ndiyo iliyo kubwa kuliko zote kwa miaka mingi na
imekuwa ikiongezeka. Kwa mfano, mwaka 2005/2006 zilitengwa shilingi bilioni 669.5
wakati mwaka 2014/2015 zimetengwa shilingi trilioni 3.1. Katika kipindi hicho, bajeti
ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu imeongezeka kutoka shilingi bilioni 56.1 hadi
shilingi bilioni 345. Kwa sababu hiyo idadi ya wanafunzi wanaofaidika imeongezeka
kutoka 16,345 mwaka 2005 hadi 98,000 mwaka 2014. Shule za msingi zimeongezeka kutoka
14,257 mwaka 2005 hadi 16,343 mwaka 2014 na hivyo kufanya idadi ya wanafunzi nayo
kukua kutoka milioni 7.54 hadi milioni 8.23. Kwa upande wa sekondari shule zimeongezeka
531 mwaka 2005 hadi 4,576 mwaka 2014. Idadi ya wanafunzi nayo imeongezeka kutoka 524,325
mwaka 2005 hadi 1,804.056 mwaka 2014.
Upanuzi huu mkubwa na wa kihistoria
umetokea pia kwenye vyuo vya elimu ya ufundi stadi ambapo vyuo vimeongezeka kutoka
184 hadi 744 kati ya mwaka 2005 na 2014. Kwa upande wa elimu ya juu, idadi ya vyuo
imeongezeka kutoka 26 hadi 50 kati ya mwaka 2005 na 2014 na kufanya idadi ya wanafunzi
wa vyuo vikuu iongezeke kutoka wanafunzi 40,719 mwaka 2005 hadi wanafunzi 200,986
mwaka 2014. Leo hii tunapokutana hapa, hatuna tena tatizo na fursa ya kupata elimu
kwa elimu ya msingi, sekondari, ufundi na elimu ya juu.
Mwaka 2005, urari
wa wanafunzi kati yetu na wenzetu wa Afrika Mashariki ulikuwa wa chini mno kwa upande
wetu. Kenya walikuwa na wanafunzi wa sekondari 925,341 na wa vyuo vikuu 108,407 ikilinganishwa
na Tanzania iliyokuwa na wanafunzi 524,325 wa sekondari na 40,719 wa vyuo vikuu. Uganda
ilikuwa na wanafunzi 728,393 wa sekondari na 124,313 wa vyuo vikuu. Sasa hali ni tofauti.
Kwa mwaka 2013, kwa mfano, Kenya ilikuwa na wanafunzi wa sekondari 2,104,300 na wanafunzi
wa vyuo vikuu 324,600. Katika mwaka huohuo, Uganda walikuwa na wanafunzi wa sekondari
1,362,739 na wa vyuo vikuu 140,403. Ongezeko hili linatuweka katika hali nzuri ya
ushindani tunapoelekea katika ushindani wa soko la pamoja ndani ya Afrika Mashariki
ikilinganishwa na hali ilivyokuwa miaka 10 iliyopita. Jukumu letu ni kuimarisha ubora
wa elimu yetu na hasa iwe ni ile inayokidhi mahitaji ya soko la ajira nchini, Afrika
Masharini na dunia.
Juhudi zetu hizi za kuendeleza elimu zimetambulika duniani
na kutupatia heshima kubwa zikiwemo tuzo mbalimbali. Tumekuwa nchi ya kupigiwa mfano
katika kutekeleza Malengo ya Milenia (MDGs) yanayohusu fursa ya watoto kupata elimu
ya msingi, na usawa wa kijinsi baina ya watoto wa kiume na wa kike kupata elimu ya
msingi na sekondari. Haya na mengine mazuri tuliyofanya ni mambo ya kujivunia. Ni
mafanikio yanayotokana na utekelezaji mzuri wa Sera tatu za elimu ya Msingi, Ufundi
na Elimu ya Juu zilizokuwepo.
Ndugu Wadau wa Elimu;
Mafanikio hayo
makubwa nayo yamezua changamoto mpya mbalimbali. Miongoni mwake ipo ile ya malengo
ya Elimu kuwa sawa na goli linalohama kila unapolikaribia. Hali hii haipo hapa nchini
kwetu pekee, bali ipo kote duniani. Nimebahatika kutembelea nchi nyingi na kuona yanayofanyika.
Hali kadhalika nimesoma yanayoendelea kwenye nchi mbalimbali kuhusu elimu. Ukweli
ni kwamba hakuna nchi duniani ambayo imemaliza changamoto zote zihusuzo elimu. Katika
kila nchi kuna mjadala unaoendelea kuhusu ubora wa elimu. Na, sababu ni moja, uboreshaji
wa elimu ni jambo endelevu. Iko hivyo kwa nchi zinazoendelea kama yetu na hata zile
zilizoendelea. Tofauti yetu ipo kwenye aina ya changamoto zilizopo. Nchi zilizoendelea
hazina matatizo yanayozikabili nchi zinazoendelea.
Ni jambo la kutia moyo
kuwa tangu uhuru mpaka sasa matatizo mbalimbali yanayoisibu elimu yametambuliwa na
kushughulikiwa. Katika awamu hii ya uongozi wa nchi yetu tumetoa msukumo maalum tena
mkubwa katika kutafuta majawabu ya changamoto zinazokabili sekta ya elimu nchini.
Bahati nzuri tumepata mafanikio kwenye nyanja nyingi. Nimekwishaelezea jinsi idadi
ya shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo vya ufundi na vyuo vikuu vilivyoongezeka.
Mambo hayo yameongeza sana fursa za elimu nchini. Hivi leo watoto wote wenye umri
wa kwenda shule wanaweza kuwa shule labda wakatae wenyewe au wakatazwe na wazazi au
walezi wasioona mbali. Watoto wote wanaofaulu darasa la saba wana hakika ya kwenda
sekondari na vyuo vikuu vina nafasi wazi zinazosubiri wanafunzi wenye sifa kuzijaza.
Kimsingi
tunaweza kusema kuwa suala la watoto na vijana wetu chini kupata fursa ya kupata elimu
inayolingana na umri wao siyo tatizo kubwa tena la kutuumiza vichwa. Hata hivyo, kazi
kubwa inayohitajika kuendelea kufanyika ni kuhakikisha kuwa elimu wanayopata watoto
na vijana wetu ni bora. Kwa ajili hiyo, hatuna budi kuendelea kuboresha mazingira
ya kutolea elimu. Walimu wa kutosha wawepo kwa masomo yote. Tena wawe ni walimu
wanaoyamudu vyema masomo wanayofundisha. Hali kadhalika, huduma za msingi kwa maisha
na utendaji kazi wa walimu ziboreshwe pamoja na maslahi yao. Vifaa vya kufundishia
na vile vya kusomea na kujifunzia vipatikane kwa uhakika. Majengo ya kufundishia na
huduma mbalimbali shuleni na vyuoni yawepo ya kutosha tena yaliyo bora. Pamoja na
hayo, mifumo na miundo ya uendeshaji na usimamizi wa elimu nchini iendelee kuboreshwe
zaidi na zaidi.
Sera Mpya na Matumaini Mapya
Ndugu Wadau wa Elimu; Sera
Mpya ya Elimu inatupa mwanzo mpya na matumaini mapya ya kututoa hapa tulipo sasa na
kutupeleka mbele kwenye neema na mafanikio makubwa zaidi. Mahali ambapo nyingi ya
changamoto zinazotukabili sasa zitakuwa hazipo ila zitakuwepo zile za kupeleka elimu
yetu mbele zaidi. Sera mpya inatambua umuhimu na nafasi ya elimu kwa maendeleo ya
nchi yetu na watu wake. Sera inatambua kuwa Elimu ni silaha ya ukombozi kwa Watanzania
dhidi ya umaskini na madhila yake. Ni nyenzo ya uhakika ya kutupeleka kwenye uchumi
wa kati ifikapo mwaka 2025. Kwa sababu hiyo, Sera inasisitiza umuhimu wa kuendelea
kupanua fursa kwa kila mtoto mwenye umri wa kwenda shule aende shule. Sera Mpya inatoa
dhima kwa taifa kuanza safari ya kumuwezesha kila mtoto anayeanza darasa la kwanza
aweze kupata elimu ya sekondari ya mpaka kidato cha nne. Hili ni lengo la muda mrefu
kwamba elimu ya msingi iwe mpaka kidato cha nne badala ya darasa la saba kama ilivyo
sasa. Hili ni lengo ambalo halitakamilika mara baada ya uzinduzi huu. Yanahitajika
maandalizi makubwa. Katika kuanza safari ya kuelekea huko, Serikali imeamua kufuta
ada ya elimu ya sekondari kuanzia mwaka 2016 ili wale waliofaulu kwenda kidato cha
kwanza wasishindwe kusoma.
Sera Mpya ya elimu imeweka msisitizo wa pekee kwa
kila mtoto kupata elimu ya awali kabla ya kupata elimu ya msingi. Tumedhamiria pia
kuwekeza zaidi katika stadi za Kuandika, Kusoma na Kuhesabu (KKK) katika miaka miwili
ya elimu ya msingi. Azma yetu ni kujenga msingi imara wa elimu kwa wanafunzi nchini
ambao hutegemea sana upatikanaji wa stadi hizo. Watoto wanapoimarishwa vya kutosha
kwa upande wa kusoma, kuandika na kuhesabu, aghalabu humudu vyema masomo yao shuleni.
Aidha, itasaidia kurekebisha upungufu uliopo sasa.
Ndugu Wadau wa Elimu;
Ni
ukweli ulio dhahiri kwamba ili tuweze kupata maendeleo makubwa ya kiuchumi lazima
tuongeze matumizi ya sayansi na teknolojia nchini. Tunaweza kufanya hivyo tu kwa kuwa
na wanasayansi wengi. Sera hii inasisitiza kuimarishwa kwa muundo na utaratibu wa
ufundishaji wa masomo ya Hisabati, Sayansi na Teknolojia katika ngazi zote. Kazi hii
tayari tumekwishaianza na tunaendelea nayo kwa ari na nguvu. Tumetoa msukumo mkubwa
katika ujenzi wa maabara na naamini, Juni, 2015 tutafikia malengo yetu.
Tunapanua
mafunzo ya walimu wa sayansi. Tutakapotekeleza mradi wa matumizi ya computer mashuleni
tutakuwa tumepiga hatua kubwa muhimu. Sera hii imetoa mwongozo kwa changamoto nyingine
nyingi muhimu ambazo zimetolewa maoni na wadau mbalimbali. Kwa mfano, Sera inaelekeza
sasa kutumika kwa utaratibu wa kila somo kitabu kimoja kwa shule zote badala ya utaratibu
wa awali wa kila shule kuwa na kitabu chake. Sera inatoa msisitizo kuwa elimu ni huduma
na inaelekeza kuwekwa kwa utaratibu utakaodhibiti upangaji wa ada katika shule za
binafsi kwa utaratibu wa kuweka ada elekezi (indicative fees) kwa msingi wa gharama
halisi kwa mwanafunzi (Student Unit Course).
Hii itatoa ahueni kwa wazazi
na walezi na kuwawezesha kumudu gharama za kusomesha watoto wao katika shule za binafsi.
Suala la ubora wa elimu inayotolewa tumeliwekea mkazo wa kipekee katika sera hii mpya.
Tutaimarisha mfumo wetu wa usimamizi na ukaguzi wa shule zetu kwa lengo la kuimarisha
ubora wa elimu inayotolewa. Tutajenga uwezo wa Wizara kwa kutenga fedha za kutosha
kwa shughuli za ukaguzi, kuajiri wakaguzi wa kutosha na kuwapatia vitendea kazi vya
kuwawezesha wakaguzi kufanya kazi zao kwa ufanisi nchi nzima. Madhali tumeshapata
mafanikio ya kutosha kwenye kupanua fursa ya kupata elimu, sasa tunaelekeza nguvu
zetu kwenye kusimamia ubora wa elimu inayotolewa.
Wito kwa Wadau
Mheshimiwa
Waziri; Ndugu Wadau wa Elimu;
Mafanikio yote tuliyoyapata katika Sekta ya Elimu
yamepatikana kutokana na ushirikiano wa wadau wote wakiwemo walimu, wazazi, wananchi
wetu wote na wadau wa maendeleo. Mafanikio haya hayana budi kuenziwa na kuendelezwa.
Tunapoanza utekelezaji wa Sera Mpya ya Elimu, hatuna budi kukumbushana tena wajibu
wetu na kushirikiana kufikia malengo yetu haya mapya. Mdau mkubwa wa kwanza katika
elimu ni mzazi na mlezi ambao ndiyo viongozi wa kaya wanazotoka wanafunzi wetu. Ninyi
mnao wajibu wa kipekee wa kuwahamasisha na kuwahimiza watoto wenu kupenda shule kwa
kuwajengea mazingira mazuri ya kuwawezesha kusoma. Jihusisheni na elimu ya watoto
wenu, na jengeni uhusiano na walimu wao katika kufuatilia maendeleo ya watoto wenu.
Wakati mwingine inashangaza sana kuona wazazi na walezi kutojali kujua maendeleo ya
watoto wao shuleni. Hawakagui maendeleo yao, wala hawajihusishi na kamati za elimu
za shule za watoto wao na kata wanazoishi. Njia bora ya kutatua changamoto za elimu
za nchi ni kwa kila mmoja wetu kushiriki katika kutatua changamoto zilizoko katika
shule iliyoko katika eneo lake analoishi.
Walimu ni wadau wenye wajibu wa kipekee
sana. Jukumu lao la kuwafumbua macho na kuwaongezea upeo wa ufahamu wa vijana wetu
pamoja na kuwandaa kuwa raia wema halina mfano wake. Halina badala yake. Mnafanya
kazi nzuri lakini mnatakiwa kufanya vizuri zaidi leo na siku za usoni. Elimu ni kitu
chenye unyumbufu mkubwa na mabadiliko mengi na hasa siku hizi. Lazima muende na wakati.
Ni ninyi waalimu, pengine kuliko watu wengi wengine mtakaoumba Tanzania ya kesho iliyo
bora kupitia elimu mnayowapa wanafunzi. Ninyi walimu ndiyo wa kutusaidia kuleta mabadiliko
chanya katika jamii na nchi yetu. Nawaomba sana muendelee kujizatiti katika kutambua
uzito wa majukumu yenu na kuyatekeleza. Sisi Serikalini tutaendelea kufanya kila lililo
katika uwezo wetu kuboresha maslahi yenu na mazingira yenu ya kazi.
Nawaomba
pia wamiliki wa shule, hususan shule zinazomilikiwa na mashirika ya dini na watu na
makampuni binafsi nanyi mtimize ipasavyo wajibu wenu. Tunatambua na kuthamini mchango
wenu mkubwa katika utoaji wa elimu. Nawaomba mkumbuke kuwa Elimu ni haki ya mtoto
hivyo mjiepushe na upendeleo na ubaguzi. Elimu ni huduma, hivyo mtoze ada zinazohimilika.
Aidha, hamna budi kuzingatia mitaala na miongozo inayotolewa na Wizara ya Elimu na
Taasisi zake kuhusu elimu. Serikali inawahakikishia kuwa tutaendelea kuweka mazingira
rafiki ya kuwawezesha kutimiza wajibu wenu huo wa kutoa huduma ya elimu. Ni kwa sababu
hiyo tumewatambua katika Sera hii na mmeshirikishwa kwa ukamilifu katika mchakato
wote wa kuitunga. Naomba tuendeleze ushirikiano wetu katika utekelezaji wa Sera hii.
Sina budi kuwashukuru pia wadau wetu wa maendeleo kwa michango yao muhimu iliyotuwezesha
kufikia mafanikio makubwa katika Sekta ya Elimu. Tunapowashukuru, tunawaomba waendelee
kushirikiana nasi tunapoianza safari yetu hii ya kutekeleza Sera Mpya ya Elimu. Utekelezaji
wa Sera hii utahitaji rasilimali nyingi na hivyo tutashukuru kupata mchango wao katika
kuongezea nguvu jitihada zetu. Mchango wao utatuwezesha kupata matokeo makubwa kwa
haraka.
Hitimisho
Mheshimiwa Waziri; Ndugu Wadau wa Elimu;
Ni
jambo la faraja kubwa kwangu kwamba, katika kipindi changu cha uongozi kwa ushirikiano
wetu tumeweza kupata mafanikio makubwa na ya kujivunia katika kuendeleza Elimu nchini.
Sera hii tunayoizindua leo ni mojawapo ya mafanikio hayo. Naamini kuwa tuliyoyafanya
yamechangia kwa kiasi kikubwa kuzikomboa kaya nyingi kutokana na kutoa fursa kwa watoto
wengi zaidi wa Watanzania kupata elimu ikiwa ni pamoja na watoto wa kike. Bado tunayo
kazi kubwa ya kufanya mbele yetu.
Bahati nzuri, tunayatambua na tunaendelea
kuyafanya. Sera ya Elimu tunayoizindua leo inatoa mwongozo na kutupa mwelekeo mzuri
wa namna ya kufanya yanayotakiwa kufanyika sasa na miaka 10 ijayo. Uzinduzi wa Sera
hii mpya ya elimu, na yale yaliyomo katika sera hii ni ushahidi tosha wa dhamira yangu
na ya wenzetu wote tulioshirikiana kutayarisha sera hii kuona elimu nchini ianzidi
kuimarika na kuwa bora zaidi. Napenda sasa, kwa heshima na taadhima kubwa kutamka
kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 imezinduliwa rasmi. Asanteni sana.