Baba Mtakatifu Francisko tangu alipokabidhiwa dhamana na utume wa kuliongoza Kanisa
Katoliki, alishauriwa na Makardinali kufanya mageuzi makubwa katika Sekretarieti ya
Vatican ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Kikanisa kwa kusoma alama
za nyakati. Tangu mwaka 2013 Baba Mtakatifu anajielekeza zaidi katika masuala makuu
matatu katika mageuzi haya: maboresho, udogo na ubora; mambo ambayo ni mwongozo wa
Baraza la Makardinali ambalo linaendelea kufanya kazi bega kwa bega na Baba Mtakatifu
Francisko.
Mkutano wa Makardinali uliofunguliwa Alhamisi, 12 Februari 2015
na Baba Mtakatifu unapania kutoa ushauri aminifu na endelevu utakaomwezesha Khalifa
wa Mtakatifu Petro kuliongoza Kanisa la Kristo; kwa kuzingatia ubora, ufanisi na tija,
kama alivyobainisha Askofu Marcello Semeraro, Katibu wa Baraza la Makardinali, wakati
akiwasilisha taarifa elekezi kwa Makardinali. Hii ni taarifa iliyotolewa na Padre
Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican wakati akizungumza na waandishi wa habari
mjini Vatican, siku ya Alhamisi.
Kwa upande wake anasema Padre Lombardi, Kardinali
Rodriguez Maradiaga amefafanua kwa kina na mapana: kanuni, dira na mwongozo wa mageuzi
ambayo Baba Mtakatifu anapania kufanya kwenye Sekretarieti ya Vatican. Amebainisha
asili na uwezekano wa kuunganisha baadhi ya Mabaraza ya Kipapa, ili kupunguza ukubwa
wa Sekretarieti, kwa kujikita katika ubora, tija na ufanisi. Sekretarieti kuu ya mji
wa Vatican inawajibu wa kuratibu shughuli mbali mbali zinazofanywa na Mabaraza ya
Kipapa, kumbe hapa hakuna wazo la kuanzisha tena miundo mipya.
Padre Lombardi
anabainisha kwamba, ufafanuzi wa kitaalimungu na kisheria uliotolewa unaonesha kwamba,
kuna uwezekano mkubwa wa kuunganisha mabaraza makuu mawili ambayo yanamwingiliano
wa tema pamoja na utendaji wake wa kazi: "Familia, Walei na Maisha" na upande wa pili
ni "Upendo, haki na amani.
Hapa baadhi ya Mabaraza ya Kipapa pamoja na taasisi
mbali mbali zinaweza kuunganishwa katika makundi haya mawili na hivyo kuunda Mabaraza
makuu mawili, yaani: Baraza la Kipapa la Familia, Walei na Maisha; pili ni Baraza
la Kipapa la Upendo, haki na amani.
Padre Lombardi anasema, muundo wa Kisinodi
ni kati ya mambo ambayo yanapatiwa kipaumbele cha pekee katika utekelezaji mpya wa
shughuli na mikakati ya Sekretarieti kuu; changamoto ni kuweza kuteuwa watu watakaotekeleza
dhamana hii, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa huduma na uwajibikaji. Makardinali
wanakumbushwa kwamba, mabadiliko haya ni makubwa pengine yatachukua muda mrefu zaidi
kabla ya kuanza utekelezaji wake. Hapa kuna haja ya kuunda Tume maalum itakayoshughulikia
mwongozo wa uundaji wa Mabaraza haya na hatimaye, kufanyiwa tathmini na Baraza la
Makardinali katika vikao vyake na baadaye kutolewa maoni na Makardinali, Maaskofu
na Mabaraza ya Kipapa.
Tume ya Makardinali itakuwa na dhamana ya kuandaa muswada
ambao utawasilishwa kwa Baba Mtakatifu kwa ajili ya kufanyiwa maamuzi na hatimaye,
utekelezaji wake na kwamba, baadhi ya mambo yanaweza kuanza kutekelezwa kwa majaribio
wakati ambapo Kanisa linaendelea kusubiri Waraka kamili unaobainisha mageuzi haya
ndani ya Kanisa.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.