2015-02-14 10:52:55

Kazi tumeiona!


Baraza la Makardinali katika mkutano wake wa siku mbili uliokuwa unafanyika mjini Vatican, linampongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa ujasiri wake aliouonesha katika kuanzisha mchakato wa mageuzi ndani ya Sekretarieti ya Vatican, kwani hali ya uchumi ilikuwa imefikia pabaya. RealAudioMP3

Kanisa halina budi kuendelea kujikita katika misingi ya ukweli, uwazi, uadilifu na maadili katika matumizi ya fedha na mali ya Kanisa ambayo kimsingi ni kwa ajili ya mchakato wa Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Huu ni muhtasari ambao umetolewa na Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Vatican siku ya Ijumaa na kusema kwamba, Makardinali 164 wameshiriki katika mkutano wao uliokuwa unaongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, ili kuchangia mchakato wa mageuzi unaoendelea kuvaliwa njuga na Kanisa kwa wakati huu, ili kuliwezesha Kanisa, kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara.

Makardinali wamejadili kwa kina na mapana kuhusu mada na taasisi mbali mbali za uchumi zinazosimamiwa na Vatican, chini ya uongozi wa Kardinali George Pell na Kardinali Reinhard Marx. Makardinali wamechangia mawazo kuhusu Benki kuu ya Vatican, IOR na matarajio yake kwa siku za usoni. Kimsingi Makardinali wameridhika na hatua mbali mbali ambazo zimechukuliwa kama sehemu ya mchakato wa mabadiliko katika sekta ya uchumi mjini Vatican.

Makardinali wanasema, kanuni ya ukweli, uwazi, uadilifu, weledi na maadili ni mambo msingi sana katika mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa mali ya Kanisa. Mabadiliko yanayoendelea kufanyika mjini Vatican, hayana budi kuendelezwa na kutekelezwa hata katika Makanisa mahalia na taasisi zote zinazosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa. Hizi ndizo cheche za mabadiliko zinazoletwa na Baba Mtakatifu Francisko, wanasema Makardinali, "hapa hakuna kulala hadi kieleweke"!

Makardinali wameendesha mkutano wao anasema Padre Federico Lombardi katika hali ya amani, utulivu, udugu na mshikamano, kwa kupembua kwa kina na mapana mahusiano kati ya Sekretarieti kuu ya Vatican, Makanisa mahalia pamoja na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki. Hapa Makardinali wamekazia kanuni ya auni inayoonesha huduma ya upendo inayotolewa na Sekretarieti ya Vatican kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa mahalia pamoja na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki.

Makardinali wameonesha dhamana, wajibu na utume unaopaswa kutekelezwa na Sekretarieti kuu ya Vatican, kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kuyasaidia Makanisa yale ambayo bado "yanachechemea" katika masuala mbali mbali, ili kuweza kutekeleza utume wake barabara. Muundo wa utekelezaji wa kazi za Sekretarieti kuu ya Vatican hauna budi wanasema Makardinali kujikita katika uratibu mzuri unaofumbatwa katika mshikamano wa Kikanisa na kanuni ya auni badala ya mtindo wa kuzungumza na kufanya vikao ambavyo wakati mwingine havina tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya Kanisa.

Makardinali wamesisitiza kwamba, msimamo wa Kanisa katika masuala mbali mbali na ushirikiano wa kimataifa hauna budi kuwa wazi na endelevu, kwa kuhakikisha kwamba, Mabaraza na taasisi za Kipapa zinazohusika na masuala haya zinashirikishwa kikamilifu, ili kuwa na kauli na msimamo mmoja; hali ambayo inahitaji kuratibiwa kikamilifu.

Makardinali wanasema kwamba, mchakato wa mageuzi unapania pia kupunguza idadi ya wafanyakazi, kwa kuzingatia sifa na vigezo vinavyotakiwa na kwamba, Sekretarieti ya Vatican haina budi kuonesha ile taswira ya Kanisa la Kiulimwengu kwa kuwa na wafanyakazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Nafasi ya walei, hasa wanawake ndani ya Kanisa imesisitiziwa sana na Makardinali na kwamba, mageuzi haya ni mchakato endelevu mintarafu Mafundisho ya Kanisa.

Mwishoni Makardinali wameridhia kwamba, utekelezaji wa maamuzi ambayo tayari yamekwishafikiwa unaweza kuanza taratibu, badala ya kuendelea kukaa na kusubiri kukamilisha mfumo mzima wa mageuzi, ambao kimsingi utahitaji muda mrefu zaidi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.