Sensa ya Viwanda Tanzania kutimua vumbi 23 Februari 2015
Serikali ya Tanzania imesema kuwa maandalizi ya Sensa ya Viwanda ya mwaka 2013 itakayofanyika
nchi nzima kuanzia Februari 23 mwaka huu yamekamilika hivyo wamiliki wa viwanda na
wadau mbalimbali wanatakiwa kutoa ushirikiano kwa wadadisi watakaopita katika maeneo
yao kukusanya takwimu wakati wa Sensa hiyo.
Akizungumza wakati wa hafla ya
kufunga mafunzo na kuwaapisha wasimamizi na wadadisi wa Sensa ya Viwanda ya mwaka
2013 iliyofanyika katika Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika jana jijini Dar es
salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa alisema kuwa
maandalizi ya awali ya Sensa hiyo yamekamilika yakihusisha uhamasishaji wa ushiriki
wa wenye viwanda kwenye Sensa hiyo, utoaji wa elimu kwa wadadisi na wasimamizi watakaoendesha
zoezi hilo.
Alisema kuwa kutokana na umuhimu wa Sensa hiyo wamiliki wa viwanda
katika maeneo mbalimbali watashiriki kutoa takwimu zitakazojazwa katika madodoso maalum
yaliyoandaliwa ili kuliwezesha taifa kuweka Sera na mipango ya maendeleo inayotokana
na takwimu sahihi za viwanda vilivyopo nchini. Aliongeza kuwa mafanikio ya Sensa hiyo
yatatokana na wamiliki wa viwanda kutambua na kuithamini Sensa hiyo kwa kutoa ushirikiano
wa kuwapatia takwimu sahihi wadadisi watakaopita katika maeneo yao kukusanya taarifa
zinazohusu masuala mbalimbali yakiwemo ya uzalishaji wa bidhaa na masuala ya ajira;
Dkt. Chuwa alibainisha kuwa upatikanaji wa takwimu sahihi kuhusu Sekta ya Viwanda
nchini Tanzania utaiwezesha Serikali kutambua mchango wa viwanda katika ajira, uzalishaji
na pato la taifa hivyo kuweka Sera na mipango endelevu ya maendeleo itakayoliwezesha
taifa na sekta hiyo kupiga hatua kimaendeleo.
“Sensa hii ya viwanda ni muhimu
kwa maendeleo ya nchi yetu, na mafanikio yake yatatokana na wenye viwanda kutupa ushirikiano
maana bila wao kutoa takwimu sahihi mipango ya maendeleo kuhusu viwanda haitatekelezeka
kwa sababu ya kukosa takwimu sahihi” Amesisitiza Dkt. Chuwa. Kuhusu wasimamizi na
wadadisi watakaoendesha zoezi hilo litakalofanyika kwa muda wa miezi 3, Dkt. Chuwa
aliwataka wafuate sheria, taratibu na kanuni zilizowekwa ili kuwezesha upatikanaji
wa takwimu bora.
Naye Mkurugenzi wa shughuli za Takwimu wa Ofisi ya Taifa
ya Takwimu, Aldegunda Komba akizungumza na wadadisi hao alisema kuwa wadadisi hao
wamepewa dhamana kubwa ya kutimiza lengo liliowekwa na Serikali la kuwa na takwimu
sahihi kuhusu mchango wa viwanda katika maendeleo ya taifa. “Mafunzo tuliyowapatia
kwa vitendo na nadharia yamewajengea uwezo wa kukusanya takwimu bora, tunaomba zoezi
hili mlifanye vizuri tunatarajia mtaitumia vizuri elimu mliyoipata kwa kufanya kazi
kwa umakini mkubwa kwa manufaa ya taifa letu”. Amesisitiza Bi. Komba.
Aidha,
alibainisha kuwa kukamilika kwa Sensa hiyo kutaliwezesha taifa kutambaua mchango wa
Sekta ya Viwanda katika uchumi na pato la taifa. Kwa upande wake Kamishna wa Viapo
ambaye pia ni Mwanasheria wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Oscar Mangula akizungumza
na wasimamizi na wadadisi wa Sensa hiyo aliwataka kuzingatia Sheria, kanuni na taratibu
zinazosimamia zoezi hilo.