2015-02-16 11:01:48

Familia ni kisima cha miito!


Baraza la Maaskofu Katoliki Poland katika barua yake ya kichungaji kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, linakazia umuhimu wa mshikamano kati ya familia na maisha ya kitawa, kwa kutambua kwamba, familia ni chimbuko la miito mitakatifu na mahali pa kukuza na kulelea miito hii. RealAudioMP3

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia wanasema Maaskofu, watu wengi wanamezwa mno na malimwengu, ubinafsi na uchoyo; kinzani na migawanyiko. Watawa ni mashuhuda wa maisha ya Kijumuiya na kielelezo kwamba, maisha upendo na udugu si kikwazo katika ukuaji wa mtu: kiroho na kimwili, bali ni chachu ya mshikamano wa upendo dhidi ya ubinafsi na kinzani.

Baraza la Maaskofu Katoliki Poland linabainisha kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya Familia na Maisha ya Kitawa; kuna tofauti kubwa inayojionesha katika karama za Mashirika ya kitawa na kazi za kitume, zote hizi ni kazi ya Roho Mtakatifu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa; karama hizi zinakamilishana na wala hakuna misigano.

Ni wajibu wa familia za Kikristo kuendelea kuboresha maisha na utume wao, kwa kuiga mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, bila kusahau umoja unaojikita katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Baraza la Maaskofu Katoliki Poland linahitimisha barua yake ya kichungaji kwa Familia ya Mungu nchini humo kwa kukumbusha kwamba, familia za Kikristo ni chemchemi ya miito mitakatifu ndani ya Kanisa; hapa ni mahali pa watu kujifunza, ubaba, umama na udugu kama msingi wa imani katika mchakato wa maisha ya kitawa!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.